Monday, April 13, 2026

SEKTA YA VIWANDA YASHIRIKIANA NA VETA, ENABEL KUANDAA WATAALAMU


Ushirikiano kati ya VETA, Enabel na kiwanda cha Kasulu Sugar umeanza kuzaa matunda baada ya vijana 36 waliokuwa wakifanya kazi bila vyeti kutathminiwa na kupatiwa vyeti kupitia mfumo wa urasimishaji wa ujuzi (RPL).

Meneja Rasilimali Watu wa Kasulu Sugar, Samweli George Aoram, amesema hayo wakati Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, alipotembelea kiwanda hicho Aprili 9 hadi 10, 2026.

Amesema hatua hiyo imechangiwa na ushirikiano thabiti baina ya taasisi hizo, akibainisha kuwa pia wanafunzi 20 kutoka VETA Kasulu wanaendelea na mafunzo kwa vitendo kiwandani hapo huku wakichangia uzalishaji.

Aoram amesema kampuni iko tayari kuendeleza ushirikiano huo ili kupata wataalamu wenye ujuzi unaoendana na mahitaji ya kazi.

Naye Meneja wa Mradi wa Wezesha Binti kutoka taasisi ya Enabel, Christine Karungi, amesema lengo ni kuelewa mahitaji ya waajiri ili kuhakikisha mafunzo yanayotolewa yanatatua changamoto za ajira kwa vijana.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amesema ushirikiano kati ya taasisi za mafunzo na viwanda ni nguzo muhimu katika kuzalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji halisi ya soko la ajira.

Amesema ziara hiyo imelenga kujionea mahitaji ya ujuzi viwandani na kuimarisha ushirikiano utakaosaidia kuboresha mitaala ya mafunzo ili iendane na mazingira ya kazi.

Amefafanua kuwa kupitia ushirikiano huo, VETA inalenga kuandaa mitaala inayozingatia mahitaji ya waajiri pamoja na kuongeza fursa za mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi.

“Ushirikiano wa karibu na viwanda utatusaidia kuandaa wahitimu watakaoanza kazi moja kwa moja bila kuhitaji mafunzo ya ziada,” amesema.

Aidha, amesema hatua hiyo inawajengea uwezo wakufunzi kwa kuwapatia uzoefu wa teknolojia za kisasa viwandani, hali inayoongeza ufanisi wao wanaporejea kufundisha.

TANESCO Hanang Yapokea Gari Jipya la Kisasa Kuimarisha Huduma za Umeme





Na John Walter -Hanang'

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Wilaya ya Hanang’ mkoani Manyara limepokea gari jipya aina ya Isuzu FRR lenye mitambo ya kisasa kwa ajili ya kuboresha huduma za umeme wilayani humo.

Gari hilo limekabidhiwa leo rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Hanang’, Almish Hazal, katika hafla iliyofanyika kwenye ofisi za TANESCO Hanang’.

 Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Hazal amesema gari hilo lina uwezo mkubwa wa kubeba vifaa vizito, kubadilisha nguzo pamoja na transfoma kwa urahisi, hivyo litasaidia kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya TANESCO.

Hazal amesema kuwa hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuboresha huduma za umeme, akieleza kuwa vijiji vyote 96 vya Wilaya ya Hanang’ tayari vimepata umeme, na sasa juhudi zinaelekezwa kwenye vitongoji 116 vilivyopo katika kata 33 za wilaya hiyo.

“Gari hili litasaidia sana utendaji kazi wa TANESCO, hasa kuwafikia wananchi kwa haraka pale changamoto za umeme zinapotokea,” amesema Hazal.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa TANESCO Wilaya ya Hanang’, Mhandisi Mwitondi Charles Rugembe, amesema kabla ya kupatikana kwa gari hilo walilazimika kukodi gari kwa gharama kubwa, hali iliyoongeza matumizi yasiyo ya lazima.

“Awali tulikuwa tunakodi gari na kutumia gharama kubwa, lakini sasa serikali imeokoa fedha hizo kupitia upatikanaji wa gari hili jipya,” amesema Rugembe.

Ameongeza kuwa gari hilo litasaidia kupunguza changamoto ya kukatika kwa umeme mara kwa mara, kwani sasa wataalamu wataweza kufika kwa wakati kwenye maeneo yenye hitilafu na kufanya matengenezo haraka.

Naye Mbunge wa Jimbo la Hanang’, Asia Halamga, amesema kuwa TANESCO wilayani humo tayari imepata gari la kutembelea pamoja na gari hilo jipya la kazi nzito, jambo linaloonesha dhamira ya serikali katika kuboresha miundombinu ya huduma za umeme.

Asia amewataka wananchi kuendelea kumuombea Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ili aendelee kupeleka miradi zaidi ya maendeleo katika Wilaya ya Hanang’.


Saturday, April 11, 2026

BAYI: AMANI NDIO MUHIMILI WA MAFANIKIO KATIKA MICHEZO

 

Amani na michezo vimetajwa kuwa ni vitu vyenye uhusiano wa karibu, ambapo kila kimoja kinakiimarisha kingine katika kujenga jamii na taifa imara.

 Michezo hustawi zaidi katika mazingira yenye utulivu, huku ikiwa ni chombo muhimu cha kukuza umoja, mshikamano wa kijamii, na maelewano miongoni mwa watu wenye asili na tamaduni tofauti. 

Kupitia michezo, jamii hujenga jukwaa la pamoja lenye ushindani unaoambatana na heshima, nidhamu, na urafiki, hali inayopunguza hofu na kuongeza kuaminiana.

Mmoja wa wanamichezo mashuhuri na sauti yenye heshima duniani katika riadha, Filbert Bayi, anaamini kuwa amani na michezo haviwezi kutenganishwa. 

Katika mahojiano maalum, Bayi ambaye amewahi kushikilia rekodi ya dunia, alibainisha kuwa hakuna nchi inayoweza kukuza vipaji vya michezo bila kuwepo kwa amani na utulivu. Alisisitiza kuwa michezo si burudani pekee, bali ni chanzo kikubwa cha ajira, huduma za kijamii, na undugu miongoni mwa watu wa mataifa mbalimbali.

Bayi alieleza kuwa amani huweka mazingira rafiki kwa wanamichezo kufanya mazoezi na kuonesha vipaji vyao bila hofu ya usalama. 

Alitolea mfano Tanzania kama kioo cha namna amani inavyochochea maendeleo ya michezo, kwani wanamichezo wana nafasi ya kushindana katika hali ya utulivu. Aliongeza kuwa katika ngazi ya kimataifa, michezo imekuwa ikitumika kupunguza uhasama kati ya mataifa yaliyowahi kuwa kwenye migogoro, akitolea mfano wa mataifa hayo kutembea pamoja wakati wa ufunguzi wa michezo mikubwa.

Mbali na hayo, Bayi alikumbusha tukio la kihistoria la kususia michezo ya Olimpiki ya mwaka 1976 kupinga ubaguzi wa rangi kama ujumbe wa kusisitiza haki, usawa, na amani. Alihitimisha kwa kutoa rai kwa serikali, vyombo vya michezo, na jamii kwa ujumla kuendelea kuwekeza katika michezo kama njia ya kukuza amani, hasa kwa vijana. Alisisitiza kuwa kudumisha amani na umoja ndiyo siri ya kujenga Tanzania imara na yenye ustawi kwa vizazi vijavyo.

CCM MKOA WA TANGA YAWAPA MWEZI MMOJA VIONGOZI WA JIJI LA TANGA KUHAKIKSHA SOKO LA MGANDINI LINABORESHWA NA KUIMARISHWA USAFI.


 Na Rebeca Duwe Tanga


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga na mjumbe wa kamati kuu ya Halmashauri kuu ya CCM TaifaRajab Abdurhaman ametoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.


Hayo aliyasema wakati wa ziara yake ya kufuatilia utekelezajia wa magagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo lilipo jijini Tanga ambapo viongozi wa jiji walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali .

Aidha alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu katika soko hilo ili kuweza kuondoa changamoto ya tope kwa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.


Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Chama cha Mapinduzi.


“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.


Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.


Sambamba na hayo wa Mwenyekiti CCM Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.


“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.Rajab


Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.


Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.


Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.


Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.


Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.


Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.


Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.


Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.


Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.


Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.


Kwa upande wake, Naibu Meya ambaye pia ni Diwani wa kata ya mwanzange ambalo eneo lililopo soko hilo, Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Friday, April 10, 2026

AMANI NI SILAHA YA KUTIMIZA NDOTO NA MAONO YETU- MSIGWA



Na mwandishi wetu, Dodoma

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Gerson Msigwa amesisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kuendelea kufanya kazi kwa bidii pamoja na kulinda na kudumisha amani na mshikamano uliopo nchini kama msingi muhimu unaoweza kumsaidia kila Mmoja kuweza kutimiza ndoto na maono waliyo nayo kwa maendeleo na ustawi wa mtu mmoja mmoja, familia na Taifa kwa ujumla.

Msigwa ameyasema hayo wakati akizungumza ma Chombo kimoja cha habari Mjini Dodoma leo Jumamosi Aprili 10, 2026, akisisitiza kuwa hata matarajio, matamanio na mipango iliyo kwenye Dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 hayawezi kufikiwa bila ya amani, utulivu na mshikamano wa jamii utakaowezesha sekta binafsi na kila Mtanzania kujielekeza katika kuendeleza shughuli za kiuchumi na Kijamii.

"Hatuwezi kufanya kazi kama nchi haina utulivu, niwaombe Watanzania tulinde amani, utulivu na mshikamano wetu kwa gharama yoyote kwani ndoto hizi kubwa za kufikia matarajio na matamanio yetu zitatimia ikiwa tuna amani, utulivu na mshikamano." Amesema Msigwa.

Msemaji huyo wa serikali amesisitiza kuwa Dira 2050 katika kutimiza lengo la kuwa na uchumi wa Dola za Marekani trilioni moja unategemea sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 na sekta ya Umma kwa asilimia 30 pekee, hivyo badala ya kupoteza muda kubishana na kushughulika na mambo ya maana, Msigwa ameomba kila Mtanzania kujielekeza katika uzalishaji mali na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo nchini zikivutia zaidi kutokana na amani na utulivu uliopo nchini Tanzania.

Thursday, April 9, 2026

SAMAMBA ATOA WITO GST KUBORESHA MAZINGIRA YA KAZI, KUIMARISHA USHIRIKIANO


Na Mwandishi Wetu - Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, ameitaka Menejimenti ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kuhakikisha inajenga mazingira rafiki ya kazi yatakayowawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kujisikia salama kazini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi la GST uliofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, Eng. Samamba amesema mazingira bora ya kazi ni msingi muhimu wa kuongeza tija, ubunifu na ufanisi katika utumishi wa umma.

Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuiwezesha GST kuwa kitovu cha takwimu za jiosayansi zenye ubora na zinazopatikana kwa urahisi kwa wadau mbalimbali.

“Ni wajibu wa kila mtumishi kutekeleza majukumu aliyopewa kwa weledi na kuchangia kikamilifu mafanikio ya taasisi,” amesema Eng. Samamba.

Aidha, amewataka watumishi kuimarisha mshikamano, umoja na ushirikiano kazini, akibainisha kuwa hali hiyo itaongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na kuinua hadhi ya utumishi wa umma.
Katika hatua nyingine, Eng. Samamba amewapongeza viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi la GST, akieleza kuwa baraza hilo lina jukumu muhimu la kushauri uongozi juu ya ufanisi wa kazi, mipango ya maendeleo, pamoja na kuboresha ustawi wa wafanyakazi.

Amebainisha kuwa majukumu ya baraza yanajumuisha pia kujadili mipango ya mapato na matumizi, kupanga mikakati ya maendeleo ya taasisi, na kuimarisha ushirikiano kati ya wafanyakazi na uongozi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa GST, Eng. Ally Samaje, amesema taasisi hiyo itaendelea kuboresha utendaji wake ili kuchangia kikamilifu maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Ameongeza kuwa GST imejipanga kuboresha huduma zake za jiosayansi na maabara, sambamba na kuendana na mabadiliko ya teknolojia, ili kutoa matokeo yenye tija kwa uchumi wa taifa.

Wednesday, April 8, 2026

TRA TANGA YAVUKA MALENGO KATIKA UKUSANYAJI WA MAPATO NDANI YA MIEZI TISA KUANZIA JULAI 2025 HADI MACH 2026.


 MAMLAKA ya mapato (TRA)mkoani Tanga imeweka rekodi mpya ya ukusanyaji wa mapato baada ya kukusanya jumla ya Shilingi Bilioni 406.17 katika kipindi cha miezi tisa (Julai 2025 – Machi 2026), ikiwa ni ongezeko la asilimia 137 ya lengo lililowekwa.


Katika kipindi hicho, Mkoa ulikadiriwa kukusanya kiasi cha Shilingi Bilioni 296.3, ambapo ufanisi huo mkubwa uliovuka lengo kwa takriban Shilingi Bilioni 110, umetajwa kuwa ni matokeo ya ushirikiano wa karibu kati ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), walipakodi, na vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Tanga.


Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa, Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Castro John, amewashukuru walipakodi wa Tanga kwa kulipa kodi kwa hiari na kushirikiana na taasisi mbalimbali kama Chama cha Wafanyabiashara (JWT) na Chama cha Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA).


"Huu ni ufanisi mkubwa ambao haujawahi kutokea. Tunamshukuru Mkuu wa Mkoa na vyombo vya usalama kwa kuhakikisha mazingira ya ukusanyaji kodi yanakuwa salama. Sifa hizi ni za walipakodi wa Tanga ambao wamekuwa wasikivu na wazalendo kwa nchi yao," alisema John.


Licha ya mafanikio hayo, John ametoa onyo dhidi ya wafanyabiashara wanaotumia njia zisizo rasmi (njia za panya) kuingiza bidhaa nchini. Alibainisha kuwa bidhaa za magendo siyo tu zinaikosesha serikali mapato, bali ni hatari kwa afya ya mlaji kwani hazijapita katika taasisi za udhibiti wa ubora.


Aliongeza kuwa operesheni dhidi ya magendo zinaendelea na wafanyabiashara kadhaa wameshakamatwa na kutozwa faini kubwa (Penalties), huku akisisitiza kuwa chombo chochote kitakachokutwa kimebeba bidhaa za magendo kitataifishwa kulingana na sheria. Aidha, aliwataka wananchi kudai risiti za EFD na wafanyabiashara kutoa risiti halali katika kila manunuzi.


Meneja huyo, amewahimiza wafanyabiashara kutumia Bandari ya Tanga ambayo sasa inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kutoa mizigo kwa wakati, jambo linalochochea ukuaji wa biashara mkoani hapa.


Kuhusu wafanyabiashara wenye madeni makubwa, TRA imewataka kufika ofisini kwa ajili ya majadiliano (Negotiations) ili kuwekewa utaratibu wa kulipa kwa awamu. Mamlaka hiyo imebainisha kuwa imeweka "Dawati la Wafanyabiashara" kwa ajili ya kutoa elimu na kusaidia kukuza biashara ndogo ziweze kufikia hatua ya kuwa walipakodi wakubwa.


Meneja huyo ametoa wito kwa wafanyabiashara kujitokeza kukadiriwa mapato yao ili kuepuka changamoto wakati wa zoezi la ukaguzi barabarani.

Tuesday, March 24, 2026

DUNIA YAIPIGIA SALUTE TANZANIA: TUZO ZA STANBIC JIJINI LONDON NI JIBU KWA WANAOBWABWAJA MITANDAONI



Wakati baadhi ya watu wakitumia muda wao kwenye mitandao ya kijamii kubwabwaja na kupotosha kuwa uchumi wa Tanzania unayumba, jumuiya ya kimataifa imetoa jibu la kishindo kupitia sekta ya fedha. Tuzo tatu za kimataifa alizotunukiwa Mtendaji Mkuu wa Stanbic Tanzania, Manzi Rwegasira, jijini London nchini Uingereza, ni kielelezo tosha kuwa mfumo wetu wa kifedha uko imara na unaheshimika duniani.

Jarida la Euromoney, ambalo ni mamlaka ya juu ya tathmini ya kibenki duniani, haliwezi kuipa Benki ya Stanbic tuzo ya Benki Bora ya Kimataifa kwa mwaka wa pili mfululizo kama mazingira ya biashara na usalama wa shilingi yetu yangekuwa shakani. Hii ni tafsiri ya wazi kuwa Tanzania ina watu wenye akili na weledi wanaosimamia misingi ya fedha, na si kama inavyochorwa na "wapiga kelele" wa kidijitali.

Ushindi huu ni salamu kwa wawekezaji kuwa shilingi ya Tanzania na mfumo wake wa kibenki ni sehemu salama ya kuweka na kukuza mali. Kitendo cha Stanbic kutajwa kuwa Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalumu (Private Banking) kinaonyesha uwezo wa kipekee wa kuunganisha uchumi wa ndani na masoko ya dunia.

Hii ina maana kuwa, licha ya changamoto za kiuchumi zinazoikumba dunia kwa sasa, Tanzania imefanikiwa kujenga "daraja la kifedha" linalowawezesha wateja kukuza mali zao nje ya mipaka kwa usalama. Heshima hii tuliyoipata jijini London inathibitisha kuwa sera zetu za kifedha zinaaminika na majopo huru ya wataalamu wa kimataifa, jambo linalowapa imani washirika wa maendeleo na wafanyabiashara wakubwa duniani.

Aidha, Tuzo ya Benki Bora kwa Kizazi Kijacho iliyonyakuliwa na Stanbic ni ujumbe mzito kwa mustakabali wa biashara za Kitanzania kuelekea Dira ya 2050. Hii inaashiria kuwa kuna maandalizi ya dhati ya kuwavusha warithi wa mali na vijana kusimamia uchumi kwa uwajibikaji.

Tunapoona taasisi zetu zikishinda tuzo za namna hii, tafsiri yake ni kwamba uchumi wetu haujajengwa kwa kubahatisha, bali kwa mikakati inayolenga uendelevu wa vizazi. Ni uthibitisho kuwa Tanzania inapiga hatua kubwa katika namna mali zinavyoundwa na kusimamiwa, ikijitofautisha na mataifa mengine yanayokumbwa na migogoro ya usimamizi wa rasilimali.

Kwa upande wa huduma kwa wateja, tuzo hiyo ya tatu inashindilia msumari kwenye ukweli kwamba mabenki yetu yameacha kufanya kazi kama ofisi za kutoa fedha tu, bali yamekuwa washauri wa kimkakati wa maamuzi ya kifedha. Huu ni ushindi wa kila Mtanzania anayeamini katika maendeleo ya nchi yake.

Hii inatupa picha kuwa Tanzania ipo sawa na mataifa mengine makubwa duniani katika kutoa huduma za kiwango cha juu. Hivyo, badala ya kusikiliza upotoshaji wa mitandaoni unaodai "Tanzania haiwezekani," tuzo hizi za Euromoney Private Banking Awards 2026 ni kioo kinachoonyesha kuwa Tanzania inawezekana na inasonga mbele kwa kasi ya ajabu katika anga za kimataifa.

Mafanikio haya ya Stanbic Tanzania ni heshima kwa nchi na ni kigezo cha tathmini kuwa uchumi wetu unaenda vyema chini ya usimamizi makini.

Tunapokuwa na benki zinazong'ara London, maana yake ni kwamba soko letu la fedha limekomaa na lina ushindani unaohitajika kuvuta mitaji mipya. Ni wakati wa Watanzania, hasa vijana, kuacha kuyumbishwa na maneno ya mitandaoni na badala yake waone fahari na fursa zilizopo katika mfumo wetu wa kifedha uliopata baraka za dunia. Tanzania inaheshimika, shilingi yetu inalindwa na weledi, na mustakabali wa mali za Watanzania upo katika mikono salama na ya kisasa.





Labels:Habari



SHARE:








COMMENTSBLOGGERFACEBOOK: DISQUS





WEEK TRENDING

Monday, March 23, 2026

MIRADI YA SHILINGI BILIONI 85 KUCHOCHEA USHIRIKIANO WA TANZANIA NA AUSTRIA


Tanzania na Austria zimekubaliana kuimarisha ushirikiano wa kimaendeleo kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati yenye thamani ya Euro milioni 30 (takriban Shilingi bilioni 85), itakayolenga sekta za elimu, usalama na ufundi.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Munde, Machi 23, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa mazungumzo na ujumbe kutoka Austria ulioongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko. Amesema ziara hiyo imekuja wakati muafaka ambapo Tanzania inahitimisha Dira ya Maendeleo ya 2025 na kuanza mchakato wa Dira mpya ya 2050.

Mhe. Munde amebainisha kuwa Austria imekuwa ikifadhili miradi muhimu kupitia mikopo nafuu inayochangia moja kwa moja maendeleo ya wananchi, ikiwemo mradi wa ukarabati na uwekaji wa mifumo ya kisasa katika Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Karume (KIST) Zanzibar pamoja na maboresho ya mfumo wa elimu visiwani humo. Miradi mingine ni ukarabati wa Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) pamoja na ununuzi na usambazaji wa magari ya kuzima moto na vifaa vya uokoaji Zanzibar.

Aidha, Mhe. Munde amewasilisha salamu za shukrani kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisisitiza kuwa Austria ni mshirika wa maendeleo anayeaminika na kwamba Tanzania iko tayari kuimarisha ushirikiano huo kwa lengo la kuinua hali ya kijamii na kiuchumi ya wananchi.

Kwa upande wake, Balozi Dkt. Liko amepongeza ushirikiano huo madhubuti na kuahidi kuwa Austria itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta za utalii na viwanda ili kuongeza tija ya kiuchumi kwa pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, pande zote mbili pia zimejadili utekelezaji wa Mkakati wa Austria na Afrika wa mwaka 2026–2029 unaolenga kuimarisha amani na usalama, kukuza uchumi wa kijani, kukabiliana na uhamiaji haramu huku ikiimarishwa mifumo ya uhamiaji wa kisheria na wenye tija, pamoja na kuendeleza sayansi na elimu.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...