NA REBECCA DUWE TANGA
Moto mkubwa uliozuka majira ya saa 2:30 usiku wa kuamkia leo umeteketeza nyumba na maduka katika standi ya daladala iliyopo Barabara ya 12 jijini Tanga, na kusababisha wamiliki kukosa mahali pa kulala huku wakipoteza mali zao zote.
Akizungumza kwa masikitiko makubwa, mmoja wa waathirika wa janga hilo, Hamisi Abdalah, ameiomba Serikali kuwaangalia kwa jicho la huruma waathirika wa moto huo kutokana na kupoteza makazi na mali zao.
Abdalah alisema moto huo ulianza majira ya saa 2:00 usiku, baada ya moshi kuonekana katika chumba kimoja cha nyumba yake wakati akiwa amelala pamoja na mjukuu wake.
Alisema alifanikiwa kutoka nje ya nyumba hiyo akiwa na Mwanae wa miaka 6, lakini hakufanikiwa kuchukua hata simu yake ya mkononi.
“Ombi langu kwa Mama Samia ni kwamba atusaidie ili tuweze kupata mavazi, malazi na mahitaji mengine, kwani kwa sasa tumekaa bila kuwa na chochote,” alisema Abdalah.
Kwa upande wake, mmiliki wa maduka mawili, Godias Kimath, alisema tukio hilo wamelipokea kwa masikitiko makubwa baada ya maduka yote mawili kuteketea na hakuna mali iliyoweza kuokolewa.
Kimath alisema wakati akipata taarifa kuhusu tukio hilo alikuwa akitoka mazoezini, ndipo akaambiwa kuwa kulikuwa na harufu ya moshi katika eneo hilo.
Alisema alipofika katika eneo la tukio, awali hakuweza kuona moto, lakini baadaye walilazimika kutafuta msaada kutoka kwa Jeshi la Zima Moto na Uokoaji.
“Jeshi la Zima Moto lilipofika, moto ulikuwa tayari umeshika kasi na kuteketeza mali zilizokuwemo ndani ya maduka,” alisema Kimath.
Aidha, Kimath alisema pamoja na kupata hasara kubwa, anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumlinda na kumpa nguvu ya kuanza upya na kutafuta mali nyingine.
Moto huo umesababisha hasara kubwa kwa waathirika, huku chanzo cha moto huo kikiwa bado hakijafahamika.




























