Wednesday, June 10, 2026

DKT. MAULID: UONGOZI WA KIMKAKATI NI MSINGI WA MAFANIKIO YA SEKTA YA ELIMU


Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt Maulid J. Maulid leo umefungua Mafunzo ya Uongozi wa Kimkakati (Strategic Leadership) kwa viongozi wa shule za sekondari wa Manispaa ya Shinyanga, yakiwakutanisha washiriki 44 wakiwemo Wakuu wa Shule za Sekondari 22 na Makamu Wakuu wa Shule 22. 

Mafunzo haya yanatolewa na ADEM kwa kushirikiana na African Centre for School Leadership (ACSL) kupitia VVOB kwa kufadhiliwa na Mastercard Foundation.

Akifungua mafunzo hayo, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, alisisitiza umuhimu wa uongozi wa kimkakati katika kuimarisha utendaji wa taasisi za umma na kufanikisha malengo ya maendeleo ya sekta ya elimu.

“Uongozi wa kimkakati ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha taasisi za umma zinafikia malengo yake kwa ufanisi. Viongozi wanapaswa kuwa na uwezo wa kutazama mbele, kupanga kwa weledi na kusimamia rasilimali zilizopo ili kuleta matokeo chanya kwa taasisi wanazoziongoza,” alisema Dkt. Maulid.

Aidha, Dkt. Maulid alieleza kuwa mafunzo hayo yanatekelezwa kwa kutumia mfumo wa kisasa wa ufundishaji unaowapa washiriki fursa ya kujifunza kwa vitendo, kubadilishana uzoefu na kupata maarifa yatakayowawezesha kukabiliana na changamoto za kiuongozi katika mazingira yao ya kazi.

“Mafunzo haya yanaendeshwa kwa mfumo wa kisasa utakaohakikisha kunakuwa na mawasiliano ya mara kwa mara, lengo kuu likiwa ni kutoa nafasi kwa washiriki kutoa mrejesho kwa wazeshaji kuhusiana na maendeleo ya utekelezaji wa mada. Tunatarajia washiriki wote watatumia kikamilifu fursa hii kujifunza na kujijengea uwezo zaidi,” aliongeza.

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu huyo alibainisha kuwa washiriki watakaofanya vizuri katika mafunzo hayo watatambuliwa na kutunukiwa vyeti, hatua inayolenga kuongeza motisha na kuhamasisha ushiriki wenye tija katika mchakato mzima wa kujifunza.

Sambamba na hilo, Dkt. Maulid alisisitiza umuhimu wa ufuatiliaji wa utekelezaji wa maarifa na ujuzi unaotolewa katika mafunzo hayo, akieleza kuwa mafanikio ya programu hiyo yatapimwa kupitia mabadiliko chanya yatakayoonekana katika usimamizi na utendaji wa shule husika.

CBE YAHUISHA MITAALA TISA KUENDANA NA TEKNOLOJIA NA MAHITAJI YA SOKO LA AJIRA


Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kipo katika mchakato wa kupitia na kuhuisha mitaala tisa ya masomo ili iendane na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023), pamoja na mahitaji ya sasa ya soko la ajira nchini.

Akizungumza Juni 10, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wa wadau uliowakutanisha zaidi ya taasisi 40, Mkuu wa Chuo cha CBE, Prof. Edda Tandi Lwoga, amesema maboresho hayo yanalenga kuhakikisha chuo kinazalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya dunia ya sasa na ya baadaye.

Prof. Lwoga amesema hatua hiyo pia inalenga kukiandaa chuo kuwapokea wanafunzi wanaotoka katika mfumo mpya wa elimu ya sekondari unaosisitiza zaidi amali na umahiri, hivyo kuhitaji mitaala inayozingatia maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya sekta mbalimbali za uchumi.

Mkutano huo ulihusisha wanataaluma kutoka vyuo mbalimbali, wawakilishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), wawakilishi wa shule za sekondari pamoja na wadau wa elimu kutoka sekta za umma na binafsi.

Ameeleza kuwa mapitio hayo pia yanazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, inayolenga kujenga uchumi shindani unaotegemea maarifa, ubunifu na matumizi ya teknolojia.

Mitaala inayofanyiwa mapitio ni pamoja na Banking and Finance, Accounting and Finance, Accounting and Taxation, Digital Marketing, Business Administration, Finance and Economics, Bachelor Degree in Business Studies, Bookkeeping na Master of Science in IT Project Management.

Katika maboresho hayo, CBE imejumuisha masuala ya Akili Mnemba (AI) katika masomo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), huku masomo ya bima yakiongezwa katika programu za fedha ili kuimarisha uelewa wa wanafunzi kuhusu sekta hiyo inayokuwa kwa kasi.

Uongozi wa chuo umesisitiza kuwa ushirikishwaji wa wadau, hususan waajiri, katika mchakato wa kuandaa mitaala hiyo utasaidia kuzalisha wahitimu wenye ushindani katika soko la ajira, wenye uwezo wa kujiajiri, kuajiri wengine na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.

Tuesday, June 9, 2026

CWM Yasisitiza Malezi ya Maadili kwa Wafanyakazi wa Majumbani


Chama wa wafanyakazi wakatoliki CWM kinaendelea na mchakato wa kutoa semina kwa wanawake wa makundi mbali ili kupaza sauti kwa jamii kutambua thamani,wajibu na haki za wafanyakazi wa majumbani 

Mkakati wa kuyafikia makundi hayo ni sehemu ya utekelezaji wa maono na misingi ya Chama hicho kuwa sauti kwa wasio na sauti hasa wafanyakazi wa majumbani ambao katika utekelezaji wa majukumu yao hukutana na vikwazo mbalimbali 

Aidha leo June 5 CWM imekutanisha kundi la wanawake wakatoliki na makundi mengine ya wanawake katika parokia ya Teule ya Mtakatifu Benedict Mkundi Jimboni Morogoro 

Miongoni mwa mambo yanayojadiliwa katika mafunzo hayo ni kukazia mchakato wa uwepo wa mikataba ya ajira kwa wafanyakazi wa majumbani, haki na wajibu wao kama zilivyo kazi nyingine 

EDSON YEYEYE ni Mratibu CWM Taifa,amewaagiza washiriki hao kuimarisha malezi ya kimaadili kwa wafanyakazi hao, ili kulinda heshima na utu wa Mfanyakazi wa nyumbani. 

Kwa upande wake Frola Ng'eni Katibu wa CHODAWU mkoa wa  Morogoro amesema mfanyakazi ana haki ya kushikishwa kujiunga na mfuko wa jamii,Nssf kwa ajili ya akiba yake ya baadaye.

Hata hivyo amesema kuwa sekta ya wafanyakazi wa majumbani ni sekta muhimu katika kukuza pato la familia na taifa, hivyo wanatakiwa kupewa haki wanazostahili bila kunyanyaswa

CWM inalenga kuyafikia makundi mengi ya wanawake Jimboni Morogoro ambapo hivi karibuni wanatarajia kukutana na kundi la wafanyakazi wa Majumbani ili kukamilisha mkakati wa kuwapeleka katika mafunzo ya ufundi stadi katika chuo cha Veta Mikumi

Wednesday, June 3, 2026

Airtel Yaongeza Uwekezaji Zanzibar, Yaingia Ushirikiano na ZECO Kuimarisha Huduma za Kidigitali

Kampuni ya mawasiliano ya Airtel Tanzania, kupitia huduma yake ya Airtel Money, imeingia mkataba wa kimkakati na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) kupitia mpango uitwao “Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali”. Ushirikiano huu unalenga kuleta mageuzi makubwa katika ununuzi na malipo ya nishati ya umeme wa mfumo wa TUKUZA visiwani humo. Kupitia mfumo huo mpya, wateja wa Airtel sasa wataweza kununua umeme wa TUKUZA kwa haraka, usalama na urahisi mkubwa kupitia simu zao za mkononi, mahali popote na wakati wowote, bila kulazmika kufika vituoni. Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini Zanzibar, Mhe. Seif Kombo Pandu, ameupongeza ushirikiano huo akitaja kuwa ni hatua kubwa kuelekea uchumi wa kidigitali na kuboresha utoaji wa huduma za umma. “Ushirikiano huu unaonesha dhamira yetu ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kisasa na zinazofikika kwa urahisi kupitia teknolojia. Umeme ni kichocheo kikuu cha uchumi wetu, ukisaidia sekta za utalii, afya, elimu, viwanda, pamoja na biashara ndogo na za kati (SMEs). Kila hatua inayorahisisha upatikanaji wake inachangia moja kwa moja katika maendeleo ya Zanzibar,” alisema Mhe. Pandu. Naibu Waziri aliongeza kuwa mpango huo unaenda sambamba na malengo ya Sera ya Nishati Zanzibar ya mwaka 2025 pamoja na Mpango wa Maendeleo ya Nishati wa Miaka 15 (2025–2040), unaolenga kuimarisha usalama wa nishati na kupunguza gharama za uendeshaji. Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Airtel Money Tanzania, Bw. Andrew Rugamba, alisema: “Kupitia ushirikiano huu na ZECO, wateja wa TUKUZA sasa wanaweza kurejesha nishati ya umeme kwenye makazi au biashara zao ndani ya sekunde chache tu. Huu ndio urahisi na ufanisi tunaotaka kuuleta kwa wananchi wa Zanzibar.” Bw. Rugamba alibainisha kuwa, kupitia kampeni ya “Airtel Kila Kona”, kampuni hiyo imeendelea kuwekeza kwa kiasi kikubwa Zanzibar. Uwekezaji huo ni pamoja na kufungua vituo vipya vya huduma katika Mkoa wa Mjini Magharibi (eneo la ZSSF Mbweni) na kituo kikubwa cha kisasa katika Jengo la Muzammil, Mlandege. Naye Meneja Mipango na Biashara wa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) Bi. Aisha Omary, alifafanua kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa shirika hilo wa kutumia ubunifu wa kidigitali kuondokana na mifumo ya kizamani ya utoaji huduma. “Huu siyo tu urahisi wa malipo, bali ni hatua kubwa ya kujenga mfumo wa nishati wenye ufanisi na unaowajumuisha wananchi wengi zaidi,” alisema Bi. Omary. Katika kuhakikisha huduma hiyo inasafiri bila vikwazo, Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), Bw. Arafat Ally Haji, aliahidi kuwa benki hiyo itahakikisha mawakala wote wa Airtel Money visiwani humo wanakuwa na ukwasi (float) wa kutosha wakati wote. “Kupitia ushirikiano wetu na Airtel, PBZ itahakikisha miamala yote, ikiwemo ununuzi huu wa umeme wa TUKUZA, inafanyika kwa haraka na ufanisi wa hali ya juu bila kukwama kwa kukosekana kwa fedha mtandaoni,” alisisitiza Bw. Arafat. Uzinduzi huu wa mpango wa “Airtel Money na ZECO – Tukuza Kidigitali” unadhihirisha nguvu ya ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi (PPP) katika kuongeza ujumuishi wa kifedha na kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.

DKT. RAJABU SEIF AIPONGEZA NEMC KWA ELIMU YA UHIFADHI WA MAZINGIRA


Ni kauli yake Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), anayeshugulikia Afya, Dkt. Rajabu Seif, alipotembelea banda la NEMC viwanja vya Jakaya Kikwete Convention Centre, Jijini Dodoma kwenye maonesho ya kuelekea maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani yanayofanyika 05/06 Kila Mwaka ambayo kwa mwaka huu yanakaulimbiu isemayo Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania.

Akiwa katika banda hilo, Dkt. Seif alipongeza juhudi za NEMC katika kuelimisha wananchi kuhusu masuala ya uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.

Alisema kazi inayofanywa na NEMC ina mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa jamii kuhusu wajibu wao wa kulinda mazingira na kuhakikisha rasilimali za asili zinatunzwa kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Katika banda hilo, wananchi wanapata elimu kuhusu umuhimu wa kufanya Tathmini ya Athari kwa Mazingira na Jamii, umuhimu wa upandaji miti, utenganishaji wa taka kuanzia kwenye chanzo, pamoja na dhana ya taka sifuri inayolenga kupunguza uzalishaji wa taka na kuongeza matumizi ya mbinu za urejelezaji.

Dkt. Seif alisisitiza kuwa ushirikiano kati ya NEMC, taasisi mbalimbali na wananchi ni muhimu katika kufanikisha agenda ya uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira nchini inafanikiwa kwa maendeleo endelevu

Tuesday, June 2, 2026

Breaking : UMMY MWALIMU ALAMBA UTEUZI..SASA MSHAURI WA RAIS SAMIA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, amemteua Bi. Ummy Ally Mwalimu kuwa Mshauri wa Rais anayeshughulikia Masuala ya Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dkt. Moses Kusiluka, uteuzi huo umetangazwa leo Juni 2, 2026 kupitia Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu.

Bi. Ummy Mwalimu ni mmoja wa viongozi wenye uzoefu mkubwa katika utumishi wa umma nchini, akiwa amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za uwaziri katika Serikali ya Tanzania. Katika kipindi cha uongozi wake, amewahi kuhudumu katika sekta za afya, mazingira, Wizara ya Katiba na Sheria pamoja na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

VINGOZI WA DINI WATAKIWA KUWA MSTARI WA MBELE KATIKA MALEZI.


 Na Rebeca Duwe Tanga 


 Viongozi wa Dini wametakiwa kushirikiana na Jamii kwa kuzingatia suala la malezi ya watoto na vijana ili kuweza kupata kizazi kilicho bora katika jamii kwa maslahi mapana ya taifa kwa ujumla.


Haya aliyasema mwanyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga ustdh Rajabu Abdrahman wakati akizungumza na waandishi wa habari wilayani Pangani katika kijiji cha Stahabu Pwani wakati dua ya kuombea dua ya kuwaombe ndugu waliotangualia mbele ya haki, ambapo alisema Suala la malezi na makuzi ya watoto ni jukumu la jamii kuweza kushirikia na viongozi wa dini ili kupata jamii ambayo ina msimamo mzuri wa kiimani na kimaadili.


Aidha Mwenyekiti Rajabu alisema kwamba ni vyema kushirikiana na viongozi wa Dini ili waweze kukemea mmomnyoko wa maadlii uliokitithiri katika Jamii kwani kwa kufanya hivyo itasaidia kupunguza wimbi la wahalifu na kuwa na jamii salama.


"Viongozi wa dini wana nafasi kubwa ya kuijenga jamii salama kwa kuwa wao ndio wanakaa na watu kwenye nyumba za ibada hivyo tukashirikana nao wote kujenga kizazi kijacho kwa kuweza kuwakemea maadili mabovu ili tuwe na kizazi kijacho "

alisema Mwenyekiti Rajabu. 


Hata hivyo Mwenyekiti Rajab alisisitiza umuhimu wa malezi bora katika jamii hasa viongozi wa dini kuwa mstari wa mbele kukemea uovu kwa sababu ndio nguvu kazi ya baadaye na viongozi wa baadaye kwa aajili ya jami ijayao.


Kwa upande wake Mkuu Balozi Batilda Burian alimpongeza Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tanga kwa kufanya jambo la kuwaunganisha viongozi mbalimbali kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa na nje ya mkoa kwa ajili dua ya kuwombea ndugu waliotangulia mbele ya haki.

Friday, May 29, 2026

MADIWANI WAASWA KUWA CHACHU YA MAENDELEO KISHAPU NA KUEPUKA MGONGANO WA MASLAHI

 Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga

Na Stella Herman,Shinyanga

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi, amewataka madiwani kusimamia kwa umakini miradi ya maendeleo katika maeneo yao huku akisisitiza kuwa wao ndiyo wawakilishi wa wananchi na nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa.

Akizungumza  wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani kuhusu kujiepusha na vitendo vya rushwa, kubaini mianya ya rushwa pamoja na kuwakumbusha maadili na wajibu wao, Masindi amesema viongozi hao wanapaswa kuwa chachu ya mabadiliko kwa kuwajibika ipasavyo katika maeneo wanayoyaongoza.

Amesema wananchi wanawategemea madiwani kuwasimamia na kuwawakilisha vizuri, hivyo wanapaswa kuangalia changamoto zilizopo katika kata zao na kuchukua hatua kwa wakati ili kuhakikisha maendeleo yanapatikana.

“Wananchi watawapima baada ya miaka mitano kwa kazi mtakazozifanya, Maendeleo ya kata yanawategemea ninyi, msipofanya maamuzi sahihi kata zenu haziwezi kupata maendeleo,” amesema Masindi.

Aidha amewataka madiwani kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, nidhamu pamoja na kutunza siri za vikao na majukumu yao, akieleza kuwa dhamana waliyopewa ni kubwa ndiyo maana Serikali imeamua kutoa mafunzo hayo ili kuwakumbusha wajibu wao kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mwendesha Mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu ambaye pia ni wakili  Maximilian Kyabona, amewaasa madiwani kujiepusha kutanguliza maslahi binafsi mbele na kusahau kuwa wao ni wawakilishi wa wananchi.

Kyabona amesema madiwani ndiyo watakaowezesha Halmashauri ya Kishapu kupata maendeleo iwapo watawajibika ipasavyo, kupinga rushwa na kufichua mianya yote inayoweza kusababisha miradi ya maendeleo kushindwa kutekelezwa.

Alitaja baadhi ya mambo ambayo madiwani wanapaswa kuyaepuka kuwa ni pamoja na kubadili vifungu vya matumizi ya fedha, kuchukuliana posho pamoja na kujihusisha na zabuni mbalimbali zinazoweza kuleta mgongano wa maslahi.


Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kishapu Josephat Limbe akizungumza wakati wa mafunzo kwa madiwani yaliyotolewa na TAKUKURU
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kishapu Atuganile Stephen akifuatilia mafunzo ya madiwani
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga

Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kishapu Josephat Limbe akizungumza wakati wa mafunzo kwa madiwani yaliyotolewa na TAKUKURU
Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kishapu Atuganile Stephen 
amesema mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha madiwani wajibu wao pamoja na suala la maadili katika kusimamia miradi na kujiepusha kutanguliza mbele maslahi yao binafsi badala ya kuwatumikia wananchi waliowachagua.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...