Monday, May 11, 2026

TUME YATEUA WAGOMBEA 17 UCHAGUZI MDOGO JIMBO LA ISMANI



Na. Mwandishi Wetu, Ismani
Wagombea 17 wameteuliwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi kugombea ubunge Jimbo la Ismani lililopo Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Mkoani Iringa.

Uteuzi huo umefanywa kwa niaba ya Tume na Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo la Ismani, Ndugu. Caroline Angwen Otieno leo tarehe 10 Mei, 2026.


Wagombea walioteuliwa na vyama vyao kwenye mabano ni Ndugu. Emmanuela Kaganda Mtatifikolo (CCM), Ndugu. Farida Issa Mwapungu (MAKINI), Ndugu. Asha Athumani Chuma (UPDP), Ndugu. Protas Shaibu Mgimbila (CCK), Ndugu. Fidelis Daud Mtikile (SAU), Ndugu. Hadija Husen Makawa (ADA-TADEA) Ndugu. Zavely Raurent Seleleka (UDP) na Ndugu. Subira Majuto Kalolo (NLD).


Wengine ni Ndugu. Bernard George Mwingira (DP), Ndugu. Burton Emilyo Chetenge (NCCR-Mageuzi), Ndugu. Mbalinga Christian Thomas (N.R.A), Ndugu. Mark Isdory Mhemela (AAFP), Ndugu. Nassim Yahaya Upete (CUF), Ndugu. Mwaka Lameck Mgimwa (TLP), Ndugu. Asma Abdallah Othman (UMD), Ndugu. Maimuna Martin Lumato (ADC) na Ndugu. Daudi Issa Masasi (CHAUMMA).


Akizungumza baada ya uteuzi huo, Msimamizi wa Uchaguzi wa Jimbo hilo, Ndugu. Caroline Angwen Otieno amesema kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume,


Kampeni kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa Jimbo la Ismani pamoja na kata 12 za Tanzania Bara zitaanza kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika siku ya Jumatatu tarehe 01 Juni, 2026.


Baada ya hatua hii ya uteuzi, kinachofuata ni kubandika fomu za uteuzi eneo la wazi kwa ajili ya kuwapa fursa ya kuweka pingamizi wale wanaoruhusiwa kuweka pingamizi kwa mujibu wa sheria.


Baada ya saa 24 kupita na endapo hakutakuwa na pingamizi wagombea hao 17 wataendelea na kampeni kuanzia kesho tarehe 11 hadi 31 Mei, 2026 na uchaguzi utafanyika tarehe 01 Juni, 2026, amesema.


Kata 12 za Tanzania Bara zitakazofanya uchaguzi mdogo wa Udiwani ni Mzimuni iliyopo Manispaa ya Kinondoni; Zongomera, Manispaa ya Kahama; Itilo, Halmashauri ya Mji wa Nzega; Ketare, Halmashauri ya Mji wa Tarime na Nyumbigwa, Halmashauri ya Mji wa Kasulu.


Nyingine ni kata ya Kala iliyoko Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi; Ziba, Halmashauri ya Wilaya Igunga; Kamsisi, Halmashauri ya Wilaya ya Mlele; Nyamugali, Halmashauri ya wilaya ya Buhigwe; Namasakata Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru; Bwongera, Halmashauri ya Wilaya ya Chato na Kibiti Halmashauri ya Wilaya ya Kibiti.

















Data na huduma za Airtel Money zapaisha mapato ya Airtel Africa, faida ikikua zaidi ya mara mbili

Matumizi ya intaneti (data) na huduma za fedha kupitia simu yamekuwa injini kuu ya ukuaji wa mapato ya Airtel Africa, huku kampuni hiyo ya mawasiliano ikitangaza ongezeko kubwa la mapato na faida kwa mwaka ulioishia Machi 31, 2026, kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya huduma za kidijitali katika masoko yake 14 Afrika.

Kampuni hiyo imesema faida halisi imepanda zaidi ya mara mbili hadi dola milioni 813 kutoka dola milioni 328 mwaka uliopita, ikiwa imechangiwa na ongezeko la mapato ya uendeshaji na faida za ubadilishaji wa fedha za kigeni. 

Mapato yamepanda kwa asilimia 29.5 hadi dola bilioni 6.42 kwa thamani ya ripoti, huku ukuaji wa sarafu thabiti ukiwa asilimia 24.

Airtel Africa imesema mafanikio haya yamechochewa zaidi na ongezeko kubwa la matumizi ya data na huduma za Airtel Money, vinavyoendelea kubadili muundo wa mapato yake na kuongeza matumizi ya wateja.

Mkurugenzi Mtendaji, Sunil Taldar, amesema matokeo haya yanaonyesha “msingi imara wa biashara na utekelezaji wenye nidhamu,” akibainisha kuwa matumizi ya huduma za kidijitali na uwekezaji wa mtandao ni nguzo kuu za ukuaji wa kampuni.

“Mkakati wetu umeleta ongezeko la rekodi la wateja, mapato na faida kabla ya kodi na riba (EBITDA),” amesema Taldar. “Data na huduma za fedha mtandao ni injini muhimu ya ukuaji wetu katika kuongeza upatikanaji wa huduma za kidijitali barani Afrika.”

Idadi ya wateja wa Airtel Africa imeongezeka kwa asilimia 10.5 hadi milioni 183.5, ikiwa ni ongezeko kubwa zaidi kuwahi kurekodiwa na kampuni hiyo. Wateja wa huduma za data wamefikia milioni 84.2, huku matumizi ya simu janja yakipanda hadi asilimia 49.5, jambo lililochochea ongezeko la matumizi ya data.

Matumizi ya data kwa kila mteja yameongezeka hadi GB 8.9 kwa mwezi kutoka GB 7.0 mwaka uliopita. Mapato ya data yamepanda kwa asilimia 35.2 kwa sarafu thabiti, na kuifanya kuwa chanzo kikuu cha mapato ya kampuni.

Huduma za Airtel Money nazo zimeendelea kukua kwa kasi, ambapo wateja wameongezeka kwa asilimia 21.3 hadi milioni 54.1. Thamani ya miamala kwa mwaka imepanda kwa asilimia 49 na kufikia zaidi ya dola bilioni 215 katika robo ya nne ya mwaka wa fedha.

Kampuni imesema mapato ya Airtel Money yameongezeka kwa asilimia 28.4 kwa sarafu thabiti, yakichochewa na matumizi ya malipo ya kidijitali, huduma za wafanyabiashara na miamala ya kimataifa.

Faida kabla ya riba, kodi na makato (EBITDA) imepanda kwa asilimia 30.4 kwa sarafu thabiti hadi dola bilioni 3.16, huku kiwango cha faida kikifikia asilimia 49.3 kutokana na udhibiti wa gharama na ukuaji wa mapato.

Airtel imesema ongezeko la matumizi ya data na huduma za fedha limeisaidia kampuni kukabiliana na changamoto za mfumuko wa bei na mabadiliko ya sarafu katika baadhi ya nchi, hususan Nigeria.

Faida ya uendeshaji imepanda kwa asilimia 45.1 hadi dola bilioni 2.12, huku faida kwa hisa moja (EPS) ikipanda hadi senti 18.6 kutoka senti 6.0 mwaka uliopita.

Uwekezaji wa mtaji umeongezeka kwa asilimia 31.9 hadi dola milioni 884, ukiwa umeelekezwa katika upanuzi wa mtandao, ikiwemo ujenzi wa zaidi ya vituo 3,250 vipya na kuongeza kilomita 3,200 za nyaya za fiber.

Airtel inatarajia kuongeza uwekezaji hadi takribani dola bilioni 1.1 mwaka wa fedha 2027 ili kuimarisha miundombinu ya kidijitali na huduma za mtandao wa kasi.

Mtandao wa 4G sasa unapatikana katika asilimia 98.5 ya vituo vyote, huku zaidi ya vituo 3,100 vya 5G vikiwa vinafanya kazi katika masoko sita.

Taldar amesema teknolojia ya akili bandia (AI) na kidijitali imeboresha huduma kwa wateja na kuongeza ufanisi wa ndani ya kampuni kupitia matumizi ya programu ya MyAirtel.

Airtel Money na huduma za data zimeendelea kuwa nguzo kuu za ukuaji wa kampuni, huku mkakati ukiwa ni kuongeza ujumuishaji wa kifedha na kidijitali barani Afrika, ambapo kiwango cha upatikanaji wa huduma za benki bado ni cha chini.

Kampuni pia inaendelea kupanua ushirikiano wa kimkakati, ikiwemo mradi wa mawasiliano ya satelaiti na SpaceX kupitia Starlink Direct-to-Cell, unaolenga kufikisha huduma katika maeneo ya vijijini yasiyo na mtandao wa kawaida.

Airtel Africa inaendelea kuwa na mtazamo chanya wa ukuaji licha ya shinikizo la gharama za nishati, ikibainisha kuwa mahitaji ya huduma za kidijitali bado yako juu katika masoko yake.

Wednesday, May 6, 2026

Picha : SIMANZI SHINYANGA, MAMIA WAJITOKEZA KUMZIKA VICTORY SENGE, AZIKWA KWA HESHIMA KUBWA

Mume wa marehemu Victory Emmanuel Senge, Bw. Victor, akishiriki kushusha jeneza lenye mwili wa mkewe wakati wa mazishi yaliyofanyika Mjini Shinyanga. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Mume wa marehemu Victory Emmanuel Senge, Bw. Victor, akiweka udongo katika kaburi la mkewe wakati wa maziko yaliyofanyika Mjini Shinyanga.
Mume wa marehemu Victory Emmanuel Senge, Bw. Victor, akiweka shada la maua katika kaburi la mkewe wakati wa mazishi yaliyofanyika Mjini Shinyanga.
Baba mzazi wa marehemu Victory Emmanuel Senge, Mchungaji Emmanuel Senge, akizungumza wakati wa ibada ya mazishi ya binti yake iliyofanyika Mjini Shinyanga.
Baba mzazi wa marehemu Victory Emmanuel Senge, Mchungaji Emmanuel Senge, akizungumza wakati wa ibada ya mazishi ya binti yake iliyofanyika Mjini Shinyanga.
Wafanyakazi wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa marehemu Victory Emmanuel Senge wakati wa shughuli za mazishi zilizofanyika Mjini Shinyanga.
Victory Emmanuel Senge enzi za uhai wake
Victory Emmanuel Senge enzi za uhai wake
Victory Emmanuel Senge enzi za uhai wake

****
Mamia ya waombolezaji wamejitokeza kushiriki mazishi ya marehemu Victory Emmanuel Senge (35) yaliyofanyika Mjini Shinyanga, kufuatia kifo chake kilichotokea Jumamosi Mei 2, 2026 katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza, alikokuwa akipatiwa matibabu baada ya changamoto za uzazi.

Ndugu, jamaa, marafiki, wafanyakazi wenzake pamoja na wakazi wa Shinyanga wamejitokeza kwa wingi katika eneo la Bushushu, Mwalugoye, leo Jumatano Mei 6, 2026  kushiriki ibada ya kumuaga na safari ya mwisho ya marehemu ambaye alikuwa akiheshimika kwa wengi kutokana na utu wake na mchango wake kwa jamii.

Marehemu Victory alikuwa Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga, ambapo alihudumu kwa weledi mkubwa na kujenga mahusiano mazuri na wateja pamoja na jamii kwa ujumla.

Mbali na kazi yake serikalini, marehemu pia alikuwa mfanyabiashara aliyefanikiwa na mmiliki wa maduka ya nguo ya Victorious yaliyopo Ngokolo Mjini Shinyanga, jambo lililomfanya kugusa maisha ya watu wengi kupitia ajira na huduma zake.

Ibada ya kuaga mwili ilianza nyumbani Mwalugoye kabla ya kuendelea katika Kanisa la TAG PCC Bushushu, ambako waombolezaji walipata nafasi ya kutoa heshima zao za mwisho na kumuombea marehemu.

Baada ya ibada hiyo, mwili wa marehemu ulisindikizwa kwenda makaburini Bushushu yaliyopo Barabara ya Shy Park ambako ulizikwa huku simanzi na huzuni vikitawala kwa waombolezaji wengi waliohudhuria.

Wengi waliomfahamu wameeleza kushtushwa na kifo chake, wakimtaja kuwa alikuwa mtu mwenye upendo, mchapakazi, mwenye moyo wa kusaidia na aliyekuwa karibu na jamii.

Kifo cha Victory Senge kimeacha pengo kubwa kwa familia, ndugu, jamaa, marafiki na jamii ya Shinyanga kwa ujumla, huku akikumbukwa kwa uchapakazi wake, moyo wa kujituma na mchango wake mkubwa katika maendeleo ya jamii.
Mwili wa Victory Emmanuel Senge ukiwa nyumbani kwake Bushushu Mjini Shinyanga
Mwili wa Victory Emmanuel Senge ukitolewa nyumbani kwake Bushushu Mjini Shinyanga kwa ajili ya kupelekwa Kanisani
Mwili wa Victory Emmanuel Senge ukiwasili Kanisani
Mwili wa Victory Emmanuel Senge ukiwa Kanisani



Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...