Saturday, April 11, 2026

BAYI: AMANI NDIO MUHIMILI WA MAFANIKIO KATIKA MICHEZO

 

Amani na michezo vimetajwa kuwa ni vitu vyenye uhusiano wa karibu, ambapo kila kimoja kinakiimarisha kingine katika kujenga jamii na taifa imara.

 Michezo hustawi zaidi katika mazingira yenye utulivu, huku ikiwa ni chombo muhimu cha kukuza umoja, mshikamano wa kijamii, na maelewano miongoni mwa watu wenye asili na tamaduni tofauti. 

Kupitia michezo, jamii hujenga jukwaa la pamoja lenye ushindani unaoambatana na heshima, nidhamu, na urafiki, hali inayopunguza hofu na kuongeza kuaminiana.

Mmoja wa wanamichezo mashuhuri na sauti yenye heshima duniani katika riadha, Filbert Bayi, anaamini kuwa amani na michezo haviwezi kutenganishwa. 

Katika mahojiano maalum, Bayi ambaye amewahi kushikilia rekodi ya dunia, alibainisha kuwa hakuna nchi inayoweza kukuza vipaji vya michezo bila kuwepo kwa amani na utulivu. Alisisitiza kuwa michezo si burudani pekee, bali ni chanzo kikubwa cha ajira, huduma za kijamii, na undugu miongoni mwa watu wa mataifa mbalimbali.

Bayi alieleza kuwa amani huweka mazingira rafiki kwa wanamichezo kufanya mazoezi na kuonesha vipaji vyao bila hofu ya usalama. 

Alitolea mfano Tanzania kama kioo cha namna amani inavyochochea maendeleo ya michezo, kwani wanamichezo wana nafasi ya kushindana katika hali ya utulivu. Aliongeza kuwa katika ngazi ya kimataifa, michezo imekuwa ikitumika kupunguza uhasama kati ya mataifa yaliyowahi kuwa kwenye migogoro, akitolea mfano wa mataifa hayo kutembea pamoja wakati wa ufunguzi wa michezo mikubwa.

Mbali na hayo, Bayi alikumbusha tukio la kihistoria la kususia michezo ya Olimpiki ya mwaka 1976 kupinga ubaguzi wa rangi kama ujumbe wa kusisitiza haki, usawa, na amani. Alihitimisha kwa kutoa rai kwa serikali, vyombo vya michezo, na jamii kwa ujumla kuendelea kuwekeza katika michezo kama njia ya kukuza amani, hasa kwa vijana. Alisisitiza kuwa kudumisha amani na umoja ndiyo siri ya kujenga Tanzania imara na yenye ustawi kwa vizazi vijavyo.

CCM MKOA WA TANGA YAWAPA MWEZI MMOJA VIONGOZI WA JIJI LA TANGA KUHAKIKSHA SOKO LA MGANDINI LINABORESHWA NA KUIMARISHWA USAFI.


 Na Rebeca Duwe Tanga


Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Tanga na mjumbe wa kamati kuu ya Halmashauri kuu ya CCM TaifaRajab Abdurhaman ametoa maelekezo kwa Halmashauri ya Jiji la Tanga kuhakikisha maeneo ya kukusanyia taka katika soko la Mgandini yanaboreshwa kwa kujazwa kifusi ikiwemo kurekebisha barabara za ndani ili kuimarisha usafi.


Hayo aliyasema wakati wa ziara yake ya kufuatilia utekelezajia wa magagizo aliyoyatoa awali kuhusu kuboresha usafi wa soko hilo lilipo jijini Tanga ambapo viongozi wa jiji walianza kuyafanyia kazi ikiwemo kuondosha uchafuzi uliokuwepo awali .

Aidha alisisitiza umuhimu wa kuhakikisha maji ya mvua yanaelekezwa ipasavyo kwenye mifereji ili kuepusha mafuriko na uharibifu wa miundombinu katika soko hilo ili kuweza kuondoa changamoto ya tope kwa wafanyabiashara na wananchi kwa ujumla.

Awali, wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya usafi, Mwenyekiti huyo hakuridhishwa na mazingira ya soko hilo na kutoa muda wa mwezi mmoja kwa uongozi wa Jiji kuhakikisha hali ya usafi inaboreshwa.


Akizungumza baada ya kufanya ziara ya ufuatiliaji, Rajab aliwapongeza Mstahiki Meya pamoja na viongozi wa Jiji kwa kuchukua hatua na kuanza kutekeleza maelekezo yaliyotolewa na Chama cha Mapinduzi.


“Hatuhitaji viongozi wa kulalamika, tunahitaji viongozi wanaochukua hatua kutatua changamoto za wananchi. Mlichokifanya ni kutimiza wajibu wenu,” alisema.


Alisema kuwa hali ya uchafu iliyokuwepo awali haikuwafurahisha viongozi wala wafanyabiashara, hivyo hatua zilizochukuliwa zinaonesha uwajibikaji wa uongozi.


Sambamba na hayo wa Mwenyekiti CCM Rajab alisisitiza kuwa atarejea kukagua maendeleo hayo baada ya wiki mbili na kuonya kuwa hataki kusikia visingizio badala ya utekelezaji.


“Ndani ya mwezi mmoja kuanzia Aprili 9 hadi Mei 9, tunatarajia kuona kazi imeanza. Hatutaki hadithi, tunataka vitendo,” alisisitiza.Rajab


Aidha, alieleza kuwa Jiji la Tanga ni taswira ya mkoa huo, hivyo linapaswa kuwa safi na lenye mpangilio mzuri.


Alikumbusha kuwa zamani Tanga ilikuwa mji unaojulikana kwa usafi na ustaarabu, hivyo ipo haja ya kurejesha hali hiyo.


Kuhusu huduma za vyoo katika soko hilo, Mwenyekiti alieleza kutoridhishwa na hali iliyopo, akibainisha kuwa choo kilichopo hakitoshelezi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya watumiaji.


Alisema kuwa hali hiyo inasababisha baadhi ya watu kulazimika kujisaidia katika maeneo yasiyofaa, jambo linalohatarisha afya za wananchi na wafanyabiashara.


Alisisitiza umuhimu wa Jiji kutafuta suluhisho la kudumu, ikiwemo kuboresha mfumo wa maji taka ili kuendana na ongezeko la watumiaji.


Hata hivyo, aliwapongeza viongozi kwa kuanza mpango wa kujenga choo kipya chenye matundu 12 kitakachosaidia kupunguza changamoto hiyo, hasa katika kipindi hiki ambacho soko linatarajiwa kujengwa upya.


Pia alizungumzia changamoto ya msongamano wa magari yanayoleta bidhaa sokoni hapo, akielekeza kuwepo kwa utaratibu maalum wa magari kuingia na kushusha mizigo kwa mpangilio ili kupunguza msongamano na kuboresha usafi.


Alipendekeza magari yapaki katika maeneo maalum yaliyo nje ya soko, kisha yaingie kwa zamu kushusha bidhaa.


Katika hatua nyengine alisisitiza umuhimu wa kujenga mifereji ya maji ili kuzuia maji ya mvua kutuama au kuingia sokoni, hali inayochangia uchafu na uharibifu wa mazingira.


Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa Jiji kuwa karibu na wananchi na kushughulikia changamoto zao kwa vitendo, akibainisha kuwa wananchi hao ndio chanzo cha mapato ya Jiji kupitia kodi.


Kwa upande wake, Naibu Meya ambaye pia ni Diwani wa kata ya mwanzange ambalo eneo lililopo soko hilo, Khalid Rashid alisema kuwa Jiji lina mpango wa kuboresha miundombinu ya ndani ya soko, ikiwemo njia za kupita ili kuondoa changamoto ya matope wakati wa mvua. Alibainisha kuwa kazi hiyo inatarajiwa kuanza ndani ya wiki moja.

Friday, April 10, 2026

AMANI NI SILAHA YA KUTIMIZA NDOTO NA MAONO YETU- MSIGWA



Na mwandishi wetu, Dodoma

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Gerson Msigwa amesisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kuendelea kufanya kazi kwa bidii pamoja na kulinda na kudumisha amani na mshikamano uliopo nchini kama msingi muhimu unaoweza kumsaidia kila Mmoja kuweza kutimiza ndoto na maono waliyo nayo kwa maendeleo na ustawi wa mtu mmoja mmoja, familia na Taifa kwa ujumla.

Msigwa ameyasema hayo wakati akizungumza ma Chombo kimoja cha habari Mjini Dodoma leo Jumamosi Aprili 10, 2026, akisisitiza kuwa hata matarajio, matamanio na mipango iliyo kwenye Dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 hayawezi kufikiwa bila ya amani, utulivu na mshikamano wa jamii utakaowezesha sekta binafsi na kila Mtanzania kujielekeza katika kuendeleza shughuli za kiuchumi na Kijamii.

"Hatuwezi kufanya kazi kama nchi haina utulivu, niwaombe Watanzania tulinde amani, utulivu na mshikamano wetu kwa gharama yoyote kwani ndoto hizi kubwa za kufikia matarajio na matamanio yetu zitatimia ikiwa tuna amani, utulivu na mshikamano." Amesema Msigwa.

Msemaji huyo wa serikali amesisitiza kuwa Dira 2050 katika kutimiza lengo la kuwa na uchumi wa Dola za Marekani trilioni moja unategemea sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 na sekta ya Umma kwa asilimia 30 pekee, hivyo badala ya kupoteza muda kubishana na kushughulika na mambo ya maana, Msigwa ameomba kila Mtanzania kujielekeza katika uzalishaji mali na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo nchini zikivutia zaidi kutokana na amani na utulivu uliopo nchini Tanzania.

Thursday, April 9, 2026

SAMAMBA ATOA WITO GST KUBORESHA MAZINGIRA YA KAZI, KUIMARISHA USHIRIKIANO


Na Mwandishi Wetu - Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, ameitaka Menejimenti ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kuhakikisha inajenga mazingira rafiki ya kazi yatakayowawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kujisikia salama kazini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi la GST uliofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, Eng. Samamba amesema mazingira bora ya kazi ni msingi muhimu wa kuongeza tija, ubunifu na ufanisi katika utumishi wa umma.

Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuiwezesha GST kuwa kitovu cha takwimu za jiosayansi zenye ubora na zinazopatikana kwa urahisi kwa wadau mbalimbali.

“Ni wajibu wa kila mtumishi kutekeleza majukumu aliyopewa kwa weledi na kuchangia kikamilifu mafanikio ya taasisi,” amesema Eng. Samamba.

Aidha, amewataka watumishi kuimarisha mshikamano, umoja na ushirikiano kazini, akibainisha kuwa hali hiyo itaongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na kuinua hadhi ya utumishi wa umma.
Katika hatua nyingine, Eng. Samamba amewapongeza viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi la GST, akieleza kuwa baraza hilo lina jukumu muhimu la kushauri uongozi juu ya ufanisi wa kazi, mipango ya maendeleo, pamoja na kuboresha ustawi wa wafanyakazi.

Amebainisha kuwa majukumu ya baraza yanajumuisha pia kujadili mipango ya mapato na matumizi, kupanga mikakati ya maendeleo ya taasisi, na kuimarisha ushirikiano kati ya wafanyakazi na uongozi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa GST, Eng. Ally Samaje, amesema taasisi hiyo itaendelea kuboresha utendaji wake ili kuchangia kikamilifu maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Ameongeza kuwa GST imejipanga kuboresha huduma zake za jiosayansi na maabara, sambamba na kuendana na mabadiliko ya teknolojia, ili kutoa matokeo yenye tija kwa uchumi wa taifa.

Wednesday, April 8, 2026

TRA TANGA YAVUKA MALENGO KATIKA UKUSANYAJI WA MAPATO NDANI YA MIEZI TISA KUANZIA JULAI 2025 HADI MACH 2026.


 MAMLAKA ya mapato (TRA)mkoani Tanga imeweka rekodi mpya ya ukusanyaji wa mapato baada ya kukusanya jumla ya Shilingi Bilioni 406.17 katika kipindi cha miezi tisa (Julai 2025 – Machi 2026), ikiwa ni ongezeko la asilimia 137 ya lengo lililowekwa.


Katika kipindi hicho, Mkoa ulikadiriwa kukusanya kiasi cha Shilingi Bilioni 296.3, ambapo ufanisi huo mkubwa uliovuka lengo kwa takriban Shilingi Bilioni 110, umetajwa kuwa ni matokeo ya ushirikiano wa karibu kati ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), walipakodi, na vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Tanga.


Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa, Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Castro John, amewashukuru walipakodi wa Tanga kwa kulipa kodi kwa hiari na kushirikiana na taasisi mbalimbali kama Chama cha Wafanyabiashara (JWT) na Chama cha Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA).


"Huu ni ufanisi mkubwa ambao haujawahi kutokea. Tunamshukuru Mkuu wa Mkoa na vyombo vya usalama kwa kuhakikisha mazingira ya ukusanyaji kodi yanakuwa salama. Sifa hizi ni za walipakodi wa Tanga ambao wamekuwa wasikivu na wazalendo kwa nchi yao," alisema John.


Licha ya mafanikio hayo, John ametoa onyo dhidi ya wafanyabiashara wanaotumia njia zisizo rasmi (njia za panya) kuingiza bidhaa nchini. Alibainisha kuwa bidhaa za magendo siyo tu zinaikosesha serikali mapato, bali ni hatari kwa afya ya mlaji kwani hazijapita katika taasisi za udhibiti wa ubora.


Aliongeza kuwa operesheni dhidi ya magendo zinaendelea na wafanyabiashara kadhaa wameshakamatwa na kutozwa faini kubwa (Penalties), huku akisisitiza kuwa chombo chochote kitakachokutwa kimebeba bidhaa za magendo kitataifishwa kulingana na sheria. Aidha, aliwataka wananchi kudai risiti za EFD na wafanyabiashara kutoa risiti halali katika kila manunuzi.


Meneja huyo, amewahimiza wafanyabiashara kutumia Bandari ya Tanga ambayo sasa inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kutoa mizigo kwa wakati, jambo linalochochea ukuaji wa biashara mkoani hapa.


Kuhusu wafanyabiashara wenye madeni makubwa, TRA imewataka kufika ofisini kwa ajili ya majadiliano (Negotiations) ili kuwekewa utaratibu wa kulipa kwa awamu. Mamlaka hiyo imebainisha kuwa imeweka "Dawati la Wafanyabiashara" kwa ajili ya kutoa elimu na kusaidia kukuza biashara ndogo ziweze kufikia hatua ya kuwa walipakodi wakubwa.


Meneja huyo ametoa wito kwa wafanyabiashara kujitokeza kukadiriwa mapato yao ili kuepuka changamoto wakati wa zoezi la ukaguzi barabarani.

Tuesday, March 24, 2026

DUNIA YAIPIGIA SALUTE TANZANIA: TUZO ZA STANBIC JIJINI LONDON NI JIBU KWA WANAOBWABWAJA MITANDAONI



Wakati baadhi ya watu wakitumia muda wao kwenye mitandao ya kijamii kubwabwaja na kupotosha kuwa uchumi wa Tanzania unayumba, jumuiya ya kimataifa imetoa jibu la kishindo kupitia sekta ya fedha. Tuzo tatu za kimataifa alizotunukiwa Mtendaji Mkuu wa Stanbic Tanzania, Manzi Rwegasira, jijini London nchini Uingereza, ni kielelezo tosha kuwa mfumo wetu wa kifedha uko imara na unaheshimika duniani.

Jarida la Euromoney, ambalo ni mamlaka ya juu ya tathmini ya kibenki duniani, haliwezi kuipa Benki ya Stanbic tuzo ya Benki Bora ya Kimataifa kwa mwaka wa pili mfululizo kama mazingira ya biashara na usalama wa shilingi yetu yangekuwa shakani. Hii ni tafsiri ya wazi kuwa Tanzania ina watu wenye akili na weledi wanaosimamia misingi ya fedha, na si kama inavyochorwa na "wapiga kelele" wa kidijitali.

Ushindi huu ni salamu kwa wawekezaji kuwa shilingi ya Tanzania na mfumo wake wa kibenki ni sehemu salama ya kuweka na kukuza mali. Kitendo cha Stanbic kutajwa kuwa Benki Bora ya Kimataifa kwa Wateja Maalumu (Private Banking) kinaonyesha uwezo wa kipekee wa kuunganisha uchumi wa ndani na masoko ya dunia.

Hii ina maana kuwa, licha ya changamoto za kiuchumi zinazoikumba dunia kwa sasa, Tanzania imefanikiwa kujenga "daraja la kifedha" linalowawezesha wateja kukuza mali zao nje ya mipaka kwa usalama. Heshima hii tuliyoipata jijini London inathibitisha kuwa sera zetu za kifedha zinaaminika na majopo huru ya wataalamu wa kimataifa, jambo linalowapa imani washirika wa maendeleo na wafanyabiashara wakubwa duniani.

Aidha, Tuzo ya Benki Bora kwa Kizazi Kijacho iliyonyakuliwa na Stanbic ni ujumbe mzito kwa mustakabali wa biashara za Kitanzania kuelekea Dira ya 2050. Hii inaashiria kuwa kuna maandalizi ya dhati ya kuwavusha warithi wa mali na vijana kusimamia uchumi kwa uwajibikaji.

Tunapoona taasisi zetu zikishinda tuzo za namna hii, tafsiri yake ni kwamba uchumi wetu haujajengwa kwa kubahatisha, bali kwa mikakati inayolenga uendelevu wa vizazi. Ni uthibitisho kuwa Tanzania inapiga hatua kubwa katika namna mali zinavyoundwa na kusimamiwa, ikijitofautisha na mataifa mengine yanayokumbwa na migogoro ya usimamizi wa rasilimali.

Kwa upande wa huduma kwa wateja, tuzo hiyo ya tatu inashindilia msumari kwenye ukweli kwamba mabenki yetu yameacha kufanya kazi kama ofisi za kutoa fedha tu, bali yamekuwa washauri wa kimkakati wa maamuzi ya kifedha. Huu ni ushindi wa kila Mtanzania anayeamini katika maendeleo ya nchi yake.

Hii inatupa picha kuwa Tanzania ipo sawa na mataifa mengine makubwa duniani katika kutoa huduma za kiwango cha juu. Hivyo, badala ya kusikiliza upotoshaji wa mitandaoni unaodai "Tanzania haiwezekani," tuzo hizi za Euromoney Private Banking Awards 2026 ni kioo kinachoonyesha kuwa Tanzania inawezekana na inasonga mbele kwa kasi ya ajabu katika anga za kimataifa.

Mafanikio haya ya Stanbic Tanzania ni heshima kwa nchi na ni kigezo cha tathmini kuwa uchumi wetu unaenda vyema chini ya usimamizi makini.

Tunapokuwa na benki zinazong'ara London, maana yake ni kwamba soko letu la fedha limekomaa na lina ushindani unaohitajika kuvuta mitaji mipya. Ni wakati wa Watanzania, hasa vijana, kuacha kuyumbishwa na maneno ya mitandaoni na badala yake waone fahari na fursa zilizopo katika mfumo wetu wa kifedha uliopata baraka za dunia. Tanzania inaheshimika, shilingi yetu inalindwa na weledi, na mustakabali wa mali za Watanzania upo katika mikono salama na ya kisasa.





Labels:Habari



SHARE:








COMMENTSBLOGGERFACEBOOK: DISQUS





WEEK TRENDING

Monday, March 23, 2026

MIRADI YA SHILINGI BILIONI 85 KUCHOCHEA USHIRIKIANO WA TANZANIA NA AUSTRIA


Tanzania na Austria zimekubaliana kuimarisha ushirikiano wa kimaendeleo kupitia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati yenye thamani ya Euro milioni 30 (takriban Shilingi bilioni 85), itakayolenga sekta za elimu, usalama na ufundi.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mhandisi Mshamu Munde, Machi 23, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa mazungumzo na ujumbe kutoka Austria ulioongozwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria anayeshughulikia masuala ya kisiasa, Mhe. Balozi Dkt. Hannah Liko. Amesema ziara hiyo imekuja wakati muafaka ambapo Tanzania inahitimisha Dira ya Maendeleo ya 2025 na kuanza mchakato wa Dira mpya ya 2050.

Mhe. Munde amebainisha kuwa Austria imekuwa ikifadhili miradi muhimu kupitia mikopo nafuu inayochangia moja kwa moja maendeleo ya wananchi, ikiwemo mradi wa ukarabati na uwekaji wa mifumo ya kisasa katika Chuo cha Sayansi na Teknolojia cha Karume (KIST) Zanzibar pamoja na maboresho ya mfumo wa elimu visiwani humo. Miradi mingine ni ukarabati wa Chuo cha Ufundi Arusha (ATC) pamoja na ununuzi na usambazaji wa magari ya kuzima moto na vifaa vya uokoaji Zanzibar.

Aidha, Mhe. Munde amewasilisha salamu za shukrani kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, akisisitiza kuwa Austria ni mshirika wa maendeleo anayeaminika na kwamba Tanzania iko tayari kuimarisha ushirikiano huo kwa lengo la kuinua hali ya kijamii na kiuchumi ya wananchi.

Kwa upande wake, Balozi Dkt. Liko amepongeza ushirikiano huo madhubuti na kuahidi kuwa Austria itaendelea kushirikiana na Tanzania katika sekta za utalii na viwanda ili kuongeza tija ya kiuchumi kwa pande zote mbili.

Katika mazungumzo hayo, pande zote mbili pia zimejadili utekelezaji wa Mkakati wa Austria na Afrika wa mwaka 2026–2029 unaolenga kuimarisha amani na usalama, kukuza uchumi wa kijani, kukabiliana na uhamiaji haramu huku ikiimarishwa mifumo ya uhamiaji wa kisheria na wenye tija, pamoja na kuendeleza sayansi na elimu.

Sunday, March 22, 2026

Mwili wa mwanaume waokotwa Magugu, wananchi waishi kwa hofu.


Na John Walter-Babati

Tukio la kusikitisha limeutikisa wakazi wa eneo la Magugu, wilayani Babati mkoani Manyara, baada ya mwili wa mwanaume ambaye bado hajatambulika kukutwa umetupwa pembeni mwa barabara kuu ya Babati–Arusha.

Kwa mujibu wa taarifa za awali, marehemu ana dalili za kuuawa kikatili, huku chanzo cha tukio hilo kikiwa bado hakijabainika.

Wananchi wa eneo hilo wameeleza hofu kubwa kufuatia tukio hilo, wakihofia usalama wao na kuziomba mamlaka husika kuchukua hatua za haraka kuwabaini wahusika na kuimarisha ulinzi.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Magugu, Lohay Amos, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo, akieleza kuwa limetokea usiku wa kuamkia Machi 19 katika eneo la Kwa Chami.

Amesema mwili wa marehemu ulikutwa ukiwa na majeraha makubwa kichwani, ambapo inaelezwa kuwa alipigwa na kitu kizito kinachofanana na shoka, hali iliyosababisha kuharibika kwa taswira ya uso na kufanya kuwa vigumu kutambulika.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya Magugu huku uchunguzi ukiendelea.

Mkuu wa Polisi Wilaya ya Babati, Mrakibu wa Polisi Ernesta Mwambinga, alifika eneo la tukio na kuwahakikishia wananchi kuwa Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa kina ili kuwabaini waliohusika na tukio hilo la kinyama.

Amewataka wananchi kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa zozote zitakazosaidia uchunguzi, akisisitiza kuwa taarifa hizo zitahifadhiwa kwa siri.

Wananchi wa Magugu wamelalamikia kuongezeka kwa matukio ya ukatili katika eneo hilo, wakitaka ulinzi uimarishwe pamoja na uwekaji wa taa za barabarani, hasa katika maeneo yenye giza nene nyakati za usiku.

Jeshi la Polisi linaendelea na jitihada za kumtambua marehemu na kubaini ukweli wa tukio hilo.

 

Saturday, March 14, 2026

MFUMO WA “ONGEA NA WAZIRI” WAIMARISHA MAWASILIANO KATI YA SERIKALI NA WANANCHI


Waziri wa Afya, Mhe. Mohamed Mchengerwa, amesema mfumo wa "Ongea na Waziri" ni daraja muhimu kati ya serikali na wananchi unaolenga kusikiliza moja kwa moja maoni, kero na mapendekezo ya wananchi kuhusu huduma za afya.

Amesema mfumo huo, uliozinduliwa rasmi Januari 26, 2026, unalenga kuongeza uwazi na uwajibikaji katika utoaji wa huduma za afya na kuhakikisha maamuzi ya serikali yanaendana na mahitaji halisi ya wananchi.

Waziri Mchengerwa ametoa kauli hiyo Machi 13, 2026 wakati wa ziara yake katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala jijini Dar es Salaam, ambapo pia alishiriki katika tukio la "Ongea na Waziri" lililowakutanisha watumishi wa afya na wananchi kwa lengo la kusikiliza changamoto na kupokea maoni kuhusu utoaji wa huduma za afya.

Amesema kuanzishwa kwa mfumo huo kunaonesha dhamira ya serikali ya kuweka kipaumbele katika kusikiliza wananchi kama msingi wa kuboresha huduma na kuimarisha uwajibikaji katika sekta ya afya.

Aidha, Waziri Mchengerwa amesema serikali ipo mbioni kuandaa mwongozo utakaotumika katika hospitali zote za serikali ili kukabiliana na malalamiko ya wananchi kuhusu gharama kubwa za matibabu na upatikanaji wa dawa. 


Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe, amesema mfumo wa kidijitali wa "Ongea na Waziri" ulioanzishwa na Waziri Mchengerwa unalenga kusikiliza na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika sekta ya afya.

Dkt. Shekalaghe amesema kupitia mfumo huo wananchi wanapata nafasi ya kuwasilisha changamoto na maoni yao moja kwa moja kwa Waziri, jambo linalosaidia kupatikana kwa ufumbuzi wa haraka na kuimarisha utoaji wa huduma za afya.

Ameongeza kuwa wizara itafanya majumuisho ya maswali yaliyoulizwa katika mwezi uliopita ili kutathmini ni maswali mangapi yamepatiwa majibu pamoja na hatua zilizochukuliwa katika kuyatatua.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali ya Mwananyamala, Evancy Asenga, amemshukuru Waziri Mchengerwa kwa ziara yake hospitalini hapo na kuahidi kutekeleza maagizo yote yaliyotolewa ili kuboresha huduma, hususan katika eneo la mapokezi ya wananchi.

Pia ameomba serikali kufanikisha ujenzi wa jengo kubwa la ghorofa katika hospitali hiyo ili kurahisisha utoaji wa huduma. 


Asenga amesema hospitali hiyo imefanikiwa kufanya mageuzi makubwa katika utoaji wa huduma kutokana na uwekezaji mkubwa uliofanywa na serikali ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, Dkt. Mercy Maya, amesema hospitali hiyo inaendelea kuimarisha na kupanua huduma za kibingwa kwa kuboresha miundombinu na kuongeza vifaa tiba ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora kwa wakati.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...