Sunday, June 21, 2026

TARURA KUENDELEA KUJENGA MADARAJA YA MAWE NCHI NZIMA -SUNGURA



Na Mwandishi wetu, Dodoma

Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) inaendelea na uboreshaji wa miundombinu ya barabara nchini huku serikali ikiwa imetoa takribani ya Dola Milioni 65 kwa ajili ya kurejesha mawasiliano yaliyoharibika kutokana na mvua za El Nino za mwaka 2023/2024.

Akizungumza na Wanahabari Kwenye Maadhimisho ya wiki ya utumishi wa umma mkoani Dodoma Mkuu wa kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma Tarura, Catherine Sungura amesema TARURA wanahudumia barabara za wilaya zenye urefu wa Kilomita 144,429 nchi nzima zikiwemo barabara za lami,mawe,changarawe na udongo.

Tunaendelea kujenga Madaraja nchi nzima katika kuhakikisha jamii inapata huduma za maendeleo kupitia barabara hizo hivyo kufikia sasa tunaMadaraja ya Mawe yapatayo 490 .

" Kutokana na mvua Za mwaka 2023/2024 Tarura tulipokea fedha kutoka benki ya dunia takribani ya dola Milioni 65 kwa ajili ya kurejesha mawasiliano ya barabara ambazo ziliathirika na Mvua za Elnino ambapo kwa sasa tumerudisha Mawasiliano ya barabara hizo kwa asilimia 70 katika Vijiji,Wilaya na Mikoa." Amesema Mkuu wa kitengo Sungura"

Aidha, mameneja wa mikoa hususani mkoa wa tabora wilaya ya sikonge na urambo huduma zimerejea kwa wananchi kama kawaida hivyo tarura tunaendelea kuboresha miradi mbalimbali ukiwemo mradi wa TACTIC katika miji 45 ambapo tunajenga masoko, barabara za lami na Mradi wa DMDp 2 ambao tunajenga takribani kilomita 250 katika wilaya 5 za mkoa wa Dar es Salaam.

Vilevile kwa mkoa wa Dar esalaam tuwatoe hofu Wananchi kuwa wakandarasi wamerejea kukamilisha miundombinu ya barabara hiyo hivyo Mtaa wa majohe kivule kuna kilomita 2 za barabara za zege vilevile kigamboni.

Katika Hatua nyingine tarura tumetoa ajira kwa kikundi cha maafisa usafirishaji (bodaboda) mkoani morogoro wilaya ya ifakara na ambapo wanafanya matengenezo ya kawaida ya miundombinu na hivyo wanaenda kuinuka kiuchumi kupitia miradi wa RISE.

Kwa upande wake afisa utumishi mkuu Speransia Mhapa ameongeza kuwa tarura imefanya mabadiliko mbalimbali kwenye sekta ya miundombinu nchini ambapo tunatambua katika maendeleo hayo watumishi wa umma wamekuwa na mchango mkubwa katika kukamilisha suala hilo la miundombinu.

Nitoe wito Kwa wananchi wote wanaoendelea kutembelea kwenye maadhimisho haya wafike kwenye banda la Tarura kupata elimu na huduma mbalimbali zinazotolewa na Wakala wa barabara za mijini na Vijijini (TARURA)

Saturday, June 20, 2026

TBA YATEKELEZA MPANGO WA NYUMBA ZA GHARAMA NAFUU KWA WANANCHI



Katika kutekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 inayolenga kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu, Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) umeendelea kutekeleza mpango wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ili kuwawezesha wananchi, hususan vijana, kumudu kumiliki makazi.

Akizungumza katika Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayofanyika kitaifa katika viwanja vya Chinangali Park jijini Dodoma, Mkurugenzi wa Huduma Saidizi wa TBA, Bi. Amina Lumuli, amesema kuwa TBA tayari imeanza kutekeleza miradi ya nyumba za gharama nafuu katika mkoa wa Dar es Salaam.

Bi. Lumuli ametaja Mradi wa Temeke Kota kuwa ni miongoni mwa miradi hiyo, akibainisha kuwa utekelezaji wa mpango huo utaendelea katika maeneo mbalimbali nchini.


"Tunawakaribisha wawekezaji kuja kushirikiana nasi ili kwa pamoja tuweze kufanikisha lengo la Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050 la kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na ya gharama nafuu," amesema Bi. Lumuli.

Aidha, Bi. Lumuli amesema utekelezaji wa mradi huu unatokana na dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuhakikisha wananchi wanapata makazi bora na yenye gharama nafuu.

Amesema TBA itaendelea kuhakikisha makundi yote, yakiwemo makundi maalum, yanafikiwa na kunufaika na programu hii ya nyumba za gharama nafuu.



POLISI WAFICHUA MPANGO WA UHALIFU JULAI 7

Jeshi la Polisi limetoa onyo kali kwa watu wote wanaohamasisha na kupanga kutekeleza vitendo vya uvunjifu wa amani na uhalifu nchini, wakiwemo wale wanaochochea kufanyika kwa maandamano mnamo tarehe 7 Julai mwaka huu.
Onyo hilo limetolewa kufuatia kuwepo kwa maswali mengi kutoka kwa baadhi ya wananchi hivi karibuni, wakitaka kujua jinsi jeshi hilo linavyofuatilia na kushughulikia uhamasishaji huo wa uvunjifu wa amani unaoendelea kufanywa na baadhi ya watu kupitia majukwaa mbalimbali ya mitandao ya kijamii.

Kupitia taarifa yake, Jeshi la Polisi limesema linafuatilia kwa karibu sana shughuli hizo zote kupitia mifumo yake mbalimbali pamoja na mitandao ya kijamii, ambapo imegundulika kuwa watu hao wameacha ajenda ya awali ya maandamano yasiyozingatia sheria na sasa wanahamasishana kufanya vitendo vizito vya kihalifu.

Miongoni mwa vitendo vya hatari vinavyohamasishwa ni pamoja na kufunga barabara, kuchoma moto shule kwa lengo la kusababisha taharuki kwa wazazi na walezi, kushambulia wananchi, kukata watu vichwa na kuua, pamoja na kuharibu mali za umma na za binafsi.

Aidha, watu hao wamediriki kwenda mbali zaidi kwa kuchocheana kupitia mitandao hiyo kuvamia askari wa vyombo vya ulinzi na usalama ili kuwapora silaha kwa ajili ya kwenda kuzitumia kutekeleza uhalifu wanaoupanga.

Jeshi la Polisi limesisitiza kuwa uhamasishaji huo wa jinai unaofanyika chini ya kivuli cha kile wanachokiita haki ya kufanya maandamano ya amani haukubaliki hata kidogo, kwani ni kinyume kabisa na sheria za nchi, misingi ya utawala wa sheria, mikataba ya kikanda na kimataifa, na unahatarisha usalama wa Taifa.

Jeshi hilo limefafanua kuwa hakuna haki yoyote inayomruhusu mtu kuhamasisha uhalifu unaokusudia kuhatarisha usalama wa maisha ya watu na mali zao, au unaokiuka haki za wengine kwa kuwajengea hofu kila siku na kuwanyima uhuru wao wa kufanya shughuli zao za kila siku za kujitafutia kipato.

Kwa sababu hiyo, Jeshi hilo limesema hatua stahiki za kisheria zinaendelea kuchukuliwa dhidi ya wahusika wote, na jeshi linaendelea kuwafuatilia kwa karibu sana kwa mujibu wa sheria za nchi.

Jeshi la Polisi limetoa wito kwa wananchi wote nchini kuungana kwa pamoja katika kushirikiana kukataa na kupinga kwa nguvu zote vitendo hivyo vya kihalifu vinavyolenga kuhatarisha maisha ya wananchi, mali zao, mali za umma, pamoja na amani ya nchi.

Vilevile, limetoa ushauri kwa mtu yeyote anayepokea ujumbe unaohamasisha uhalifu wa aina hiyo kutousambaza kabisa, bali kuufuta mara moja na kutoa taarifa kwa vyombo husika ili hatua zichukuliwe.

Jeshi limewahakikishia wananchi wote kuwa hali ya usalama nchini itaendelea kuwa shwari, yenye amani, utulivu na usalama kamili, kwani mambo hayo yatalindwa na kudumishwa kwa ushirikiano wa karibu sana kati ya Jeshi la Polisi pamoja na vyombo vingine vyote vya ulinzi na usalama.

Friday, June 19, 2026

JUMLA YA MIRADI 73 YA MWENGE WA UHURU YENYE THAMANI YA SH BILIONI 27.7 KUKAGULIWA,KUWEKEWA MAWE YA MSINGI NA KUZINDULIWA

 


Na Rebeca Duwe  Tanga


Mkuu wa mkoa wa Tanga Balozi Batilda Burian amewataka wananchi wa  Mkoa waTanga kutokeza kupoke mwenge wa uhuru  ili kuweza kuukimbiza ili kuhakikisha nuru inamulika kila mahali na kuimarisha umoja na mshikamano, ambapo utakimbizwa katika halmashauri zote 11 za mkoa huo na kukagua, kuzindua pamoja na kuweka mawe ya msingi katika miradi 73 yenye thamani ya zaidi ya 27.7


Hayo aliyasema wakati akizungumza na waandishi wa habari ,kuhusu maandalizi ya Mbio za Mwenge wa Uhuru  mwaka huu ambapo alisema Mwenge wa Uhuru utapokelewa katika Viwanja vya Shule ya Msingi Mji Mpya, Kijiji cha Mtoro, Kata ya Tunguli wilayani Kilindi ukitokea Mkoa wa Morogoro.



Alisema baada ya mapokezi hayo, Mwenge utakimbizwa kwa umbali wa kilometa 1,340 kupitia halmashauri zote za Mkoa wa Tanga kabla ya kukabidhiwa Mkoa wa Kilimanjaro Juni 28 mwaka huu katika Uwanja wa Shule ya Msingi Hedaru.


Dk. Burian alisema kati ya miradi 73 itakayofanyiwa kazi na Mwenge wa Uhuru, miradi 34 itawekewa mawe ya msingi, miradi 26 itafunguliwa na kuzinduliwa, miradi 11 ya vijana itakaguliwa pamoja na miradi miwili ya sekta ya maji.


Alifafanua kuwa miradi hiyo ina thamani ya Sh bilioni 27.76, ambapo Sh milioni 300.6 ni nguvu za wananchi, Sh bilioni 1.27 ni michango ya halmashauri, Sh bilioni 10.7 ni fedha za Serikali Kuu na Sh bilioni 15.47 ni mchango wa wahisani.


Akizungumzia kaulimbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu inayosema, “Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo,” Dk. Burian alisema mkoa umejipanga kuhakikisha wananchi wa makundi mbalimbali wanashiriki kikamilifu katika shughuli zote za Mwenge.


Alisema viongozi wa serikali, watumishi wa umma, viongozi wa dini, wanawake, vijana, watu wenye mahitaji maalumu pamoja na makundi mengine wamehamasishwa kushiriki kikamilifu kuanzia mapokezi hadi makabidhiano ya Mwenge wa Uhuru.


Aidha, wananchi watapata fursa ya kuushika na kuukimbiza Mwenge huo kama sehemu ya kuimarisha mshikamano, umoja wa kitaifa na ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.


Mbali na kuhamasisha maendeleo, Mwenge wa Uhuru utaendelea kutoa elimu kuhusu mapambano dhidi ya rushwa, malaria, VVU/UKIMWI, matumizi ya dawa za kulevya pamoja na umuhimu wa lishe bora kwa jamii.


Dk. Burian aliwataka wananchi wa Mkoa wa Tanga kujitokeza kwa wingi katika maeneo ya mapokezi, miradi na mikesha mbalimbali ili kushiriki shughuli za Mwenge wa Uhuru na kufaidika na ujumbe wake.


Alisema mkoa umejipanga kikamilifu kuhakikisha wananchi wanapata burudani na hamasa kupitia ushiriki wa wasanii na vikundi vya sanaa vitakavyoshiriki katika maeneo yote ambayo Mwenge wa Uhuru utakesha.



Sunday, June 14, 2026

PROF. SHEMDOE AIELEKEZA KAMPUNI YA CRBC KUKAMILISHA UJENZI WA BARABARA 7 UBUNGO IFIKAPO AGOSTI 14, 2026

Na OWM - TAMISEMI, Dar es Salaam

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe ametaka Mkandarasi kampuni ya China Railways and Bridges Corporation (CRBC) inayojenga barabara tisa (9) za lami zenye urefu wa kilometa 5.42 kukamilisha ujenzi wa barabara saba (7) zilizosalia ifikapo Agosti 14, 2026, barabara hizo zinajengwa kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II) katika kata za Sinza, Mburahati, Mabibo na Makurumla wilayani Ubungo.

Prof. Shemdoe ametoa maelekezo hayo Juni 13, 2026 Katika Manispaa ya Ubungo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua ujenzi wa barabara 23 zenye urefu wa kilometa 52.37 zinazojengwa wilayani Ubungo katika kata 11 kupitia utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).

Prof. Shemdoe amesitiza kuwa, mkandarasi huyo anayesuasua katika ujenzi wa barabara hizo kwa kisingizio cha lami kuchelewa kufika kutokana na vita ya Mashariki ya Kati, hatopewa muda wa nyongeza wa kukamilisha ujenzi wa barabara hizo iwapo atashindwa kukamilisha ifikapo Agosti 14, 2026 kwa mujibu wa mkataba.

“TARURA hakuna kumuongezea muda mkandarasi huyu, atafute lami popote atakapoipata na afanye kazi usiku na mchana kukamilisha barabara hizi 7 zilizosalia ili kuwaondolea adha wananchi,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Katika kuhakikisha barabara zinakamilika kwa wakati, Prof. Shemdoe ameitaka TARURA na Mshauri Elekekezi (NIMETA Consult (T) kumshauri mkandarasi CRBC kwa kuangalia uwezekano wa kukabidhi baadhi ya barabara hizo kwa mkandarasi mwingine (sub contract) ili ujenzi ukamilike kwa wakati.

Aidha, Prof. Shemdoe amemuelekeza Mtendaji Mkuu wa TARURA Mhandisi Victor Seff kumuondoa Mkuu wa Kitengo cha Fedha na Uhasibu Bw. Evans Mgeusa anayesimamia Fedha za Miradi ya Benki ya Dunia kwa kitendo cha kuchelewesha malipo na kumleta mwingine ambaye atafanya kazi kwa weledi na wakati.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemuelekeza Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI Bw. Adolf Ndunguru kuwaondoa Wahasibu Bw. Julius Bashuta na Mbwana Mkembe wa kitengo hicho cha Fedha na Uhasibu kinachosimamia  fedha za miradi ya Benki ya Dunia, na kuwaleta wengine ambao watafanya kazi vizuri na kwa uaminifu. 

Akizungumzia jitihada za Serikali ya Awamu ya Sita, Prof. Shemdoe amempongeza Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha utiaji saini wa mikataba minne ya ujenzi wa barabara za wilaya ya Ubungo yenye thamani ya shilingi bilioni 77, 457,169,172.73 kupitia Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).

Kwa upande wake Mkazi wa Sinza Bw. Jawa Waziri amemshukuru Prof. Shemdoe kwa kufanya ziara ya ukaguzi wa barabara ya mtaa wake wa Sinza Lion na kumpongeza kwa kumuelekeza mkandarasi CRBC kukamilisha kwa wakati barabara hiyo ambayo imekuwa ni kero kwa wakazi wa eneo hilo.










STAMICO YATAMBULIWA KAMA SHIRIKA BORA LA MADINI TANZANIA


DAR ES SALAAM

Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) limeendelea kuthibitisha ubora wake barani Afrika baada ya kutwaa tuzo mbili muhimu katika Tuzo za Kampuni Bora za Mwaka Afrika (Africa Company of the Year Awards - ACOYA).

Katika hafla ya utoaji wa tuzo hizo iliyofanyika Juni 12, 2026 katika Ukumbi wa Superdome, Oysterbay jijini Dar es Salaam, STAMICO iliibuka mshindi mkubwa wa usiku huo kwa kujinyakulia tuzo ya Shirika Bora la Madini la Mwaka Tanzania pamoja na Tuzo Kuu ya Mshindi wa Jumla wa ACOYA, ambayo ndiyo tuzo kubwa zaidi ya hafla hiyo.

Tuzo hizo zilipokelewa kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa STAMICO, Dkt. Venance Mwasse, na Meneja wa Masoko na Uhusiano wa Umma wa shirika hilo, Deus Alex Ntukamazina.

Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kupokea tuzo hizo, Ntukamazina alisema ushindi huo ni wa pili mfululizo kwa STAMICO katika tuzo hizo za bara la Afrika, jambo linaloonesha mafanikio makubwa ya mabadiliko yanayoendelea ndani ya shirika hilo.

Alisema tuzo hizo ni uthibitisho wa kutambuliwa kwa juhudi, ubunifu na kujitolea kwa watendaji wa STAMICO katika kuligeuza shirika hilo kuwa miongoni mwa taasisi zenye ufanisi na kuaminika zaidi katika sekta ya madini.

“Kwa shirika letu, huu ni ushahidi kwamba kazi kubwa inayofanyika katika kulibadilisha STAMICO inatambuliwa na kuthaminiwa. Ni matokeo ya juhudi za pamoja za kuhakikisha tunatoa mchango mkubwa katika maendeleo ya sekta ya madini nchini,” alisema Ntukamazina.

Alipoulizwa kuhusu siri ya mafanikio ya STAMICO kutoka kuwa shirika lililokuwa likikabiliwa na changamoto miaka iliyopita hadi kuwa taasisi inayoshinda tuzo za kimataifa, Ntukamazina alieleza kuwa uongozi bora na mipango ya kimkakati ndiyo msingi wa mafanikio hayo.

Alimpongeza Dkt. Mwasse kwa uongozi wake thabiti, bunifu na wenye maono ambao umewezesha STAMICO kupanua shughuli zake za kibiashara, kuongeza gawio kwa Serikali na kuimarisha ushirikiano na wachimbaji wadogo pamoja na wawekezaji wakubwa katika sekta ya madini.

Kwa ushindi huo wa tuzo mbili za bara la Afrika, STAMICO imeendelea kuipeperusha vyema bendera ya Tanzania na kuweka viwango vya juu vya utendaji kwa mashirika ya umma barani Afrika.

Saturday, June 13, 2026

SHEIKH PEMBE ASISITIZA KUHUSU UMUHIMU WA AMANI, ATAKA WAISLAMU KUILINDA NCHI YAO



Imamu Mkuu Masjid Mtambani Sheikh Shabani Pembe amewataka Waislamu na Watanzania wote kwa ujumla kuendelea kudumisha na kuilinda amani ya Tanzania, akisisitiza kuwa ikiwa serikali ingeruhusu kufanyika kwa kile kilichokuwa kimepangwa, kuratibiwa na kuhamasisha Oktoba 29, 2025 basi Tanzania isingeweza kukalika tena kutokana na uvunjifu wa amani ambao ungetokea wakati ule wa Uchaguzi.

Sheikh Shabani Pembe amebainisha hayo wakati akitoa hotuba yake kwa waumini wa Dini ya Kiislamu Mkoani Dar Es Salaam na kuwataka Waislamu kuhukumu kile kilichotokea kwa uadilifu pamoja na kupima athari ambazo zingeweza kujitokeza ikiwa serikali ingewaaacha wale waliokuwa wamejitokeza barabarani kuendelea na matukio yao ya uvunjifu wa amani Nchini.

"Kituo chetu cha mwendokasi tumeshuhudia kikichomwa, Vituo vya Polisi vilichomwa, ATM pale Manyanya imechomwa na hata maduka ya watu yamechomwa na kuibiwa, hawa watu wangeachiwa wafanye wanavyotaka hii Nchi ingekuwa wapi? Ndugu zangu tunapohukumu tuhukumu kwa uadilifu, kwamba lengo lilikuwa waachiwe wafanya wanavyotaka? Au ilikuwa nini? Baadae wale wote waliowachochea wanaanza kuiona dola mbaya, Tunapohukumu mambo tuhukumu kwa uadilifu." Amesema Sheikh Pembe.

"Tunapohukumu mambo tuhukumu kwa uadilifu, amani ni tunu ndugu zangu, ikiondoka hii hata sisi hatuwezi kukusanyika. Ile Ijumaa ile kutoka Tegeta mpaka hapa nililipa Elfu sitini kwa bodaboda na nimefika hapa naambiwa Mufti ametangaza hakuna ibada hapa, sasa waislamu niwaombe kuipenda Nchi yako ni katika Imani. Wale wote waliokuwa wanahamasisha yale ya Oktoba 29 hakuna hata mtoto wao aliyeguswa na kiwembe, tafsiri yake ni kuwa wao na familia zao zilibaki salama, kinyume chake familia za maskini na fukara ndio waliotolewa kafara." Ameongeza kusema.

Sheikh Pembe amewakosoa vikali pia wale wanaokosoa Tume zilizoundwa kuchukua matukio hayo ya wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, akisisisitiza kuwa Tanzania ni huru na Watanzania wanapaswa kuunga mkono busara na hekima za Viongozi wao katika kupata muafaka na suluhu ya kudumu dhidi ya kile kinachotajwa kama sababu ya matukio ya Oktoba 29, 2025.

Friday, June 12, 2026

SERIKALI YAOMBA AWAMU YA PILI YA MRADI WA MAZIWA FAIDA KUANZA MWAKA 2027

 


NA REBECA DUWE TANGA 


Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeomba kuendelea kwa ushirikiano kati ya Tanzania na Ireland kupitia utekelezaji wa Awamu ya Pili ya Mradi wa Maziwa Faida kuanzia mwaka 2027 hadi 2032, ili kuendeleza mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kuimarisha uzalishaji wa maziwa, kuongeza tija na kuboresha maisha ya wafugaji nchini.



Ombi hilo limetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Dkt. Fabian Madele, wakati akifungua rasmi Maonesho ya Ubunifu na Teknolojia katika Sekta ya Maziwa (TALIRI Open Day 2026) yaliyofanyika katika Kituo cha Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI) Kanda ya Mashariki, jijini Tanga.



Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Madele amesema Mradi wa Maziwa Faida unaotekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania kupitia TALIRI na Taasisi ya Maendeleo ya Kilimo na Chakula ya Ireland (TEAGASC), kwa ufadhili wa Serikali ya Ireland kupitia Ubalozi wa Ireland nchini Tanzania, umeleta mageuzi makubwa katika sekta ya maziwa, hususani katika Mkoa wa Tanga.



Dkt. Madele amesema kabla ya kuanza kwa mradi huo, wafugaji wengi walikuwa wakizalisha wastani wa lita 3 hadi 5 za maziwa kwa ng’ombe mmoja kwa siku. Kupitia matumizi ya teknolojia bora za ufugaji, malisho bora, huduma za ugani zilizoimarishwa na mafunzo kwa wafugaji, uzalishaji umeongezeka hadi wastani wa lita 15 kwa ng’ombe mmoja kwa siku katika maeneo mengi yaliyofikiwa na mradi.


“Matokeo haya yanaonesha wazi mchango mkubwa wa utafiti, ubunifu na ushirikiano wa kimataifa katika kuongeza tija, kuboresha kipato cha wafugaji na kuimarisha usalama wa chakula na lishe nchini,” alisema Dkt. Madele.


Aidha, Dkt. Madele amesema kuwa Tanzania kwa sasa inazalisha takribani lita bilioni 4.1 za maziwa kwa mwaka, wakati mahitaji ya taifa yanakadiriwa kufikia lita bilioni 13 kwa mwaka, amesema hali hiyo inaonesha uwepo wa fursa kubwa ya kuwekeza zaidi katika uzalishaji wa maziwa ili kupunguza pengo la mahitaji na kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.


Kwa upande wake, Mwakilishi wa Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Bi. Suzanne Keatinge, ameipongeza TALIRI kwa utekelezaji mzuri wa Mradi huo na kuwatambua watafiti, wataalamu wa ugani na wadau wote waliochangia mafanikio ya mradi huo.


Nae Mkurugenzi Mkuu wa TALIRI Prof. Erick Komba, ameishukuru Serikali ya Ireland kwa ufadhili wake na kueleza kuwa mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Mradi wa Maziwa Faida (2021/2022–2025/2026) yameweka msingi imara wa kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika sekta ya maziwa nchini.


Prof. Komba alisema TALIRI itaendelea kuhakikisha kuwa matokeo ya tafiti, ubunifu na teknolojia zilizozalishwa kupitia mradi huo zinawafikia wafugaji wengi zaidi nchini kwa lengo la kuongeza uzalishaji, tija na ushindani wa sekta ya maziwa.


Aliongeza kuwa Mradi wa Maziwa Faida, uliogharimu zaidi ya Euro milioni 3 sawa na zaidi ya Shilingi bilioni 7 za Kitanzania, umenufaisha zaidi ya wanawake na vijana 3,000 katika ukanda wa pwani ya mashariki, hususan Wilaya ya Muheza mkoani Tanga.


Kwa mujibu wa Prof. Komba, mafanikio makubwa ya mradi huo ni pamoja na kufanya tafiti za malisho bora yanayostahimili mazingira ya ukanda wa pwani, kubaini aina bora za ng’ombe wa maziwa, kuwajengea uwezo maafisa ugani, kutoa mafunzo kwa wafugaji, kuimarisha vyama vya ushirika vya wafugaji, kuboresha miundombinu ya utafiti pamoja na kuanzisha mashamba darasa ambayo yamekuwa vituo muhimu vya kujifunzia na kusambaza teknolojia za kisasa za ufugaji wa ng’ombe wa maziwa.


Mradi wa Maziwa Faida unatajwa kuwa mfano bora wa ushirikiano wa maendeleo unaochochea matumizi ya utafiti na ubunifu katika kutatua changamoto za uzalishaji wa maziwa na kuchangia ukuaji endelevu wa sekta ya mifugo nchini Tanzania.

TANZANIA NA GIZ ZASAINI MAKUBALIANO YA KUIMARISHA USHIRIKISHWAJI WA WANAWAKE KATIKA TEKNOLOJIA ZA KIDIJITALI.



Na Mwandishi Wetu, WMJJWM Dar Es Salaam

Serikali ya Tanzania na Ujerumani zimesaini Makubaliano ya Utekelezaji wa Mradi wa Kituo cha Mabadiliko ya Kidijitali Tanzania (Digital Transformation Centre – DTC Tanzania), utakayochochea ushiriki wa wanawake na wasichana katika uchumi wa kidijitali kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini baina ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Ujerumani (GIZ) iliyofanyika jijini Dar es Salaam Juni 11, 2026, Mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Bw. Badru Alburnoor amesema makubaliano hayo yanafungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya nchi ya Tanzania na Ujerumani katika kuhakikisha wanawake na wasichana wanapata fursa sawa za kushiriki na kunufaika na maendeleo ya teknolojia za kidijitali.



Amesema mradi huo unaendana kikamilifu na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Jinsia na Wanawake ya mwaka 2023, Mpango wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili dhidi ya Wanawake na Watoto pamoja na Mkakati wa Uchumi wa Kidijitali wa mwaka 2024–2034.


“Teknolojia za kidijitali zimekuwa nyenzo muhimu katika kubadilisha namna wananchi wanavyojifunza, kufanya kazi, kupata huduma na kushiriki katika shughuli za maendeleo. Serikali inaona umuhimu wa kuhakikisha wanawake na wasichana hawabaki nyuma katika mabadiliko haya, bali wanakuwa sehemu ya nguvu kazi na wabunifu wa teknolojia zinazochochea maendeleo ya taifa,” amesema Alburnoor.


Ameongeza kuwa kabla ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, Wizara kwa kushirikiana na GIZ tayari imefanikiwa kutekeleza programu mbalimbali zilizolenga kukuza ushiriki wa wanawake katika sekta ya teknolojia, kuimarisha ujuzi wa kidijitali na kuhamasisha ubunifu unaotumia teknolojia katika kutatua changamoto za kijamii na kiuchumi.

Kwa mujibu wa Alburnoor, Mradi wa DTC Tanzania unalenga kuendeleza suluhisho za kidijitali zinazobuniwa ndani ya nchi huku ukijenga mazingira jumuishi ya ushiriki katika uchumi wa kidijitali kwa kuimarisha ujuzi wa kidijitali, mifumo ya ubunifu na matumizi ya teknolojia zinazoboresha maisha ya wanawake na wasichana.


Amefafanua kuwa utekelezaji wa mradi huo utajikita katika maeneo matatu makuu, ikiwemo kuandaa mkakati wa Wizara wa kuimarisha usawa wa kijinsia unaozingatia fursa na changamoto za matumizi ya teknolojia za kidijitali, kuwajengea uwezo wawakilishi 200 kutoka taasisi za Serikali na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kutumia mbinu za kidijitali katika shughuli zao za kila siku, pamoja na kuwafikia Watanzania 100,000 kupitia suluhisho za kidijitali zinazokuza usawa wa kijinsia na haki za binadamu.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkaazi wa Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZA ) Anne Hahn amesema GIZ kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania inaendelea na maandalizi ya kuanzisha Maabara ya Ubunifu wa Kidijitali (Digital Fabrication Lab) pamoja na Kituo cha Ubunifu na Utengenezaji Teknolojia (Makerspace) kitakachohifadhiwa katika Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO).


Alisema vituo hivyo vitatoa fursa kwa wanawake na wasichana kupata mafunzo ya vitendo kuhusu teknolojia zinazoibuka, kutumia vifaa vya kisasa vya kidijitali na kushiriki katika ubunifu wa teknolojia unaoweza kuzalisha ajira na kuongeza kipato.

“Lengo letu ni kuwawezesha wanawake na wasichana kuhama kutoka kuwa watumiaji wa teknolojia pekee na kuwa wabunifu, wavumbuzi na wajasiriamali wa teknolojia watakaotoa mchango mkubwa katika uchumi wa kidijitali wa Tanzania,” amesisitiza.


Naye Mkuuwa Mahusiano Ubalozi wa Ujerumani nchini amebainisha kuwa mafanikio ya mabadiliko ya kidijitali yanahitaji ushirikiano mpana wa wadau mbalimbali, hivyo Wizara itaendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za umma, mashirika yasiyo ya kiserikali, taasisi za elimu na utafiti, vituo vya ubunifu pamoja na sekta binafsi.

Amesema ushirikiano huo utawezesha Tanzania kujenga jamii inayonufaika kwa usawa na maendeleo ya teknolojia, huku ikiimarisha ushirikishwaji wa wanawake na makundi mengine maalum katika shughuli za maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Makubaliano hayo yanatarajiwa kuwa chachu ya kuongeza ushiriki wa wanawake katika sekta ya teknolojia nchini na kuchangia utekelezaji wa ajenda ya Taifa ya kujenga uchumi wa kidijitali unaojumuisha wananchi wote bila ubaguzi.
















Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...