NA REBECA DUWE TANGA
Katika kuendeleza shughuli za uwajibikaji kwa jamii, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) leo imepanda miti isiyopungua 1,000 katika Shule ya Sekondari Ummy Mwalimu iliyopo Kata ya Maweni, ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwa mamlaka hiyo.
Akizungumza wakati wa zoezi hilo, mgeni rasmi ambaye ni Naibu Kamishna wa Shughuli za Ufundi – Kodi za Ndani, Ted Frank Silkiluwasha, alisema pamoja na jukumu la kukusanya mapato ya Serikali, TRA imeendelea kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii zinazoleta maendeleo kwa wananchi.
Alisema zoezi la upandaji miti linaonesha ushirikiano mzuri uliopo kati ya TRA na jamii, huku akisisitiza umuhimu wa kuitunza miti hiyo ili iweze kukua na kutoa manufaa kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
"Utunzaji wa miti ni muhimu kwa sababu huchangia kulinda tabaka la ozone, kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi na kulinda afya ya binadamu pamoja na viumbe wengine," alisema Silkiluwasha.
Aidha, alimtaka Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga kuendelea kutoa elimu ya kodi kwa wananchi, akieleza kuwa elimu hiyo inapaswa kuwa endelevu. Pia alipendekeza Shule ya Sekondari Ummy Mwalimu kuingizwa katika mpango wa Tax Club, unaolenga kuwajengea wanafunzi uelewa na utamaduni wa kulipa kodi.
"Ukubwa wa taifa haupimwi kwa wingi wa watu au silaha, bali kwa uchumi imara. Uchumi huo hujengwa kupitia ukusanyaji wa mapato ya Serikali ambayo huwezesha kuboresha sekta za elimu, afya, miundombinu na hata kuimarisha ulinzi na usalama," alisema.
Kwa upande wake, Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Castrol John, aliwataka wafanyabiashara kuzingatia sheria za kodi na kuacha kutumia njia zisizo halali wanapoingiza bidhaa nchini.
Pia alihimiza wananchi kuwafichua wakwepa kodi, akibainisha kuwa TRA ina utaratibu wa kutoa zawadi kwa watu watakaotoa taarifa zitakazosaidia kuokoa mapato ya Serikali yanayopotea.
Naye Mhifadhi kutoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Michael Charles, aliipongeza TRA kwa hatua hiyo na kuzitaka taasisi nyingine kuiga mfano huo.
Alisema miti ina mchango mkubwa katika kuhifadhi mazingira, kuboresha ubora wa hewa, kuhifadhi viumbe hai, kuongeza vivutio vya utalii, kutoa matunda na kuchangia afya bora ya jamii.
Akitoa shukrani kwa TRA, Mkuu wa Shule ya Sekondari Ummy Mwalimu, Asha Kitundu, alisema shule hiyo ina eneo la takribani ekari 700, hivyo miti iliyopandwa itasaidia kutoa kivuli, kuzuia mmomonyoko wa udongo na kuboresha mazingira ya kujifunzia.
Aidha, aliwahamasisha wadau wengine kujitokeza kuisaidia shule hiyo, akieleza kuwa bado ni changa na inahitaji ushirikiano wa jamii katika kuendeleza maendeleo yake.
Shule ya Sekondari Ummy Mwalimu ilianzishwa mwaka 2022 ikiwa na wanafunzi 316 waliohamishwa kutoka Shule ya Sekondari Maweni. Kwa sasa shule hiyo ina wanafunzi 916 na walimu watatu, huku ikitarajia kupokea wanafunzi 83 wa Kidato cha Tano mwezi Julai mwaka huu.







































