Saturday, August 29, 2026

NDEJEMBI AAPISHWA IKULU! RAIS SAMIA ASEMA 'NAFASI IMEKABIDHIWA KWA KIJANA KAWATUMIKIE WATANZANIA BILA KUJALI TOFAUTI ZAO'

 Na Janeth Raphael - MichuziTv -Ikulu Chamwino


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema uamuzi wa kumteua Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ulizingatia sifa, uzoefu na uwezo wake wa kubeba dhamana kubwa ya uongozi wa taifa.

Rais Samia amesema nafasi hiyo imekabidhiwa tena kwa kijana, akimtaka Ndejembi kutumia fursa hiyo kujifunza, kukua kiakili na kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii na uaminifu kwa maslahi ya Watanzania.

Akizungumza leo, Agosti 29, 2026, katika hafla ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema uamuzi wa kumrudisha kijana katika nafasi hiyo ulifanyika kwa kauli moja.

“Kwa kauli moja tuliamua kuirudisha nafasi ya Makamu wa Rais kwa vijana na tuendelee kulea. Imetoka kwa kijana na tumeirudisha kwa kijana. Tunakuomba kijana (Ndejembi) ukakue sio kwa umri bali ukakue kiakili, tumekupa majukumu makubwa ni imani yangu utaweza,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema Ndejembi alipata uungwaji mkono wa wabunge kwa kauli moja kutokana na sifa alizonazo zinazomfanya astahili kushika nafasi hiyo.

“Wabunge walimpitisha Deogratius Ndejembi kwa kauli moja kwa kuzingatia sifa za Makamu wetu wa Rais,” amesema.

Amesema kabla ya kufikia nafasi ya Makamu wa Rais, Ndejembi amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na katika sekta binafsi, akieleza kuwa uzoefu huo utakuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

“Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi, kabla ya wadhifa huu, ulishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi. Sina shaka kwamba uzoefu huo utakusaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hii uliyopewa,” amesema Rais Samia.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hakuna shule maalumu inayomwandaa mtu kuwa Makamu wa Rais, bali uwezo wa kutekeleza majukumu hayo unajengwa kupitia sifa binafsi, bidii, weledi, nidhamu pamoja na utayari wa kujifunza na kusimamia utekelezaji wa majukumu.

Amesema sifa hizo zitamsaidia Ndejembi kutekeleza ipasavyo dhamana aliyopewa na taifa.

Rais Samia pia amesema uzoefu wa Ndejembi ndio uliowafanya viongozi kutokuwa na kusita katika kupitisha jina lake wakati wa kutafuta mtu wa kujaza nafasi hiyo.

“Kwa uzoefu huo ndio maana wakati tunatafuta mtu wa kujaza nafasi hii, hatukusita hata kidogo kupitisha jina lako. Hivyo ni matamanio na matarajio yetu sote Watanzania utalitumikia vyema, kwa utii, uaminifu, utu, busara, uzalendo, hekima, maarifa na uzoefu ulio nao, ukimtanguliza Mungu mbele na kwa maslahi ya taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amemtaka Ndejembi kwenda kuwatumikia Watanzania wote bila kujali tofauti zao, akisisitiza umuhimu wa kiongozi kuweka mbele maslahi ya taifa.

“Nenda ukawatumikie Watanzania bila kujali tofauti zao,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema serikali ina kazi kubwa ya kutekeleza ahadi zilizowekwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, sambamba na kuanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Amesema dira hiyo imebeba matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi, hivyo utekelezaji wake unahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora.

“Ili tuweze kutekeleza haya yote kwa maslahi ya wananchi wetu na taifa kwa ujumla, tunahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora,” amesema.

Uapisho wa Ndejembi unafungua rasmi ukurasa mpya katika safari yake ya uongozi wa kitaifa, huku akianza kutekeleza majukumu ya Makamu wa Rais chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan
















WANANCHI MATONGO NA NYANGOTO KUELIMISHWA KUHUSU UTHAMINI WA FIDIA NORTH MARA


NYAMONGO, MARA

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kupitia wataalamu kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, imefanya kikao na Kampuni ya Barrick North Mara Gold Mine pamoja na viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto, kwa lengo la kujadili maandalizi ya utoaji elimu kwa wananchi kuhusu zoezi la uthamini wa fidia linalohusishwa na upanuzi wa shughuli za Mgodi wa North Mara.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Diwani wa Kata ya Matongo, Mhe. Godfrey Mwita, amewataka viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto kushirikiana kwa karibu na wataalamu pamoja na wadau wote wanaohusika katika mchakato huo, akieleza kuwa wananchi wa maeneo hayo wanatarajiwa kuguswa na upanuzi wa shughuli za mgodi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mahusiano wa Kampuni ya Barrick, Bw. Francis Uhadi, amesema kampuni hiyo iko tayari kuanza mchakato huo kwa haraka, huku akisisitiza dhamira ya kampuni kuhakikisha haki na maslahi ya wananchi yanazingatiwa na kulindwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Akifafanua hatua zinazofuata, Mthamini Kiongozi kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, FRV. Baraka D. Mollel, amesema kikao hicho ni sehemu ya hatua muhimu kuelekea kuanza mchakato wa uthamini, baada ya hatua za awali zilizofanyika kwa kushirikisha Wizara ya Madini, ikiwemo tafiti na maandalizi mbalimbali.

Amesema hatua hizo zinalenga kuhakikisha zoezi la uthamini linafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, pamoja na kuwezesha wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu mchakato huo.

Naye Mtunzaji wa Bwawa la Mgodi, Bw. Majuto Kipande, ameeleza kuwa, tafiti za awali zilizofanyika wakati wa uanzishwaji wa mgodi zilionesha kuwa shughuli za uzalishaji zingefikia ukomo mwaka 2027. Hata hivyo, amesema tafiti zinazoendelea hivi sasa zinaonesha uwezekano wa uzalishaji kuendelea hadi kati ya mwaka 2031 na 2040.

Kwa mujibu wa Kipande, hali hiyo imeongeza umuhimu wa upanuzi wa bwawa la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu kutokana na bwawa linalotumika sasa kutaraji kufikia ukomo wa matumizi mwaka 2031.

Ameongeza kuwa, ujenzi wa bwawa jipya la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu unapaswa kukamilika kabla ya mwaka 2031, ili kuwezesha shughuli za mgodi kuendelea bila kuathiriwa na ukomo wa uwezo wa bwawa linalotumika sasa.

Mchakato wa uthamini unalenga kuhakikisha wananchi watakaoguswa na eneo la upanuzi wanapatiwa elimu na taarifa sahihi kuhusu hatua zinazochukuliwa, huku zoezi la uthamini wa fidia likitekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi.



















TMA YAWAONYA WAKAZI TANGA KUCHUKUA TAHADHARI DHIDI YA MVUA KUBWA

 


NA REBECA DUWE TANGA 


Wakazi wa Mkoa wa Tanga wametakiwa kuchukulia kwa uzito taarifa za utabiri wa hali ya hewa na kujiandaa kukabiliana na uwezekano wa kunyesha kwa mvua kubwa katika msimu ujao wa mvua, huku kukiwa na dalili za kuwepo kwa hali ya hewa ya El Niño.


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imeonya kuwa mvua hizo zinaweza kusababisha mafuriko na majanga mengine yanayohusiana na hali ya hewa, hususan katika maeneo ya mabondeni.


Meneja wa TMA Mkoa wa Tanga, Kurwa Mbwambo, alitoa tahadhari hiyo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Tanga, ambapo aliwataka wananchi pamoja na mamlaka zinazohusika na usimamizi wa majanga kutumia taarifa za hali ya hewa kuchukua hatua za tahadhari mapema.


Mbwambo alisema utabiri wa sasa unaonyesha kuwa mvua za msimu mfupi, maarufu kama mvua za Vuli, zinatarajiwa kuanza katika wiki ya kwanza ya Oktoba 2026 na kuendelea hadi Januari 2027.


Alisema viashiria vya hali ya hewa vinaonyesha kuwepo kwa hali ya El Niño, ambayo inaweza kuathiri mwenendo wa mvua katika maeneo mbalimbali nchini.


“Wananchi wasipuuze taarifa za utabiri wa hali ya hewa kwa sababu zinatolewa ili kuwawezesha kuchukua hatua za tahadhari na kulinda maisha pamoja na mali zao,” alisema Mbwambo.


Alisema uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika vifaa vya utabiri wa hali ya hewa pamoja na wataalamu umeboresha usahihi wa utabiri, ambapo kwa sasa utabiri wa hali ya hewa unafikia kiwango cha makadirio cha asilimia 94 cha usahihi.


Kwa mujibu wake, TMA tayari imewasilisha taarifa za kina za utabiri kwa Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri zote pamoja na mamlaka za wilaya, zikiwemo taarifa zinazoonyesha namna kila wilaya inavyoweza kuathiriwa na mvua hizo zinazotarajiwa.


“Tunatarajia mamlaka za wilaya tayari zimewasilisha, au zitawasilisha taarifa hizi kwa serikali za vijiji ili ziwafikie wananchi,” alisema.


Mbwambo aliwataka wananchi wanaoishi mabondeni na maeneo mengine yaliyo katika hatari ya mafuriko kuchukua tahadhari mapema badala ya kusubiri hadi mvua kubwa zianze kunyesha.


Aidha, aliwataka wananchi kusafisha mifereji ya maji inayozunguka makazi yao na katika maeneo ya jamii ili kuzuia kuziba na hatimaye kusababisha mafuriko.


Tahadhari hiyo inatolewa wakati TMA ikieleza katika mtazamo wake wa msimu wa mvua kuwa kutakuwa na shughuli kubwa za mvua katika maeneo kadhaa nchini zinazohusishwa na hali ya El Niño iliyopo.


TMA imeeleza kuwa ingawa mvua za Vuli zinatarajiwa rasmi kuanza mwezi Oktoba katika maeneo mengi, baadhi ya maeneo nchini yanaweza kuanza kupata mvua mapema kuanzia Septemba 2026.


Mamlaka hiyo pia imeonya kuwa hali ya El Niño kuelekea mwishoni mwa mwaka inaweza kusababisha msimu wa mvua unaoanza Novemba 2026 hadi Aprili 2027 kuanza mapema katika baadhi ya maeneo ambayo kwa kawaida hupata msimu mmoja mkuu wa mvua kwa mwaka.


Hata hivyo, TMA imesisitiza kuwa utabiri wa msimu hutoa mwelekeo wa hali ya hewa kwa maeneo mapana na vipindi vya miezi mitatu. Kwa hiyo, mabadiliko ya muda mfupi katika mwenendo wa mvua yataendelea kufuatiliwa kupitia utabiri wa muda wa kati na mfupi.


Wananchi na mamlaka wameelekezwa kuendelea kufuatilia taarifa mpya za hali ya hewa zinazotolewa na TMA na kuzitumia katika kupanga maandalizi pamoja na hatua za kupunguza hatari ya majanga.


Kwa Mkoa wa Tanga, ambako baadhi ya jamii zinaishi katika maeneo yaliyo hatarini kukumbwa na mafuriko, ujumbe wa Mbwambo ni muhimu zaidi wakati maandalizi ya kukabiliana na msimu ujao wa mvua yakishika kasi.



Friday, August 28, 2026

SERIKALI YAZINDUA 'UGHAIBUNI LOAN'

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Dkt. Evaline Munisi (wa tatu kutoka kushoto) akizindua rasmi Ughaibuni Loan wakati wa hafla ya kuwaaga Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya  nchi, wakati wa hafla hiyo iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam tarehe 27 Agosti, 2026.

****************

-Kuwezesha vijana kumudu mahitaji ya msingi anapoenda kufanya kazi nje ya nchi

Na: OWM (KAM), Dar es Salaam

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana nchini wanaendelea kunufaika na fursa za nje ya nchi na zenye staha kwa kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Agosti 27,2026 wakati wa uzinduzi wa mkopo wa Ughaibuni Loan unaoratibiwa na Benki ya CRDB pamoja na kuwaaga vijana 130 kati ya 530 wanaotarajia kwenda kufanya kazi nje ya nchi, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Dkt. Evaline Munisi amesema Serikali inatambua ajira za nje ya nchi kama nyenzo muhimu ya kupanua fursa za ajira, kuongeza kipato cha vijana, kukuza ujuzi na kuwajengea uzoefu wa kimataifa.

“Matokeo ya jitihada hizi yamewezesha Watanzania 14,613 kupata ajira nje ya nchi tangu Serikali ya Awamu ya Sita kuingia madarakani. Kati ya Julai 2025 hadi sasa, Watanzania 8,428 wameunganishwa na waajiri nje ya nchi,” amesema Dkt. Munisi.

Amesema mafanikio hayo yameifanya Tanzania kuendelea kuaminika kuwa na nguvu kazi salama na yenye staha duniani.

Kuhusu uzinduzi wa Ughaibuni Loan, Dkt. Munisi amesema mkopo huo unalenga kuwawezesha vijana waliopata ajira nje ya nchi kupata fedha nafuu za kugharamia maandalizi ya safari ikiwemo tiketi ya ndege, bima na visa.

“Ughaibuni Loan siyo msaada bali ni mkopo wa uwezeshaji. Nawasihi vijana wahakikishe wanafanya marejesho ili na wengine wapate fursa,” amesisitiza.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CRDB, Bw. Pendason Philemon amesema benki imetenga jumla ya Shilingi bilioni 250 kwa miaka mitano kutoa mikopo ya kati ya Sh. 500,000 hadi milioni 20 kwa kila kijana kulingana na gharama za kufika kwa mwajiri wake.

“Kigezo muhimu ni kuwa na mkataba au barua ya ajira iliyothibitishwa na wakala. Marejesho yatakuwa kwa miezi 24 na tunatoa kipindi cha neema cha miezi 2 kwa riba ya asilimia 15,” amesema Philemon.

Mwenyekiti wa Chama cha Mawakala Binafsi wa Ajira TRAA, Bw. Abdala Khalid amesema mkopo huo utawaepusha vijana na watu wasio na nia njema.

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Bi. Zuhura Yunus amesema Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi,Ajira na Mahusiano inaendelea kutafuta masoko ya uhakika ya ajira ikiwemo Saudi Arabia, Oman, Qatar, Denmark na Ujerumani.

Mmoja wa wanufaika, Dickson Tadeo Mbaga amesema kupitia mkopo huo aliweza kugharamia visa, tiketi na bima. “Ninawasihi vijana wenzangu wachangamkie fursa hii,” amesema.

Serikali imesema itaendelea kuhakikisha vijana 530 wanaokwenda kufanya kazi ughaibuni katika fani mbalimbali ikiwemo ujenzi wanalindwa na kazi zao zinakuwa zenye staha.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Dkt. Evaline Munisi akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ughaibuni Loan pamoja na tukio la kuwaaga na Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya  nchi, iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Agosti, 2026.
Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Bi. Zuhura Yunus akieleza jambo wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ughaibuni Loan pamoja na tukio la kuwaaga na Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya  nchi, iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Agosti, 2026.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB, Bw. Pendason Philemon akieleza manufaa ya Ughaibuni Loan wakati wa uzinduzi rasmi wa Mikopo kwa Wafanyakazi wanaofanya kazi nje ya nchi (Ughaibuni Loan) iliyofanyika katika Makao Makuu ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Agosti, 2026.


Baadhi ya Wadau na Vijana walionufaika na Ajira Nje ya Nchi wakifuatilia matukio wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ughaibuni Loan pamoja na tukio la kuwaaga na Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya  nchi, iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Agosti, 2026.
Naibu Waziri, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu - Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Dkt. Evaline Munisi akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa Ughaibuni Loan pamoja na tukio la kuwaaga na Watanzania wanaokwenda kufanya kazi nje ya  nchi, iliyofanyika Makao Makuu ya Benki ya CRDB, Palm Beach Jijini Dar es Salaam, tarehe 27 Agosti, 2026.

Thursday, August 27, 2026

Maktaba Mtandao Kuimarisha Huduma, Kuunganisha Mifumo ya Serikali

 


Na Rebeca Duwe Tanga 


Mfumo wa Maktaba Mtandao umeanza kuleta matokeo chanya katika utoaji wa huduma za maktaba nchini, huku ukitarajiwa kuongeza ufanisi wa upatikanaji wa taarifa na kurahisisha mawasiliano kati ya mifumo mbalimbali ya serikali na taasisi za elimu.



Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Huduma za Maktaba Tanzania (TLSB), Dkt. Mboni Ruzegea, amesema mfumo huo umejengwa kwa kuzingatia umuhimu wa mifumo ya serikali kusomana, jambo ambalo limekuwa likisisitizwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan.


Dkt. Ruzegea amesema tayari Maktaba Mtandao ina uwezo wa kuhusishwa na mifumo mbalimbali ya serikali, ikiwemo mifumo ya malipo ya serikali, madeni ya serikali pamoja na mifumo inayohusiana na sekta ya elimu, ikiwemo mfumo wa takwimu unaosimamiwa chini ya Wizara ya Elimu.


Amesema kuunganishwa kwa mifumo hiyo kutasaidia kurahisisha upatikanaji na matumizi ya taarifa, huku wananchi na wadau wa huduma za maktaba wakinufaika zaidi na teknolojia katika kupata huduma.


Dkt. Ruzegea ameyasema hayo alipokuwa akitoa ufafanuzi kuhusu kuanzishwa na kuanza kutumika kwa Maktaba Mtandao katika viwanja vya Usagara, ambako kulikuwa na Maonesho ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu.


Watunzi wa vitabu watakiwa kuwasilisha machapisho


Katika hatua nyingine, Dkt. Ruzegea amewataka waandishi na watunzi wa vitabu, majarida na machapisho mengine kuhakikisha wanawasilisha kazi zao katika Maktaba Kuu ya Taifa ili kupata namba ya utambulisho na kuwezesha machapisho hayo kuhifadhiwa kama sehemu ya kumbukumbu za taifa.


Kwa mujibu wa utaratibu huo, mwandishi anatakiwa kuwasilisha nakala mbili za chapisho lake. Hata hivyo, kutokana na mabadiliko ya teknolojia na kuongezeka kwa matumizi ya mifumo ya kidijitali, watunzi wanatakiwa pia kuwasilisha nakala ya kidijitali (soft copy) ya chapisho husika.


Dkt. Ruzegea amesema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha machapisho yanayotengenezwa nchini yanahifadhiwa kwa njia salama na yanaendelea kuwa sehemu ya hazina ya maarifa na kumbukumbu za Tanzania.


Kongamano la huduma za maktaba kurejea


Aidha, Dkt. Ruzegea amesema Bodi inatarajia kuandaa kongamano kubwa la huduma za maktaba, ambalo limekuwa likifanyika kila mwaka lakini lilisimama kwa kipindi cha miaka miwili.


Amesema kongamano hilo litakuwa na nafasi ya kujadili na kuendeleza huduma za maktaba nchini, huku Bodi ikitarajia kufanya urasimishaji wa Maktaba Mtandao, badala ya uzinduzi.


Amesema sababu ya kufanya urasimishaji badala ya uzinduzi ni kwamba huduma hiyo tayari imeanza kutumika na wananchi wanaendelea kunufaika nayo.


Chuo cha Ukutubi chafungua milango kwa Watanzania


Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Chuo cha Ukutubi na Uhifadhi Nyaraka, Bertha Mwaihojo, amewakaribisha Watanzania kujiunga na chuo hicho, akieleza kuwa ni miongoni mwa vyuo vikongwe nchini vinavyotoa mafunzo katika eneo la ukutubi na uhifadhi wa nyaraka.


Mwaihojo amesema chuo hicho kinaendeshwa na Bodi ya Huduma za Maktaba Tanzania na kinatoa mafunzo katika ngazi ya cheti na stashahada katika fani za ukutubi, uhifadhi wa nyaraka pamoja na utunzaji wa kumbukumbu.


Amesema katika kuendana na mahitaji ya soko la ajira na mabadiliko ya teknolojia, chuo hicho kinatarajia kuanzisha kozi mpya katika mwaka huu wa masomo, zikiwemo Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) na Business Information Technology.


Kwa mujibu wa Mwaihojo, chuo hicho kwa sasa kina kampasi mbili nchini, ambazo ni Bagamoyo na Dar es Salaam, hatua inayowapa fursa Watanzania kupata mafunzo katika eneo la ukutubi, uhifadhi wa nyaraka na teknolojia ya taarifa.


Teknolojia kuongeza ufanisi wa huduma za maktaba


Kwa ujumla, kuanza kutumika kwa Maktaba Mtandao kunaweka msingi wa kuifanya huduma ya maktaba iendane zaidi na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.


Mfumo huo unatarajiwa kurahisisha upatikanaji wa taarifa, kuhifadhi machapisho kwa njia ya kidijitali na kuongeza fursa kwa wananchi kupata maarifa bila kutegemea zaidi huduma za maktaba za kawaida.


Hatua hiyo pia inaipa Tanzania nafasi ya kuendelea kujenga mfumo wa kisasa wa kuhifadhi na kusambaza maarifa, sambamba na jitihada za serikali za kuunganisha mifumo na kuongeza matumizi ya teknolojia katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...