Wednesday, July 16, 2025

‎Mwenge wazindua daraja la watembea kwa miguu Tipri Mbulu. ‎


Na John Walter -Mbulu

Mradi wa ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu Tipri lililoko kata ya Gehandu, halmashauri ya mji wa Mbulu, umeleta afueni kubwa kwa wananchi takribani 3,995, wakiwemo wanafunzi ambao sasa wanaweza kuhudhuria masomo bila usumbufu wakati wote wa mwaka.

‎Akisoma taarifa ya mradi huo wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, Meneja wa TARURA wilayani Mbulu, Mhandisi Nuru Hondo, amesema kabla ya kujengwa kwa daraja hili, wanafunzi walikuwa wanakwamishwa na mvua kwa takribani miezi saba kila mwaka, jambo lililoathiri mahudhurio na maendeleo yao kielimu.

‎Ameeleza kuwa daraja hilo kutokana na uimara wake linaweza kudumu kwa miaka 70.

‎Mwenge wa Uhuru umepokelewa wilayani Mbulu kwa ziara ya kukagua, kutembelea, kuzindua na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi mbalimbali yenye thamani ya Shilingi bilioni 44, ikiwemo miradi ya afya, miundombinu ya barabara na miradi mingine ya maendeleo.

‎Miongoni mwa miradi hiyo ni daraja hili la Tipri, ambalo linaunganisha vijiji vya Tsawa na Tipri.

‎Kukosekana kwa daraja hilo kwa muda mrefu kulisababisha wananchi kupata changamoto kubwa katika kupata huduma muhimu, hasa wakati wa mvua ambapo mto huo ulikuwa unakuwa kikwazo kikubwa. Mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi milioni 158.9.

‎Akizungumza kwenye eneo la mradi, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2025, Ismail Ali Ussi, ameipongeza halmashauri ya mji wa Mbulu kwa ubunifu na utekelezaji wa mradi huu muhimu.

‎Vilevile, ameishukuru kamati ya ulinzi na usalama kwa usimamizi mzuri wa fedha za mradi.

‎Mwenge wa Uhuru mwaka huu unaendelea na kaulimbiu isemayo: ‎"Jitokeze kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu."

Mwenge wa uhuru wazindua Mradi wa nishati mbadala Manyara Girls Sekondari



Na John Walter -Babati

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Ali Ussi, amezindua mradi wa nishati mbadala katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Manyara wenye thamani ya shilingi milioni 21.9.

‎Mradi huo unalenga kurahisisha upikaji wa chakula kwa wanafunzi pamoja na kutunza mazingira kwa kupunguza ukataji miti ovyo.

‎Kiongozi huyo amesema ni jitihada za Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya nchi na kulinda afya za Wananchi.

‎Akisoma taarifa kwa Kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru Kitaifa, Mkuu wa shule ya Manyara Girls, Bi. Gisella Msofe, amesema mradi huo wa gesi safi ya kupikia utapunguza muda wa kuandaa chakula na kuchangia jitihada za shule katika uhifadhi wa mazingira.

‎Baadhi ya wanafunzi akiwemo Sabrina Msangi, Faith Flavian na Sharon Msangi, wameishukuru serikali kwa mradi huo, wakieleza kuwa sasa watakuwa na muda zaidi wa kusoma badala ya kutumia muda mwingi kutafuta kuni, pamoja na kulinda afya zao kutokana na kupunguza moshi unaotokana na kuni na mkaa.

‎Mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuhamasisha wananchi kuachana na matumizi ya mkaa na kuni ili kulinda mazingira, ambapo serikali imeanza na taasisi zinazolisha watu kuanzia 100 na imekuwa ikitoa mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku ya shilingi 17,500.


Source

Gwajima: CCM Sihami, Tunabanana Mpaka Kieleweke



"Mimi bado ni mwanachama wa Chama cha Mapinduzi na nitaendelea kuwepo. Mimi sihami, CCM nipo sana, tunabanana humu humu ndani mpaka paeleweke pakae vizuri. CCM ni chama cha kidemokrasia kama ilivyo madhumuni ya katiba yake." - Askofu Josephat Gwajima


Tuesday, July 15, 2025

Mchambuzi Hans Rafael Amchana MO Dewji Vibaya: Asitufanye Sisi Watoto

 

Mchambuzi Hans Rafael Amchana MO Dewji Vibaya: Asitufanye Sisi Watoto


Binafsi nimemsikiliza Tajiri ila sıjaona utofauti wa kile alichoongea msimu uliopita na leo.

1. Mo anasema ametoa zaidi ya Tsh 80b,inawezekana ni kweli Ila atwambie na Yeye Simba imemtengenezea kiasi gani?….maana kila mwaka anatumia Brand ya Simba kutangaza bidhaa zake.


2. Mo amesema kila mwaka anatoa hela ya usajili ila mambo yamezidi kuwa yale yale kila mwaka Simba wanasajili Wachezaji 17 na mwisho wa Msimu wanakata 14 je Mo haoni pale Simba kuna shida ya utendaji? Kwani asiwaondoe viongozi wote wanaosajili…..? na kuajiri watu wapya wa mpira kama (Technical Director na Drector of football) ili wasimamie vizuri project na Pesa zake? Kwanini ameendelea kuwakumbatia viongozi wale wale ambao kila msimu wanafuja pesa zake kwa kusajili Wachezaji wa kawaida?


Binafsi nadhani hakuna tajiri mjinga ambae kila mwaka atakubali kupoteza hela Yake Kama hapati faida……Mo amekomaa na Simba coz anapata faida,biashara zake zinaenda,Simba ni Brand kubwa ambayo kila tajiri nchini anatamani kuitumia leo asitufanye sisi kama watoto😄


Ifike Muda matamko yakome,vitendo viongee,Simba kabla ya kupata hela ya Mo wanahitaji mfumo mpya wa katiba na viongozi Ila hawa wa Sasa sioni wakifanya Jambo

Mo Dewji : Toka Mwaka 2018 Hadi Leo Nimetumia Bilioni 87 Kwa Ajili ya Simba



"Kuanzia mwaka 2018 hadi leo nimewekeza shilingi Bilioni 45 kwa ajili ya mishahara, usajili, maandalizi ya Timu na mahitaji mengine ya uendeshaji, pia nimechangia shilingi Bilioni 20 kama sehemu ya ununuzi wa hisa asilimia 49 ndani ya Simba Sports Club na mara nyingi nimekuwa nikitoa msaada nje ya mfumo rasmi, kila palipojitokeza uhitaji wa dharura kuanzia mwaka 2017 hadi 2024 nimetumia takribani Bilioni 22 katika misaada ya dharura hivyo kufanya jumla ya mchango wangu kwa Simba kufikia shilingi Bilioni 87 hivyo kusema Mo hatoe hela ni kauli ya kupotosha yenye mwelekeo wa chuki, tuachane na fitna zisizo na msingi, tujenge palipotoboka, tuzibe ufa panapovuja na tusonge mbele bila kuonyeshana vidole" 

——— 
Mohammed Dewji, Mwekezaji na Rais wa heshima wa Simba Sports Club.

Monday, July 14, 2025

‎Mwenge wa Uhuru Waweka Jiwe la Msingi Ujenzi wa Ghala la Kuhifadhi Mazao Kiteto. ‎


Na John Walter -Kiteto 

Mwenge wa Uhuru umeweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa ghala la kuhifadhi mazao katika Wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara.

‎Taatifa ya mkuu wa wilaya ya Kiteto Remidius Mwema kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025, Ismail Ussi, imesema lengo la mradi huo ni kutoa huduma za kiutawala kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala, kuinua uchumi wa wananchi na kutoa hifadhi salama ya mazao.

‎Mradi huo unagharimu shilingi milioni 149,680,000 ambazo ni mapato ya ndani ya Halmashauri.

‎Hadi sasa mradi umefikia asilimia 70 ya utekelezaji na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kuhifadhi mahitaji ya tani kati ya 437.6 hadi 600 za mazao.

‎Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru na timu yake wameridhishwa na mradi huo na hatimaye wameweka jiwe la msingi kama ishara ya kuunga mkono jitihada hizo za maendeleo.

‎Kiongozi huyo wa Mwenge ameupongeza uongozi wa Wilaya kwa kuchukua hatua hiyo muhimu ya kuwakumbuka wakulima, akieleza kuwa kupitia ghala hilo wakulima watanufaika kwa kuhifadhi mazao yao kwa usalama na kupata fursa ya kuuza kwa bei bora kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala.

‎Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025 ni:

‎"Jitokeze kushiriki uchaguzi mkuu wa 2025 kwa amani na utulivu."

Friday, July 11, 2025

Mkoa wa Manyara Wazindua Mpango wa Usambazaji Nishati Safi ya Kupikia kwa Bei ya Ruzuku


Na John Walter -Hanang'

Katika juhudi za kulinda mazingira na kuboresha afya za wananchi, leo julai 11,2025 mkoa wa Manyara umezindua rasmi mpango maalum wa usambazaji wa nishati safi ya kupikia kwa bei nafuu kupitia ruzuku ya serikali.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika wilayani Hanang', Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewataka Wakuu wa wilaya zote tano za mkoa huo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mpango huo ili kuhakikisha unafikia malengo yaliyokusudiwa. 

Ameongeza kuwa mawakala wanaosambaza mitungi hiyo ya gesi wanapaswa kuwa waaminifu kwa kuuza kwa bei iliyoelekezwa na serikali.

Mpango huu ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa Matumizi ya nishati safi kwa kizazi cha sasa na kijacho, ambao umeanza tangu mwaka 2020 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2034, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa Mratibu wa mradi huo, Abdulrazack Mkomi, serikali imetoa ruzuku kwenye mitungi ya gesi ya kilo sita, ambapo kila wilaya imepokea mitungi 3,255. 

Wananchi wataweza kununua mtungi mmoja kwa shilingi 17,500 pekee, kwa sharti la kuwa na kitambulisho cha Taifa (NIDA).

Mradi huu una lengo la kuongeza upatikanaji wa huduma za nishati safi ya kupikia, kulinda afya za wananchi dhidi ya madhara yatokanayo na moshi wa mkaa na kuni, kuboresha uchumi wa kaya na pia kuhifadhi mazingira kutokana na kupungua kwa ukataji wa miti.

Kwa mujibu wa takwimu, jumla ya mitungi 16,275 itasambazwa kwenye wilaya zote tano za Mkoa wa Manyara, huku zaidi ya shilingi milioni 284.8 zikitumika kugharamia mradi huo.

Kwa hatua hii, serikali inatarajia kuona mabadiliko makubwa katika mtindo wa maisha ya wananchi, kupungua kwa uharibifu wa mazingira na kuongezeka kwa matumizi ya nishati salama na rafiki kwa mazingira.

Thursday, July 10, 2025

CPA Mkama azindua mfuko wa uwekezaji wa iDollar awataka Watanzania kuchamkia fursa


Katika hatua ya kimkakati ya kuimarisha uwekezaji wa ndani na kuongeza mchango wa fedha za kigeni katika uchumi wa taifa, kampuni ya iTrust Finance Limited imezindua rasmi Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja ujulikanao kama iDollar Collective Investment Scheme.

Mfuko huu utawawezesha Watanzania kuwekeza kwa kutumia sarafu za kigeni kama Dola za Marekani, Pauni za Uingereza, pamoja na sarafu nyingine za kimataifa.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, alisema kuwa mafanikio haya ni matokeo ya mazingira bora ya kisera na kisheria yaliyowekwa na serikali kupitia CMSA kwa ajili ya kukuza sekta ya masoko ya mitaji nchini.

"Mfuko huu ni nyenzo muhimu ya kuhamasisha fedha za kigeni. Unachangia katika utulivu wa uchumi na kuimarisha uwezo wa nchi kukabiliana na changamoto zinazohusiana na sarafu za kigeni. Pia unawawezesha Watanzania kuwekeza akiba zao za fedha za kigeni moja kwa moja kutoka kwenye akaunti zao za benki," alisema CPA Mkama.

Aidha, aliongeza kuwa kwa kuzinduliwa kwa mfuko huu, Tanzania inajiunga na nchi nyingine za Afrika kama Kenya, Afrika Kusini, Mauritius na Ghana ambazo tayari zina mifumo kama hii. Aliwataka Watanzania, taasisi na kampuni mbalimbali kuchangamkia fursa hii ya kukuza uwekezaji kupitia sarafu za kigeni.


CPA Mkama alifafanua zaidi kuwa Mfuko wa iDollar ni miongoni mwa mifuko ya uwekezaji wa pamoja iliyosajiliwa na kuidhinishwa na CMSA, sambamba na ile inayoendeshwa na UTT AMIS. Alisisitiza kuwa mfuko huu pia utakuwa jukwaa la Watanzania wanaoishi nje ya nchi (diaspora) kuwekeza mapato yao ya kigeni na kuchangia ukuaji wa uchumi wa ndani.

Kwa upande wake, Prof. Mohamed Warsame, Mkurugenzi Mtendaji wa iTrust Finance Limited, alisema kuwa lengo la mfuko wa iDollar ni kutoa suluhisho kwa Watanzania wengi ambao tayari wana akaunti za dola katika benki lakini wanakosa njia rasmi na yenye manufaa ya kuwekeza fedha hizo.

"Mfuko huu unawapa Watanzania fursa ya kuwekeza dola zao moja kwa moja kutoka kwenye akaunti zao na kupata mapato katika dola. Tuliona umuhimu wa kuanzisha mfuko huu kufuatia mabadiliko ya kisheria yanayokataza matumizi ya sarafu za kigeni katika miamala ya ndani kama kulipa ada za shule, kodi au huduma nyingine," Prof. Warsame alieleza.

Aliongeza kuwa kufuatia agizo hilo la kisheria, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ilielekeza kuwa sarafu za kigeni hazitakiwi tena kutumika katika miamala ya ndani, na hivyo mfuko huu unatoa njia mbadala ya uwekezaji kwa watu binafsi na taasisi zinazomiliki akiba ya fedha za kigeni.

Mfuko wa iDollar utasimamiwa na iTrust Finance Limited, taasisi iliyosajiliwa na kusimamiwa na CMSA, huku CRDB Bank ikihusika na kuhifadhi na kusimamia mali za mfuko huo kama mlezi (custodian).

Kwa uzinduzi huu, Tanzania inaendelea kuchukua hatua za kuhakikisha ushirikishwaji mpana wa wananchi katika fursa za masoko ya mitaji na kuimarisha usimamizi wa fedha za kigeni kwa maendeleo endelevu ya taifa.






 

 

Kaganda awataka vijana kuwa walinzi wa mali za Serikali Babati



Na John Walter -Babati 

Mkuu wa Wilaya ya Babati, Bi. Emmanuela Kaganda, amewataka wananchi hususan vijana kuhakikisha wanalinda na kutunza mali za Serikali, ikiwemo miundombinu ya barabara na madaraja, ili kuepusha uharibifu usio wa lazima.

Bi. Kaganda ametoa wito huo leo, tarehe 09 Julai 2025, wakati akiweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa boksi kalavati kwenye barabara ya Mamire-Qash, katika kijiji cha Ngarenaro, kata ya Galapo, tarafa ya Babati.

Mradi huo unahusisha:

  • Ujenzi wa boksi kalavati moja kubwa,

  • Makalavati madogo matatu, na

  • Uwekaji wa changarawe katika urefu wa kilomita moja.

Kwa mujibu wa taarifa iliyosomwa na Mhandisi Naftali Lyatuu kutoka TARURA wilaya ya Babati, mradi huu unagharimu shilingi milioni 272,320,400, ambazo zote zimetolewa na Serikali Kuu.

Mradi huu unatarajiwa kuboresha mawasiliano na usafirishaji kati ya kata tatu muhimu za Galapo, Mamire na Endakiso, ambazo ni maeneo makuu ya kilimo.

Bi. Kaganda ameishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu muhimu.

Kwa upande wao, viongozi wa vijiji pamoja na wananchi wamenufaika, wakiishukuru Serikali kwa kuboresha miundombinu hiyo, kwani awali kipindi cha mvua walikuwa wakikumbana na changamoto kubwa za usafiri.

Daraja hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 15 Julai 2025, wakati Mwenge wa Uhuru utakapo kimbizwa katika miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Babati.

USIENDESHE CHOMBO CHA MOTO BILA LESENI!...KARIBU BRAVO LESENI NI UHAKIKA!

 


🛑 USIENDESHE CHOMBO CHA MOTO BILA LESENI!
BRAVO INSTITUTE OF TECHNOLOGY inakuletea 🔥 Mafunzo ya Udereva kwa magari, pikipiki na bajaji — kwa mfumo wa Manual na Video Technology!

✅ Mafunzo ya kisasa
✅ Tunakusaidia kupata Leseni haraka
✅ Punguzo la 12% kwa wanaojiunga sasa!

📍 Tunapatikana: Kwa Shungu, Mbasa - Ifakara, Morogoro
📞 Tupigie sasa:
📱 0769 763 285
📱 0754 422 122
🌍 Bonyeza hapa kuwasiliana WhatsApp

🟡 LESENI NI UHAKIKA – Jiunge Leo!
📢 Tupo katika mikoa yote Tanzania


Wednesday, July 9, 2025

JAMII IELIMISHWE KUWALINDA WATOTO MITANDAONI- WAKILI MPANJU

Na WMJJWM-Dodoma.

Serikali inaendelea na juhudi kuhakikisha inawalinda Watoto dhidi ya maudhui yanayoweza kuwapotezea dira na muelekeo wa maisha mtandaoni ili kuweza kujenga taifa lenye maadili na watu wanaojitambua.

Hayo yamebainishwa na Naibu katibu Mkuu wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum, Wakili Amon Mpanju katika kikao kazi cha kamati ya Taifa ya ushauri juu ya usalama na ulinzi wa watoto mitandaoni kilichofanyika Julai 09,2025 Jijini Dodoma.

Wakili Mpanju amefafanua kwamba elimu ya kuwalinda watoto mtandaoni ni muhimu kutolewa kwa jamii hususan kwa wazazi, walezi na walimu ilikupata uelewa na wao waweze kuwekeza juhudi katika vita ya kumlinda mtoto dhidi ya madhara anayoweza kupata mtoto anapotumia vifaa vya kielektroniki ipasavyo.

"Ni lazima tuielimishe jamii juu ya mabadiliko ya teknolojia kupitia majukwaa sahihi ili kuwalinda watoto kwani wao ndiyo wanaokaa nao muda mwingi lakini vilevile utekelezaji wa sheria bila kuwa na elimu juu ya masuala haya tutakuwa hatujatimiza wajibu wetu "amesema Mpanju.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa idara ya Maendeleo ya Mtoto kutoka wizara ya Maendeleo ya Jami,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum Sebastian Kitiku amesema kikao kazi hicho kimedhamiria kukamilisha mpango kazi wa Taifa juu ya matumizi ya laini za simu za watoto ili mamlaka husika ziweze kufuatilia mienendo ya watoto na kuwa rahisi kutambua pale ambapo watoto wanapokua hatarini.

Naye mkurugenzi msaidizi kutoka Ofisi ya Rais- Tamisemi Subisya Kabuje amesema ofisi ya Rais-Tamisemi itashirikiana na Wizara ya Maendeleo yq Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum kuhakikisha watoto wanakuwa salama kupitia Kuratibu utekelezaji wa afua za kumlinda mtoto mtandaoni katika tawala za Mikoa na Serikali za mitaa kwa kuhakikisha mifumo inasomana na kurahisisha zoezi hilo.



Thursday, July 3, 2025

NEEC WAJA NA FURSA ZA KIUCHUMI KATIKA MAONEHO YA 49 YA KIMATAIFA YA BIASHARA (SABA SABA)

Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi (NEEC) linashiriki katika maonesho ya 49 ya kimataifa ya Biashara katika banda la Ofisi ya Waziri Mkuu na watakuwepo hapo kipindi chote cha maonesho ili kuwawezesha Watanzania.

Akifafanua hilo Afisa Uwezeshaji kutoka Baraza Bi. Minaeli Kilimba ameeleza kuwa wamekuja kuwaelezea watanzania juu ya Mifuko ya Uezeshaji na namna wanavyoweza kunufaika nayo na kuutarifu Umma fursa zinazopatikana katika Mifuko hiyo.

Sambamba na hilo ameeleza kuwa wamekuja sabasaba kuvitangaza vituo vya uwezeshaji takribani 28 vinavyopatikana nchini ma huduma za kiuwezeshaji zinazopatikana latila vituo husika. 'Niwaombe watanzania watembelee banda la Ofisi ya Waziri Mkuu na kufika lilipo Baraza la Taifa la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ili kuweza kupata taarifa za kiuwezeshaji kiundani zaidi' aliongeza Bi. Minaeli.

REA yatoa Mkopo wa kujenga vituo vya mafuta vijijini


Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza mpango wa kuwezesha ujenzi na uendeshaji wa vituo vipya vidogo vya gharama nafuu vya bidhaa za mafuta (petrol na dizeli) maeneo ya vijijini ili kuondoa madhara yatokanayo na njia zisizo salama.

Hayo yamebainishwa Julai 3, 2025 katika Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa (Sabasaba) Jijini Dar es Salaam ndani ya Banda la Maonesho la Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Afisa Upimaji wa REA, Hussein Shamdas.

"Katika kuhakikisha nishati bora na salama inapatikana maeneo ya vijijini REA imeendelea kutekeleza majukumu yake ikihakikisha inaandaa na kutekeleza miradi mbalimbali ukiwemo mradi huu wa kuwezesha ujenzi na uendeshaji wa vituo vidogo vya bidhaa za mafuta maeneo ya vijijini," alisema Shamdas.

Alitaja baadhi ya kadhia inayowakumbuka wakazi wa maeneo ya vijijini kufuatia kutokuwepo kwa vituo vya bidhaa za petrol na dizeli katika maeneo yao kuwa ni pamoja na gharama kubwa za upatikanaji wa bidhaa hizo tofauti na bei elekezi ya Serikali.

Mbali na suala la gharama, Shamdas alisema wakati mwingine bidhaa hizo zimekuwa zikiadimika maeneo ya vijijini kutokana na umbali uliopo kutoka kwenye vituo vya mafuta pamoja na gharama kubwa za usafiri.

"Kwa sasa uuzaji na uhifadhi wa bidhaa hizi za mafuta ya petroli na dizeli kwa vijijini sio safi na salama maana wengi wanahifadhi mapipa na madumu ya plastiki ndani ya nyumba jambo ambalo ni hatari linaweza kusababisha mlipuko na kugharimu maisha ya wananchi lakini pia sio salama kwa vyombo vya moto vinavyotumia bidhaa hizo," alisema Shamdas

Madhara mengine ambayo Shamdas aliyataja ni pamoja na athari za kiafya kutokana na kuvuta hewa isiyo safi na salama kutokana na kuhifadhi bidhaa hizo ndani ya nyumba pamoja, athari za kimazingira zinazotokana na kumwagika kwa kwa mafuta maeneo mbalimbali pamoja na kuikosesha Serikali mapato kwa kuwa wauzaji wengi wa bidhaa hizo vijijini hawalipi kodi na tozo mbalimbali za Serikali.

"Kwa kutambua athari hizi na kwa kuzingatia malengo ya Sera ya Taifa ya Nishati ya Mwaka 2015, ni wajibu wa Wakala kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa nishati na kwa bei nafuu katika maeneo yote ya nchi kwa njia iliyo salama," alibainisha.

Shamdas alitoa wito kwa wananchi kote Tanzania Bara kuchangamkia fursa ya kuomba mkopo huo ili kuweza kujenga na kuendesha vituo vya mafuta ambapo alisema mwananchi atapaswa kujaza fomu maalum na hatua zingine zitaendelea na kwamba mwongozo wa uombaji wa mkopo huo unapatikana kwenye tovuti ya wakaa ambayo ni www.rea.go.tz na pia kwa sasa mwananchi anaweza kutembelea banda la REA na kupatiwa mwongozo.

Watu 82 wachukua na kurejesha fomu za kugombea CCM Manyara



Na John Walter -Babati 

Zoezi la kuchukua na kurejesha fomu za kugombea nafasi za udiwani na ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Manyara limekamilika leo, Julai 2, 2025, saa kumi kamili jioni.

Taarifa hiyo imetolewa na Katibu wa Siasa, Uenezi na Mafunzo ya Ufundi wa CCM mkoa wa Manyara, John Zwalile, ambaye amesema jumla ya wagombea 82 wamechukua na kurejesha fomu kwa wakati katika kipindi cha siku tano kuanzia Juni 28 hadi Julai 2, 2025.

Kwa mujibu wa Zwalile, idadi ya waliorejesha fomu kwa kila wilaya ni kama ifuatavyo:

Babati Mjini – 17 (wanawake 4)

Babati Vijijini – 11 (wanawake 2)

Kiteto – 9 (wanawake 2)

Hanang' – 12 (wanawake 3, wakiwemo Mbunge wa Vijana Asia Halamga)

Mbulu Vijijini – 9 (wanawake 2)

Mbulu Mjini – 5 (wanaume pekee)

Simanjiro – 15 (wanawake 5)

Zwalile amesema hakuna malalamiko yaliyopokelewa kuanzia ngazi ya kata wakati wa zoezi hilo, jambo linalodhihirisha uelewa na utulivu miongoni mwa wanachama.

Aidha, mchakato wa kuchuja majina ya wagombea utaendelea kama ifuatavyo:

Julai 4, 2025 – Ngazi ya kata

Julai 6, 2025 – Ngazi za wilaya

Julai 7, 2025 – Ngazi za jumuiya

Zwalile ametoa wito kwa wanachama wote kuendelea kushiriki kwa amani na utulivu hadi kukamilika kwa mchakato mzima wa ndani ya chama.

Kwa idadi hiyo 82 ya watia nia ina maanisha kuwa wamekichangia Chama shilingi milioni 41 kwa kulipia shilingi laki tano kwa fomu, hiyo ni kwa majimbo pekee tofauti na zile za wawakilishi wa mkoa kupitia jumuiya mbalimbali za Chama cha Mapinduzi.

Wednesday, July 2, 2025

JUMBE AREJESHA FOMU YA UBUNGE SHINYANGA MJINI... "ZOEZI LIMEENDA VIZURI, CCM IMEWEKA MAZINGIRA BORA KWA WATIA NIA"

Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mhandisi James Jumbe Wiswa leo Julai 2, 2025 amerejesha fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho kugombea Ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Akizungumza mara baada ya kurejesha fomu katika ofisi za CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhandisi Wiswa amesema zoezi la uchukuaji na urejeshaji wa fomu limeenda vizuri na kwa utulivu mkubwa bila changamoto yoyote.


"Leo nimekuja kwa mara ya pili, hatua ya kwanza ilikuwa ni uchukuaji wa fomu, nimejaza fomu, na leo ni siku ya urejeshaji. Tumekamilisha hatua ya awali ya uchukuaji na urejeshaji wa fomu. Zoezi limeenda vizuri. Kimsingi, mimi binafsi na wala sijasikia kwa mtu mwingine kama kulikuwa na changamoto yoyote katika hatua hii," amesema Mhandisi Jumbe.

Mhandisi Jumbe amepongeza uongozi wa CCM Wilaya kwa kuweka mazingira rafiki kwa watia nia na wagombea, akieleza kuwa taratibu zimekuwa rahisi na hazichukui muda mrefu.


"Unapofika kuchukua fomu unapewa control number, unalipia, unakabidhiwa fomu na kuendelea na ujazaji na uwasilishaji. Niwapongeze Mwenyekiti wa Chama, Katibu, Sekretarieti na watumishi wengine kwa maandalizi bora," ameongeza.

FAHAD AJITOSA UBUNGE SHINYANGA MJINI KUPITIA CCM: AVUNJA UKIMYA TETESI ZA ACT-WAZALENDO

Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Fahad Gulamhafiz Mukadam akionesha fomu kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

 Mtoto wa mwanasiasa mkongwe na Meya mstaafu wa Manispaa ya Shinyanga, Mzee Gulamhafiz Mukadam, bwana Fahad Gulamhafiz Mukadam, ameibuka hadharani na kutangaza rasmi nia ya kugombea Ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza leo Julai 2, 2025 mara baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho, katika ofisi za CCM wilaya ya Shinyanga Mjini, Fahad amesema ameamua kutumia haki yake ya kikatiba na ya msingi kama mwanachama wa CCM mwenye sifa stahiki, ili kuchangia maendeleo ya wananchi wa Shinyanga kupitia nafasi ya ubunge.

"Mimi ni mtoto wa Shinyanga. Nimechukua fomu kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi kugombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini. Kama ilivyo taratibu za chama chetu, kila mwenye sifa ana haki ya kugombea. Nimetumia haki yangu ya kikatiba na natamani kushirikiana na wana Shinyanga kuleta maendeleo," amesema Fahad.

Aidha, Fahad ameweka wazi kuwa amechukua hatua hiyo kama sehemu ya kutekeleza dhamira yake ya kweli ya kuwatumikia wananchi, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira ya wazi ya kisiasa nchini.
"Kupitia uongozi wa Rais Samia, kila mmoja ameruhusiwa kusema. Mengi yamesemwa kuhusu mimi, lakini leo nimeamua kuzungumza kwa vitendo. Nipo katika ofisi za CCM, chama chenye misingi, imani na miundo imara ya kuleta maendeleo kwa Watanzania," ameongeza.

Avunja Ukimya Kuhusu Tuhuma za ACT-Wazalendo

Fahad pia ametumia nafasi hiyo kukanusha vikali taarifa zilizoenea kwenye mitandao na midomo ya watu kwamba anapanga kugombea ubunge kupitia Chama cha ACT-Wazalendo.

"Wapo wanaosema nagombea kupitia ACT-Wazalendo. Pamoja na heshima kubwa niliyonayo kwa vyama vya upinzani, sijawahi kutamka wala kufikiria jambo hilo. Ni minong'ono tu ya watu, nami leo nimejibu kwa vitendo kwa kuchukua fomu kupitia CCM," amesema.

Tetesi hizo zilianza kusambaa kwenye duru za kisiasa zikidai kuwa maandalizi ya Fahad kugombea kupitia ACT-Wazalendo . 
Hata hivyo, kwa hatua ya kuchukua fomu ya CCM, mambo yamewekwa wazi.

Kwa kufanya uamuzi huo, Fahad Gulamhafiz Mukadam amejiunga na orodha ya makada kadhaa wa CCM waliokwisha tangaza nia ya kuwania ubunge Shinyanga Mjini, huku ushindani ukiendelea kupamba moto kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 2025.


Tuesday, July 1, 2025

Naibu waziri Sillo awajulia hali majeruhi ajali ya Same.


Na John Walter -Kilimanjaro 

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Daniel Sillo, amefika katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Hospitali ya Mawenzi, na Hospitali ya Wilaya ya Same leo Juni 29, 2025, kwa ajili ya kuwapa pole na kuwajulia hali majeruhi wa ajali iliyotokea jana Juni 28, 2025, Wilayani  Same, mkoani Kilimanjaro.

Ajali hiyo iliyohusisha basi la Kampuni ya Chanel One na gari dogo aina ya Coaster (Rosa) imesababisha vifo vya watu 38 na kujeruhi watu wengine 30. Mhe. Sillo ameeleza masikitiko yake kutokana na tukio hilo na kutoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao, huku akiwatakia majeruhi uponaji wa haraka.

Katika ziara hiyo, Mhe. Sillo ameambatana na Kamanda wa Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani Tanzania, SACP William Mkonda, pamoja na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, CP Awadhi Juma ambapo wametembelea pia eneo la tukio iliyotokea ajali hiyo

Aidha, Naibu Waziri Sillo ametoa wito kwa Madereva wote kuzingatia Sheria za usalama barabarani na kuwa waangalifu wakati wote ili kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.

Mhe. Sillo ameongeza kuwa Serikali kupitia Vyombo vya Usalama itaendelea kuchukua hatua kali kwa wote watakaokiuka Sheria na Kanuni za Usalama Barabarani, ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa magari ya abiria pamoja na kutoa elimu kwa Madereva.


Picha mbalimbali wakati alipowatembelea majeruhi na eneo la tukio.










Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...