Thursday, June 25, 2026

ALIYEDANGANYA FAMILIA YA MUMEWE KUWA NI MJAMZITO AKAMATWA KWA UWIZI WA MTOTO MCHANGA LUSHOTO.

 


Na Rebeca Duwe , Lushoto.


Jeshi la polisi Mkoa wa Tanga linamshikilia mwanamke mmoja aliyejulikana kwa jina la Habiba Seleman Fundi kwa tuhuma za wizi wa mtoto mchanga katika hospitali ya wilaya ya Lushoto Mkoani Tanga.


Akithibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo Kamanda wa polisi mkoa wa Tanga  Almachius Mchunguzi alisema mtuhumiwa huyo alikamatwa mnamo tarehe 21juni mwaka huu Majira ya saa 1 usiku katika kitongoji cha Garekaya Wiliyani Lushoto akiwa na mtoto  huyo.


Kamanda Mchunguzi alisema alisema kuwa manamo juni 19 mwaka huu saa 11jioni mama mzazi wa mtoto huyo Mwanaidi Juma Nyaki mkazi wa Kijiji cha Kwemakame aliripoti kupotea kwa mwanae wa siku moja .


Aidha  aliongeza kusema kuwa mtuhumiwa huyo alitumia mbinu ya kujenga urafiki wa  karibu na mama mzazi wa mtoto huyo pamoja ndugu waliokuwa wakimhudumia hospitalini hapo.


Alisema baada ya kupata imani yao alichukua fursa hiyo na kumweka mtoto ndani ya beseni lenye nguo  kisha kutoweka na mtoto bila kufahamika kwa wakati huo.


Sambamba na hayo alisema uchunguzi wa kina umebaini kuwa mtuhumiwa alikuwa akidai kwa muda mrefu kuwa ni mjamzito na kuwahakikishia  ndugu,jama wa mume wake kuwa alikuwa akisubiri kujifungua.

 

Hata hivyo baadaya muda ameuweka kufika aliamua kufanya mpango huo wa kuiba mtoto ili kuwathibitishia madai yake kwa familia  ya mumewe na watu waliokuwa wakimzunguka kuwa alikuwa mjamzito na amejifungua.


mwisho

Wednesday, June 24, 2026

UVCCM SHINYANGA: TUSIHANGAIKE NA MATUSI YA WAPINZANI MTANDAONI, TUWAJIBU KWA MATOKEO YA KAZI

Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Shinyanga, Benson Werema, akizungumza katika kikao cha Baraza la UVCCM Mkoa wa Shinyanga kilichofanyika leo Juni 24, 2026. Picha na Kadama Malunde
Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Shinyanga, Benson Werema, akizungumza katika kikao cha Baraza la UVCCM Mkoa wa Shinyanga kilichofanyika leo Juni 24, 2026.
Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Mboni Mhita, akizungumza katika kikao cha Baraza la UVCCM Mkoa wa Shinyanga

Na Kadama Malunde - Malunde 1 Blog

Jumuiya ya Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Shinyanga imewataka vijana wake kuendelea kulinda amani, kujiepusha na mijadala ya matusi kwenye mitandao ya kijamii na badala yake kujikita katika kueleza mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Sita, kusikiliza kero za wananchi na kuzitafutia ufumbuzi kama njia bora ya kujibu hoja za wapinzani.

Wito huo umetolewa leo Juni 24, 2026 na Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Shinyanga, Benson Werema, wakati akizungumza katika kikao cha Baraza la UVCCM Mkoa wa Shinyanga, ambapo amesisitiza kuwa vijana wa CCM wanapaswa kuwa mabalozi wa amani, maendeleo na mshikamano wa taifa.

SHILATU AZINDUA MASHINDANO YA KUSAKA VIPAJI KANDA YA KUSINI, SERIKALI YAIMARISHA MKAKATI WA KUKUZA SANAA NA MICHEZO KWA VIJANA

Emmanuel Shilatu 

Na Mwandishi Wetu

Serikali imeahidi kuendelea kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuhakikisha sanaa na michezo vinakuwa nyenzo muhimu za ajira, maendeleo na ustawi wa vijana nchini.

Kauli hiyo imetolewa na Ndugu Emmanuel Shilatu wakati akimwakilisha Mkuu wa Wilaya katika hafla ya uzinduzi wa Mashindano ya Kusaka Vipaji vya Sanaa na Michezo kwa Watoto kutoka mikoa ya Kanda ya Kusini.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Shilatu alisema Serikali imeweka mkazo mkubwa katika kuibua, kukuza na kuendeleza vipaji vya wanafunzi kupitia ushirikiano na wadau wa michezo na sanaa.

"Serikali imeweka vipaumbele vyake katika kuendeleza vipawa na vipaji vya wanafunzi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo na sanaa. Hivi karibuni Serikali imeboresha mfumo wa elimu ili kuwaandaa vijana kujifunza amali mbalimbali, ikiwemo michezo na sanaa, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kujitegemea," alisema Shilatu.

Kwa upande wake, mratibu wa mashindano hayo kutoka Shirika la Compassion International alisema jukwaa hilo limeandaliwa kwa lengo la kuwapa watoto na vijana fursa ya kuonyesha vipaji vyao, kujifunza, kujijengea kujiamini na kuandaa mustakabali bora wa maisha yao.

Alisema mashindano hayo yatazingatia misingi ya haki, nidhamu, ushindani wa afya pamoja na kutoa burudani yenye viwango vya hali ya juu kwa washiriki na watazamaji.

Naye mmoja wa wazazi wa washiriki, Bi. Prisca Richard, alieleza kufurahishwa na uwepo wa kambi hiyo ya kusaka vipaji, akisema ana matumaini makubwa kuwa kipaji cha mwanae kitazidi kukua na kumsaidia kutimiza ndoto zake za baadaye.

Mashindano hayo yameandaliwa na Shirika la Compassion International na yanawakutanisha washiriki pamoja na timu kutoka mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma na Njombe.

Mashindano hayo yanatarajiwa kuhitimishwa Juni 26, 2026, ambapo mgeni rasmi wa hafla ya kufunga anatarajiwa kuwa Waziri wa Vijana, Mhe. Joel Nnauka.

Tuesday, June 23, 2026

SERIKALI YABADILI GIA, SASA KUWA RAFIKI WA BIASHARA NA SIO WADHIBITI-KAPINGA


Na mwandishi wetu, Dodoma

Waziri wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amesema Serikali imebadili mtazamo katika kusimamia sekta ya viwanda na biashara kwa kuweka mkazo kwenye uwezeshaji badala ya udhibiti, akisisitiza kuwa taasisi zilizo chini ya wizara hiyo hazitakuwa “polisi wa biashara” bali washirika wa biashara katika kukuza uchumi wa taifa.

Akichangia hoja ya Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2026/2027 Bungeni jijini Dodoma Juni 22, 2026, Mhe. Kapinga amesema sekta ya viwanda na biashara ndiyo nguzo muhimu ya kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 kutokana na uwezo wake wa kuzalisha ajira kwa vijana, kuongeza pato la taifa, kuharakisha matumizi ya teknolojia na kuimarisha biashara ya kimataifa.

Amesema wabunge wamejadili kwa kina umuhimu wa kuanzisha viwanda vipya vya kimkakati, kuvilinda viwanda vilivyopo, kuongeza ajira kwa vijana na kuimarisha mazingira ya biashara, huku Serikali ikiahidi kuyafanyia kazi mapendekezo yote yaliyotolewa.

Mhe. Kapinga amesema Bajeti ya mwaka 2026/2027 imeweka mazingira rafiki kwa wawekezaji kupitia punguzo la kodi kwa viwanda vipya, unafuu wa kodi kwenye mitambo na vifaa vya uzalishaji, pamoja na kupunguza ushuru kwa malighafi zinazotumika viwandani.

Ameeleza kuwa taasisi 13 zilizo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, zikiwemo TBS na BRELA, zina jukumu la kufungua fursa za biashara na siyo kuwa kikwazo cha ukuaji wa sekta hiyo “Sisi siyo mgambo wala polisi wa biashara, Tunataka kuwa marafiki wa wafanyabiashara, kuwaelekeza, kuwawezesha na kujenga mazingira bora ya kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”



TBS YATEKETEZA TANI 110 ZA BIDHAA HAFIFU NA ZILIZOPIGWA MARUFUKU ZENYE THAMANI YA SH. MILIONI 394

NA EMMANUEL MBATILO, PWANI

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) Kanda ya Kati limeteketeza tani 110 za bidhaa hafifu na zilizopigwa marufuku zenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 394 katika zoezi lililofanyika Juni 22, 2026, Mkuranga mkoani Pwani.

Bidhaa zilizoteketezwa zinajumuisha tani 26 za bidhaa za mitumba, ikiwemo nguo za ndani na taulo ambazo kwa mujibu wa viwango na sheria za nchi haziruhusiwi kuingizwa nchini kutokana na hatari zake kwa afya ya jamii.

Bidhaa nyingine zilizoharibiwa ni tani 8 za vipodozi vilivyopigwa marufuku, tani 3 za bidhaa za chakula zilizokwisha muda wa matumizi pamoja na kiasi cha bidhaa za rangi ambazo hazikukidhi matakwa ya viwango vya ubora.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa zoezi hilo, Meneja wa TBS Kanda ya Mashariki, Bi. Noor Meghji, alisema bidhaa hizo zilipatikana kupitia ukaguzi wa mara kwa mara unaofanywa na shirika hilo katika masoko na maeneo mbalimbali ya biashara.

Alisema katika baadhi ya maeneo walibaini uwepo wa bidhaa zilizokwisha muda wa matumizi na kuwaagiza wahusika kuziondoa sokoni na kuziteketeza ili kulinda afya za watumiaji.

Bi. Meghji amewataka wananchi kuwa makini wanaponunua bidhaa mbalimbali kwa kuhakikisha wanasoma taarifa zote muhimu zilizopo kwenye vifungashio kabla ya kufanya matumizi.

“Iwapo mtumiaji atagundua tofauti yoyote kwenye bidhaa au kipodozi anachotumia, ni muhimu kutoa taarifa kwa TBS mapema ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa,” alisema.

Aidha, alifafanua kuwa lengo la TBS si kuwaadhibu au kuwaumiza wafanyabiashara kwa kuharibu bidhaa zao, bali ni kuhakikisha sheria na viwango vinazingatiwa kwa manufaa ya umma. Alisema shirika hilo linaendelea kutoa elimu kwa wafanyabiashara na wananchi kuhusu bidhaa zilizopigwa marufuku na zile zenye viambata hatarishi.

Wakati huohuo, TBS imetoa onyo kwa wafanyabiashara wanaouza bidhaa zisizokidhi viwango vya ubora au zinazohatarisha afya ya watumiaji, ikisisitiza kuwa haitasita kuchukua hatua za kisheria dhidi ya watakaobainika kukiuka sheria kwa makusudi.

Shirika hilo limeeleza kuwa wahusika wanaobainika kuingiza au kuuza bidhaa hizo wanaweza kulazimika kugharamia zoezi la uteketezaji pamoja na kukabiliwa na hatua nyingine za kisheria kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.

TBS imesisitiza dhamira yake ya kuhakikisha bidhaa zote zinazozalishwa au kuingizwa nchini zinazingatia viwango husika kwa lengo la kulinda afya ya wananchi, mazingira ya biashara na uchumi wa Taifa.

Bi. Meghji alisema kuwa endapo bidhaa hizo zingeendelea kusambazwa na kutumika sokoni, zingeweza kusababisha madhara makubwa kwa afya za watumiaji na kuathiri ustawi wa uchumi wa nchi.

“Tunawaasa wafanyabiashara kuacha kuuza bidhaa ambazo hazikidhi matakwa ya viwango, vipodozi vilivyozuiliwa pamoja na bidhaa zilizokwisha muda wa matumizi. Wakaguzi wetu wanaendelea kufanya kazi muda wote na tunashirikiana na wananchi pamoja na vyombo vingine vya dola kuhakikisha bidhaa zote zinazopatikana sokoni zinakidhi viwango vinavyotakiwa,” alisema.


Monday, June 22, 2026

TRA YATOA MSAADA KWA WATOTO NJITI HOSPITALI YA RUFAA BOMBO KATIKA MAADHIMISHO YA. MIAKA 30

 


Rebeca Duwe Tanga 


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetoa msaada wa vifaa mbalimbali katika Hospitali ya Rufaa ya Bombo mkoani Tanga kwa ajili ya kuwasaidia watoto wenye changamoto mbalimbali, wakiwemo watoto njiti, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 ya mamlaka hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Naibu Kamishna wa Huduma za Kiufundi kutoka Makao Makuu ya TRA, Ted Silkiluwasha, alisema kuwa katika jamii ya Watanzania kuna watu wenye mahitaji maalum wanaohitaji kusaidiwa, hivyo mamlaka imeona umuhimu wa kuwafikia na kuwasaidia.






Alisema Kamishna Mkuu wa TRA, Yusuph Mwenda, amesisitiza kuwa ukusanyaji wa mapato ndio unaochangia maendeleo na kuimarisha uwepo wa taifa, hivyo ni muhimu kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma katika juhudi za maendeleo.

“Sambamba na kuimarisha taifa, hatupendi kumuacha mtu yeyote nyuma. Miaka 30 ya TRA imewezekana kutokana na walipa kodi, na mamlaka inatambua kuwa uhai wa walipa kodi ndio uhai wa TRA. Ndiyo maana tumeamua kutoa msaada huu kwa watoto njiti kama sehemu ya kurudisha kwa jamii inayochangia maendeleo ya taifa kupitia kodi,” alisema Silkiluwasha.

Aliongeza kuwa Julai 1 mwaka huu TRA itatimiza miaka 30 tangu kuanzishwa kwake, ikiwa na kaulimbiu ya “Tanzania kwa Pamoja Tunajenga Taifa Letu.” Alisema mamlaka imeona umuhimu wa kufika Hospitali ya Rufaa ya Bombo kwa kuwa inahudumia watu wenye mahitaji makubwa, ili kuwajulisha kuwa wao ni sehemu muhimu ya jamii.

Kwa upande wake, Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Castro John, alisema kuwa mamlaka hiyo inaamini kila Mtanzania ni mlipa kodi wa sasa au wa baadaye, hivyo hata watoto waliotembelewa ni walipa kodi wa kesho na pengine watumishi wa baadaye wa TRA.



Alisema mtazamo huo ndio uliowasukuma kushiriki katika shughuli za kijamii na kusaidia makundi yenye mahitaji maalum.

Aidha, alizitaka taasisi nyingine, hususan mkoani Tanga, kujitokeza kusaidia watu wenye uhitaji na kushiriki katika shughuli za kijamii zinazolenga kuwatia moyo na kuboresha maisha yao.

Naye Nuru Hamisi Omari alisema kuwa hospitali hiyo hupokea watoto njiti kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Tanga. Alieleza kuwa watoto hao hupatiwa huduma mbalimbali ikiwemo kuongeza kiwango cha sukari mwilini na kusaidiwa kupumua kwa kutumia mashine maalum hadi wanapofikia uzito unaoruhusiwa.

Alifafanua kuwa mtoto anaporuhusiwa kwenda nyumbani anatakiwa kuendelea kuhudhuria kliniki maalum ya ufuatiliaji wa ukuaji hadi atakapofikia uzito wa kilo tatu, ndipo huendelea na huduma za kawaida za kliniki.

Kwa upande wake, Muuguzi Kiongozi wa Wodi ya Watoto, Sister Rukia Mbega, ameishukuru TRA kwa kuguswa na mahitaji ya watoto njiti na kutoa msaada utakaosaidia kuboresha huduma kwa watoto hao.

Alisema msaada uliotolewa unajumuisha sabuni, nepi (pampers), dawa na makopo ya maziwa ya unga, vitu ambavyo ni muhimu katika kuwahudumia watoto njiti.


Sunday, June 21, 2026

VIJANA WANAOISHI MAZINGIRA MAGUMU WAJITENGA NA MAANDAMANO YA 7/7





Na mwandishi wetu

Wakati baadhi ya wanaharakati na watumiaji wa mitandao ya Kijamii wakihamasisha maandamano kupitia mitandao ya kijamii kuelekea Julai 7, 2026, vijana wanaoishi katika mazingira magumu ambao walijikuta katikati ya vurugu zilizotokea Oktoba 29, 2025 wameeleza namna walivyobeba mzigo mkubwa wa madhara, wakisema hawatamani kuona hali kama hiyo ikijirudia.

Vijana hao wanasema kipindi hicho kilisababisha kukosekana kwa amani, chakula, sehemu za kulala na shughuli za kujipatia kipato, huku baadhi ya wenzao wakijeruhiwa, kupata ulemavu wa kudumu na wengine kupoteza maisha.

Mmoja wao, Juma Maftah, mkazi wa Ilala Dar Es Salaam amesema siku za vurugu zilikuwa ngumu zaidi kwa watu wanaoishi mitaani kuliko kundi lolote lingine.

“Tarehe 29, 2025 wakati ule kilichotokea ilikuwa changamoto sana kwangu, amani hakuna, kula ilikuwa tabu, sehemu za kulala pia kwa sisi tunaolala nje ilikuwa changamoto sana, wengine walivunjika miguu na ndugu zetu wengine walikufa.

 Ilifika hatua mpaka tukawa tunakamata mbwa mtaani na kuwala kwa siku siku ambazo zilikuwa na ukosefu wa amani kwa sisi tunaoishi katika mazingira magumu. Mimi niombe vijana wenzangu tusikubali hata kidogo kushawishika tukaingia kwenye kufanya vurugu kwani tutaishia jela, kujisababishia ulemavu au kifo. Amani ndio kila kitu kwenye maisha,” alisema.

Kwa upande wake, Baraka Richard amesema wakati wa vurugu hizo hakuweza kufanya shughuli zake za kubeba mizigo sokoni, akiwataka Vijana wengine Nchini kutokubali kushawishiwa na wito wa kushiriki maandamano au vurugu zinazoweza kuhatarisha maisha yao, wakisema uzoefu wao unaonesha kuwa matokeo yake huacha majeraha ya muda mrefu kwa watu wa kawaida.

Ripoti ya Tume ya Uchunguzi iliyoongozwa na Jaji Mkuu mstaafu Mohamed Othman Chande kuhusu matukio ya vurugu yaliyotokea baada ya uchaguzi wa mwaka 2025 ilibainisha kuwa baadhi ya vijana wanaoishi katika mazingira magumu, maeneo ya stendi na masokoni walirubuniwa kushiriki maandamano kwa kuahidiwa fedha pamoja na ajira. 

Ripoti hiyo ilionya kuhusu matumizi ya vijana walio katika mazingira magumu kwa maslahi ya kisiasa, ikisisitiza umuhimu wa kuongeza uelewa na fursa za kiuchumi ili kuwakinga dhidi ya ushawishi unaoweza kuwaingiza kwenye migogoro na vitendo vya vurugu.

TARURA KUENDELEA KUJENGA MADARAJA YA MAWE NCHI NZIMA -SUNGURA



Na Mwandishi wetu, Dodoma

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) inaendelea na uboreshaji wa miundombinu ya barabara nchini huku serikali ikiwa imetoa takribani ya Dola Milioni 65 kwa ajili ya kurejesha mawasiliano yaliyoharibika kutokana na mvua za El Nino za mwaka 2023/2024.

Akizungumza na Wanahabari Kwenye Maadhimisho ya wiki ya utumishi wa umma mkoani Dodoma Mkuu wa kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma Tarura, Catherine Sungura amesema TARURA wanahudumia barabara za wilaya zenye urefu wa Kilomita 144,429 nchi nzima zikiwemo barabara za lami,mawe,changarawe na udongo.

Tunaendelea kujenga Madaraja nchi nzima katika kuhakikisha jamii inapata huduma za maendeleo kupitia barabara hizo hivyo kufikia sasa tunaMadaraja ya Mawe yapatayo 490 .

" Kutokana na mvua Za mwaka 2023/2024 Tarura tulipokea fedha kutoka benki ya dunia takribani ya dola Milioni 65 kwa ajili ya kurejesha mawasiliano ya barabara ambazo ziliathirika na Mvua za Elnino ambapo kwa sasa tumerudisha Mawasiliano ya barabara hizo kwa asilimia 70 katika Vijiji,Wilaya na Mikoa." Amesema Mkuu wa kitengo Sungura"

Aidha, mameneja wa mikoa hususani mkoa wa tabora wilaya ya sikonge na urambo huduma zimerejea kwa wananchi kama kawaida hivyo tarura tunaendelea kuboresha miradi mbalimbali ukiwemo mradi wa TACTIC katika miji 45 ambapo tunajenga masoko, barabara za lami na Mradi wa DMDp 2 ambao tunajenga takribani kilomita 250 katika wilaya 5 za mkoa wa Dar es Salaam.

Vilevile kwa mkoa wa Dar esalaam tuwatoe hofu Wananchi kuwa wakandarasi wamerejea kukamilisha miundombinu ya barabara hiyo hivyo Mtaa wa majohe kivule kuna kilomita 2 za barabara za zege vilevile kigamboni.

Katika Hatua nyingine tarura tumetoa ajira kwa kikundi cha maafisa usafirishaji (bodaboda) mkoani morogoro wilaya ya ifakara na ambapo wanafanya matengenezo ya kawaida ya miundombinu na hivyo wanaenda kuinuka kiuchumi kupitia miradi wa RISE.

Kwa upande wake afisa utumishi mkuu Speransia Mhapa ameongeza kuwa tarura imefanya mabadiliko mbalimbali kwenye sekta ya miundombinu nchini ambapo tunatambua katika maendeleo hayo watumishi wa umma wamekuwa na mchango mkubwa katika kukamilisha suala hilo la miundombinu.

Nitoe wito Kwa wananchi wote wanaoendelea kutembelea kwenye maadhimisho haya wafike kwenye banda la Tarura kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Wakala wa barabara za mijini na Vijijini (TARURA)

Saturday, June 20, 2026

TBA YATEKELEZA MPANGO WA NYUMBA ZA GHARAMA NAFUU KWA WANANCHI



Katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu, Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umeendelea kutekeleza mpango wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ili kuwawezesha wananchi, hususan vijana, kumudu kumiliki makazi.

Akizungumza katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kitaifa katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi wa TBA, Bi. Amina Lumuli, amesema kuwa TBA tayari imeanza kutekeleza miradi ya nyumba za gharama nafuu katika mkoa wa Dar es Salaam.

Bi. Lumuli ametaja Mradi wa Temeke Kota kuwa ni miongoni mwa miradi hiyo, akibainisha kuwa utekelezaji wa mpango huo utaendelea katika maeneo mbalimbali nchini.


"Tunawakaribisha wawekezaji kuja kushirikiana nasi ili kwa pamoja tuweze kufanikisha lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 la kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu," amesema Bi. Lumuli.

Aidha, Bi. Lumuli amesema utekelezaji wa mradi huu unatokana na dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na yenye gharama nafuu.

Amesema TBA itaendelea kuhakikisha makundi yote, yakiwemo makundi maalum, yanafikiwa na kunufaika na programu hii ya nyumba za gharama nafuu.



Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...