Tuesday, April 14, 2026

WACHIMBAJI MADINI MWABOMBA WASISITIZA UMUHIMU WA AMANI NA UTULIVU


Wachimbaji madini katika Mgodi wa Mwabomba, Kata ya Idahina, Jimbo la Ushetu, wameeleza kuwa amani na utulivu ni nguzo muhimu katika shughuli za uchimbaji, wakisema bila hali hiyo kazi zao haziwezi kufanyika kwa ufanisi wala kuleta tija kwao na taifa kwa ujumla.

Baadhi ya wachimbaji hao, akiwemo Juma Ngosha na Mabula Mayala, wamesema mazingira ya amani yamekuwa yakichochea ukuaji wa shughuli za uchimbaji, kuongeza uzalishaji na kuwavutia wawekezaji, huku wakibainisha kuwa migogoro au hali ya sintofahamu inaweza kuhatarisha usalama wao pamoja na uchumi wa eneo hilo.

Aidha, wachimbaji hao wameiomba serikali kuwapatia Soko la Dhahabu katika eneo la Mwabomba ili kuwawezesha kuuza madini yao kwa urahisi na kwa bei stahiki, badala ya kulazimika kusafiri umbali mrefu kufuata masoko yaliyopo. 

Wamesema uwepo wa soko hilo utasaidia kuongeza mapato yao na kudhibiti biashara holela ya madini.

Kwa upande wake, Serikali ya Halmashauri ya Ushetu imesema ipo katika maandalizi ya kuweka utaratibu wa kuanzisha Soko la Dhahabu Mwabomba, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuboresha sekta ya madini na kuongeza mapato ya halmashauri pamoja na wananchi.

Naye Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Emmanuel Cherehani, ameahidi kulifanyia kazi suala hilo, akieleza kuwa atashirikiana na mamlaka husika kuhakikisha wachimbaji wanapata soko litakalowarahisishia shughuli zao na kuchochea maendeleo ya eneo hilo.

ANTHONY GODFREY MARIKI : PROGRAMU YA BARRICK YA KUWEKEZA KATIKA KIZAZI KIJACHO CHA WATAALAMU WA SEKTA YA MADINI INA MANUFAA MAKUBWA KWA TAIFA

Anthony Mariki , katikati akipokea ufadhili wa kwenda kusoma chuo Kikuu cha Johannesburg Afrika kusini , Shahada ya Uhandisi wa Madini , kulia Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) , Profesa Willliam Anangisye na kushoto , Meneja Mkazi wa Kampuni ya Barrick Nchini, Dkt Melkiory Ngido
Anthony Maliki , wa kwanza kushoto waliosimama akiwa na wanafunzi wenzake waliopata ufadhili wa kwenda kusoma nchini Afrika Kusini Chuo cha Johannesburg, wakiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) , waliokaa wa kwanza kushoto , Meneja Rasilimali Watu wa Barrick nchini , Lumbu Kumbula, Meneja Mkazi wa Barrick nchini , Dkt Melkiory Ngido, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa William Anangisye na wa kwanza kulia ni Mkuu wa Shule ya Madini na Jiolojia (SOMG) Profesa Elisante Mshiu.

****

“Nikiwa ni miongoni mwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Johanesburg nchini Afrika ya Kusini nikisomea fani ya uhandisi wa madini kwa ufadhili wa kampuni ya Barrick Tanzania najivunia kuwa katika programu hii ya kuwapatia mafunzo wataalamu wa sekta ya madini wa siku zijazo na ninaamini  ina manufaa makubwa kwa Tanzania ambayo ni nchi yenye hazina kubwa ya madini ya aina mbalimbali” anasema Antony Godfrey Mariki.

Godfrey Mariki ni miongoni mwa wanafunzi watano wa mwaka wa kwanza kutoka shule ya Madini na Sayansi ya Miamba (SoMG) katika Chuo Kikuu cha Dar es  salaam walioshinda ufadhili (Scholarship) ya kampuni ya Barrick yenye ubia na Serikali ya Tanzania kupitia kampuni ya Twiga Minerals ambaye kwa sasa anasoma kozi ya uhandisi wa madini nchini Afrika ya Kusini.

Katika mahojiano yaliyofanyika karibuni kutokea nchini Afrika ya Kusini, Mariki amesema anayo furaha kuona yeye na wenzake wanaendelea vizuri katika masomo yao wakiwa wanapata msaada na ufuatiliaji wa karibu kutoka kwa mfadhili yaani kampuni ya Barrick na Chuo Kikuu cha Dar es salaam ambapo walikuwa wanasoma hapo awali.

”Ufadhili huu tuliopata naamini sio wa kifedha tu bali ni fursa ya kipekee ya kujiendeleza kitaaluma kwa kupata elimu bora kutoka chuo bora barani Afrika ikizingatiwa kuwa Afrika ya Kusini imeendelea zaidi katika sekta ya madini zaidi ya hapo katika vipindi vya likizo Barrick imetupatia fursa ya kupata mafunzo ya vitendo kwenye migodi yake ili tuweze kupata maarifa zaidi”,amesema Mariki.

Kuhusiana na progamu hii Mariki anasema kuwa  Barrick imeonyesha maono yake kwa kuwekeza kwenye elimu inaolenga kuboresha sekta ya madini nchini Tazania “Kupitia program hii ni dhahiri kwamba Barrick inaanda waaalamu  wazawa kutoka Tanzania watakaoendeleza na usimamia sekta ya madini katika siku za mbele ili kuhakikisha inatoa mchango mkubwa kwa ukuaji wa uchumi wa nchi sambamba na kuwanufaisha Watanzania”,amesema.

Mariki ameongeza kuwa anafurahi kuona Barrick mbali na kutoa ufadhili huu pia imekuwa na programu mbalimbali za mafunzo zinazolenga kuwajengea uwezo wataalamu wa sekta ya madini ikiwemo kuendesha semina za wanafunzi wanaosoma fani ya madini na utafii wa madini kwa kutumia wataalamu wa kampuni ambapo pia imekuwa ikitoa fursa kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kupata mafunzo ya vitendo katika migodi yake ya North Mara na Bulyanhulu.

Akielezea historia yake fupi ya elimu amesema elimu ya msingi alisoma katika Shule ya Royal iliyopo mjini Moshi na alipomaliza alichaguliwa kujiunga na Seminari ya St,James nayo ipo mkoani Kilimanjaro baadaye masomo ya juu ya sekondari katika shule ya Kisimiri ambayo imemjenga zaidi katika safari ya kutimiza ndoto yake akaweza kupata vigezo vya kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kusomea kozi aliyoipenda ya uhandisi wa Madini.

Mariki anaamini kuwa mafanikio yoyote yanapatikana kwa kuwa na bidii katika jambo lolote ambalo mtu anafanya na kutoa wito kwa vijana wenzake nchini kuchangamkia fursa zinazojitokeza kuanzia kwenye masomo,kazi,biashara na shughuli nyinginezo zote."Mafanikio yoyote maishani  yanahitaji kufanya kazi kwa bidii",amesisitiza.

 Anasema wakati serikali ya Tanzania inakwenda kasi katika kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo kwenye sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya madini,kunahitajiwa uwekezaji wenye mipango mikubwa utakaowezesha miradi mbalimbali ya kimkakati inayoendelea kuanzishwa kuwa endelevu na sio tu kuwekeza kwenye fedha na teknolojia bali kuwekeza pia katika kupata wataalamu wa kuendesha miradi kwa kipindi cha sasa na miaka ya mbele.

Ameendelea kueleza kuwa kuwa bila kufanya uwekezaji wenye mtazamo wa kujenga biashara endelevu kwa miaka mingi, kuna hatari ya biashara nyingi hususani katika sekta nyeti kama za madini,usafirishaji na mafuta kuendelea kutegemea wataalamu wa kigeni na watanzania kuachwa nyuma na kubaki kama watazamaji.

Anashauri kuwa kuna haja ya kuwapatia vijana wengi wa kitanzania fursa za kusoma fani zenye wataalamu wachache katika vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi sambamba na kuanzishwa Progamu mbalimbali za kuwanoa vijana wa kitanzania wahitimu wa vyuo vikuu na vyuo vya ufundi kwa kuwapatia mafunzo ya vitendo kwa ajili ya kuwaanda kwendana na mabadiliko yanayotokea katika kila sekta na kushika nafasi za uongozi katika siku za usoni.

Akiongea kuhusu kupata nafasi ya Ufadhili wa Barrick kusomea taaluma ya madini nchini Afrika ya Kusini Mariki, anaeleza kuwa anajivunia kuwa miongoni mwa wanafunzi wachache waliochaguliwa kwa kuwa ushindani wa kuipata nafasi ulikuwa mkubwa sambamba na mchujo mkali uliofanywa na wataalamu mbalimbali ili kuhakikisha na kujiridhisha kuwa wanachukua watu wenye uwezo, makini na waliopo tayari kujifunza."Nina uhakika tutafanya vizuri na kupata kile kilicho bora na kukirudisha kwa taifa katika kutumikia watanzania wote kwa manufaa ya nchi ",amesisitiza.

Anasema moja ya ndoto kubwa aliyokuwa nayo katika maisha yake ni kufanya kazi katika kampuni kubwa na zenye mifumo mizuri ya kazi, jambo ambalo linaelekea kutimia kutokana na kampuni ya Barrick kutangaza pia fursa kuwapatia ajira pindi watakapomaliza elimu sambamba na kuwapatia mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kufanya kazi kwa vitendo wakati wote watakapokuwa masomoni.

Kuhusu mambo yanayomvutia kutamani kufanya kazi katika kampuni ya Barrick amesema ni mengi mbali na kupata maslahi mazuri na utaalamu wa viwango vya kimataifa pia anavutiwa na jinsi inavyotekeleza  mkakati wake endelevu  wenye mtazamo wa kujenga jamii endelevu kwendana na utekelezaji wa malengo endelevu ya milenia ya umoja wa mataifa (MDGs).

"Inafurahisha kuona kampuni inayapa kipaumbele masuala ya msingi katika kujenga biashara endelevu kama vile utunzaji wa mazingira na vyanzo vya maji,usalama wa wafanyakazi wake ,kushirikiana na jamii zilizopo katika maeneo inakofanyia biashara zake kama ambavyo inafanya kazi na wazabuni wa ndani kuhakikisha inafanya manunuzi ya ndani ya nchini kwa asilimia kubwa ,kuendesha mafunzo ya ujasiriamali kwa wazabuni ili nao biashara zao zikuwe na kuwa endelevu bila kusahau kufanikisha miradi mbalimbali ya kusaidia jamii hususani katika sekta za elimu, ,afya, ,maji safi na salama na uboreshaji wa miundombinu ya barabara", amesema Samson.

Mariki, anaeleza kuwa anaamini kuwa hadi kufikia kuhitimu shahada yake ya kwanza nchini Afrika ya Kusini, atakuwa amejifunza mambo mengi yatakayomsaidia katika safari yake ndefu ya kuwa mtaalamu wa madini sambamba na kuwa mbunifu na kutoa mawazo ya kitaalamu yanayowezesha kukabili changamoto na kuwezesha sekta ya madini nchini Tanzania kusonga mbele kwa mafanikio makubwa.

Amemalizia kwa kutoa ushauri kwa wawekezaji wengine wanaotoka nje na ndani ya nchi kuiga mfano wa Barrick kwa kuwa na mtazamo wa kujenga biashara endelevu sambamba na kuwa na programu za kuandaa wataalamu wazawa kwa kuwawezesha kupata elimu na utaalamu kama ambavyo imedhamini wanafunzi watano kusomea utaalamu wa fani ya madini nje ya nchi.

"Programu kama hii ni muhimu kwa kuwanoa vijana wasomi kupata ujuzi wa viwango vya kimataifa ,natamani kuona pia idadi ya vijana wanaochukuliwa katika Programu hii kuongezwa zaidi ya sasa ili inufaishe vijana wengi wa kitanzania", amesisitiza.

Picha : CHEREHANI AFANYA MKUTANO MKUBWA WA SHUKRANI USHETU, DARAJA LA MWABOMBA 99% ...MABALA ASEMA 'NI MBUNGE WA VITENDO!

Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani akizungumza na wananchi katika kijiji cha Mwabomba Kata ya Idahina Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga - Picha na Kadama Malunde
Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani akikaribishwa katika kijiji cha Mwabomba kata ya Idahina Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga.

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Mbunge wa Jimbo la Ushetu, Mhe. Emmanuel Cherehani amefanya ziara muhimu ya kukagua na kuhimiza utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Kata ya Idahina, Halmashauri ya Ushetu, sambamba na kufanya mkutano mkubwa wa shukrani kwa wananchi waliomchagua kuwa mbunge wao.

Katika ziara hiyo iliyofanyika leo Jumatatu Aprili 13, 2026 Mhe. Cherehani ametembelea Mradi wa Ujenzi wa Daraja la Mwabomba uliokamilika kwa asilimia 99 na tayari kuanza kutumika, pamoja na kuzindua rasmi ujenzi wa Kituo cha Afya Mwabomba (Idahina), hatua inayolenga kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Mwabomba, Mhe. Cherehani ametoa shukrani zake kwa wananchi pamoja na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinachoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, akisisitiza dhamira yake ya kuwatumikia wananchi kwa uaminifu.
“Leo Aprili 13, 2026 ni siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwangu, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima sote wananchi wa Ushetu. Nimekuja kusherehekea nanyi na kusema neno moja tu  ‘Asante’. Asanteni sana kwa kunichagua kuwa Mbunge wenu na kwa kumchagua Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa Rais na madiwani wa CCM” amesema Cherehani.

Mbunge huyo ameeleza kuwa serikali imetoa shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Mwabomba, ambalo sasa limeanza kuwahudumia wananchi bila hofu, huku akitangaza kukabidhi shilingi milioni 657 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Idahina.

“Nimekuja kuwakabidhi kiasi cha shilingi milioni 657 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na wananchi wasichangishwe hata shilingi mia. Tayari milioni 250 zipo kwenye akaunti, nataka ujenzi uanze mara moja ili wananchi waanze kupata huduma,” amesisitiza.

Aidha, ametoa maagizo kwa watendaji wa sekta ya afya kuhakikisha huduma kwa wajawazito zinatolewa bila malipo, akipiga marufuku vitendo vya kuwatoza fedha.

“Ni marufuku kumtoza hata shilingi 10 mama mjamzito. Wapokeeni, wapimeni na wahudumieni. Hawa ni wananchi wa kawaida, wanashinda mashambani ,wanatoa wapi fedha?” amehoji.
Mbali na afya, Mhe. Cherehani amezungumzia mipango ya maendeleo ikiwemo upatikanaji wa maji kupitia mradi wa Ziwa Victoria, ufunguzi wa soko la dhahabu Mwabomba na utatuzi wa changamoto za wafugaji kupata maeneo ya malisho.

Katika mkutano huo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Mabala Mlolwa aliyekuwa mgeni rasmi amempongeza Mhe. Cherehani kwa kusimamia kwa vitendo miradi ya maendeleo.
“Ushetu mna mbunge mchapakazi, mmelamba dume sana, ni mbunge wa Vitendo, Cherehani inashona maendeleo kweli kweli Ushetu. Ni vigumu kupata kiongozi mwenye upendo na jitihada kama hizi. Daraja la Mwabomba sasa linapitika, wananchi wanavuka bila hofu,” amesema Mlolwa.

Ameongeza kuwa miradi hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM na maono ya Serikali ya kuwaletea wananchi maendeleo ya kweli, huku akihimiza wananchi kuendelea kudumisha amani, mshikamano na kuunga mkono serikali yao ili kuharakisha maendeleo zaidi.

Ameongeza kuwa wananchi wanapaswa kuendelea kuunga mkono juhudi za serikali na kudumisha amani, akibainisha kuwa maendeleo yanayoonekana ni matokeo ya sera na utekelezaji wa CCM chini ya uongozi wa Rais Samia.

Mradi wa Daraja la Mwabomba kwenye barabara ya Masumbwe–Mwabomba unaounganisha mikoa ya Shinyanga na Geita, umetekelezwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kushirikiana na mkandarasi M/s Jossam & Co. Ltd, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maagizo ya Rais Samia kufuatia uharibifu wa miundombinu uliotokea hapo awali.
@malundeblog

Mbunge wa Jimbo la Ushetu Mhe. Emmanuel Cherehani amefanya mkutano mkubwa wa kuwashukuru wananchi kwa kumchagua kuwa Mbunge. Akiwa ameambatana na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mabala Mlolwa, Mbunge Cherehani amesherehekea Siku ya Kuzaliwa na Wananchi wa Kijiji cha Mwabomba kata ya Idahina. Hali kadhalika amekagua daraja la Mwabomba ambalo limekamilika kwa asilimia 99 pamoja na kukabidhi fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Mwabomba! Tazama hivi Vibe!!

♬ original sound - Malunde
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...