Thursday, June 11, 2026

NAMNA VITUO VYA KULELEA WATOTO YATIMA NA WANAOTOKA KWENYE MAZINGIRA MAGUMU VILIVYOSAIDIA KUPUNGUZA UKATILI KWA WATOTO.


Na Linda Mosseka-Manyara

Watoto ni taifa la kesho, msemo huu umezoeleka masikioni mwa wengi ukiwa umebeba maono makubwa ya maisha ya watoto wa kitanzania katika kuwaandaa kuwa watu muhimu kwenye jamii pale wanapofikisha umri wa utu uzima, ili waweze kulisaidia taifa kusonga mbele kimaendeleo kwa kutumia ujuzi, maarifa na vipaji walivyonavyo.

Mara nyingi mchakato wa watoto kuzifikia ndoto zao hukumbwa na mambo mengi mazito ikiwemo changamoto ya kiuchumi, maradhi na kubwa zaidi ni ukatili wanaofanyiwa kwenye jamii inayowazunguka hasa wazazi na ndugu wengine wakaribu wanaowategemea.

Kutokana na changamoto ya ukatili kuongezeka nchini kwa kiwango kikubwa, wadau mbalimbali kwa kushirikiana na serikali waliguswa kuwasaidia watoto wanaopitia changamoto mbalimbali kwa kuandaa vituo maalum vya malezi  ili kuhakikisha wanafikia ndoto zao.

Utaratibu wa kuanzisha vituo hivyo unasimamiwa na wizara ya maendeleo ya jamii jinsia wanawake na makundi maalum, kuanzia kwenye usajili na kuratibu namna vituo hivyo vinavyoendeshwa.

Vituo hivi ni vya binafsi, vinasajiliwa kama mashirika yasiyo ya kiserikali chini ya sheria inayosimamia mashirika hayo ya mwaka 2002 kifungu cha 56 na marejeo yake.

Katika makala hii tunaangazia ni kwa namna gani vituo hivyo vya kulelea watoto yatima na wanaotoka kwenye mazingira magumu vimesaidia kupunguza ukatili kwa watoto, ambatana nami kuanzia mwanzo hadi tamati ya makala hii jina langu ni Linda Moseka.

Kwa mujibu wa sheria za nchi ikiwemo katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na sheria ya mtoto ya mwaka 2009 zinaweka bayana kuwa mtoto ni binadamu yeyote mwenye umri chini ya miaka 18, na anastahili haki za msingi kama binadamu wengine ikiwemo haki ya kuishi, kulindwa kupata malezi bora, elimu na afya bora.

Kila kukicha nchini Tanzania na duniani kwa ujumla kumeripotiwa matukio mbalimbali ya ukatili dhidi ya watoto yanayopelekea watoto kushindwa kupata haki zao za msingi na badala yake wanajikuta kwenye dimbwi la mateso na manyanyaso yanayosababisha msongo wa mawazo na kupelekea  kufanya maamuzi magumu ikiwemo kujitoa uhai.

Kwa mujibu wa tafiti za shirika la afya duniani WHO takribani watoto bilioni moja wenye umri wa miaka 2-17 hupitia aina mbalimbali za ukatili kila mwaka ikiwemo ukatili wa kisaikolojia, kutokana na adhabu kali kutoka kwa wazazi au walezi wao.

Kwa upande wa tafiti za shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto UNICEF 2025 zimeonesha kuwa watoto 6 kati ya 10 wenye umri wa miaka 2-14 hupitia ukatili wa kisaikolojia  wakiwa nyumbani ikihusisha kutukanwa, kufokewa kwa ukali au kudhalilishwa na wazazi au walezi wao.

Ripoti hiyo imeendelea kuonesha kuwa bara la Afrika ni miongoni mwa maeneo yenye viwango vya juu zaidi vya tatizo hili kwani takribani asilimia 80 ya watoto hupitia adhabu za vurugu nyumbani zinazojumuisha vipengele vya ukatili wa kisaikolojia na kimwili.

Nchini Tanzania utafiti wa kitaifa  wa ukatili dhidi ya watoto (VACS) wa mwaka 2024 ulionesha takribani asilimia 25 ya wasichana na asilimia 31 ya wavulana walipata ukatili wa kisaikolojia kutoka kwa watu wazima kabla ya kufikisha miaka 18.

Mtiririko wa ripoti hizi unaonesha wazi kuwa bado changamoto ya ukatili kwa watoto katika jamii ni kubwa na mikakati ya ziada inahitajika ili kuhakikisha ukatili unatokomezwa, ikiwa sambamba kabisa na sheria ya mtoto ya mwaka 2009 na marejeo yake ya mwaka 2019, ambapo kifungu cha 13 kinakataza mtu yeyote kumtesa mtoto au kumfanyia adhabu nyingine ya kikatili, isiyo ya kibinadamu  au inayodhalilisha utu wake.

Moja ya njia madhubuti ambayo serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania pamoja na wadau wameamua kuitumia ili kupunguza ukatili kwa watoto ni kuanzisha vituo vya kulelea watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu, vituo hivi vinaendeshwa kwa uangalizi wa serikali na misaada ya wadau binafsi na wafadhili.

Nchini Tanzania kuna takribani mashirika 8,959 yasiyo ya kiserikali yaliyosajiliwa, yanayohudumu katika sekta mbalimbali za maendeleo ya jamii kama afya, elimu, haki za binadamu na ustawi wa watoto.

Mashirika yaliyojikita kufanya kazi katika masuala ya maendeleo na ustawi wa mtoto nchini Tanzania hadi kufikia mwaka 2025 ni takriban mashirika 142.

Katika mkoa wa Manyara kuna takribani vituo saba (7) vinavyolea watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu, moja kati ya vituo hivyo ni kituo cha Hossana Home Care Foundation kilichopo mtaa wa Nyawari, kata ya Singe wilayani Babati mkoani Manyara.


Nimepata fursa ya kutembelea kituo hicho ili kujionea maendeleo ya watoto wanaolelewa katuoni hapo, na kwa hakika nimekutana na watoto wenye nyuso nzuri za matumaini zilizojawa na tabasamu zinazoashiria kwamba wapo sehemu salama.

Nakutana na binti shupavu, mwenye kujiamini aliyebeba hadithi ya kusisimua kwa mapambano magumu aliyopitia yaliyomfanya kukataa tamaa hadi pale tumaini jipya lilipoingia baada ya kupata nafasi ya kulelewa katika kituo hicho.

Binti huyu anatambulika kwa jina la Doreen Dastan mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule ya sekondari Ft Sumaye, Doreen anasimulia hadithi ya kusisimua ya maisha yake iliyomfanya apitie changamoto ya ukatili wa kisaikolojia kutoka kwa baba yake mzazi, kwani suala la ugomvi baina ya Baba na Mama ilikuwa ni maisha ya kawaida sana kwao, achilia mbali maisha duni ya familia.

Doreen anasema aliishi maisha ya kufokewa, kutukanwa na hadi kupelekea kuwa na msongo mkubwa wa mawazo akitafakari ni lini ataipata amani kwani alikosa tumaini kabisa na hali ikawa mbaya zaidi baada ya wazazi kutengana, mama yake aliamua kuhama kutoka Morogoro na kuhamia mjini Babati baada ya kushindwa kuvumilia maisha ya manyanyaso na vipigo kwake na kwa watoto wake.


"Baba yangu hakuwa mlevi bali alikuwa mtu mkorofi sana, licha ya ugumu wa maisha tuliokuwa nao lakini ugomvi usiokwisha nyumbani ilikuwa ni changamoto nyingine kubwa kwangu, nilitamani maisha ya amani na utulivu na hata uamuzi wa mama kuhama kutoka Morogoro kuja Babati uliongeza changamoto nyingine, kwani changamoto za magonjwa kwa mama zilikuwa nyingi na hatukuwa na pesa, na iliniongezea mawazo zaidi kwakuwa nilikosa tumaini la kusonga mbele". Ameeleza Doreen.

Licha ya changamoto hizo, ndoto ya kupata elimu kwa Doreen haikufa kwani aliendelea kujitahidi kwenda shule huku Mama yake akifanya jitihada za kutafuta msaada huku na kule kwa kushirikiana na ndugu na ndipo tumaini jipya likatokea baada ya kupata nafasi ya kulelewa katika kituo cha kulelea watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu cha Hossana Home Care Foundation.

Doreen anasema ilikuwa furaha kubwa sana kwake kwenda kuanza maisha mengine ya utulivu na amani akiamini kutimiza ndoto zake za kuwa Mwandishi bora wa habari hapa nchini, na kwa sasa anakiri kupata utulivu wa akili kwani anaishi vizuri na anapata mahitaji ya msingi kama mtoto na hatamani kabisa kurudi kwa baba yake kwa kuhofia aliyoyapitia.

"Mama yangu ni fundi cherehani lakini kipato chake kilikuwa kidogo sana hata kodi ya nyumba alishindwa kulipa, ndipo kwa kushirikiana na Mama yangu mkubwa wakaamua kunitafutia msaada ili nimpunguzie mzigo wa mahitaji ya shule na ndipo nikapata nafasi kwenye kituo hichi ambacho kwakweli nimefurahi sana kwani ninaishi vizuri na nina amani hata msongo wa mawazo umeisha, naamini kwa hapa nilipo nitatimiza ndoto zangu za kuwa Mwandishi bora wa habari". Ameongeza Doreen.

Kwa sasa Doreen anafurahi kukutana na marafiki wapya katika kituo hicho akiwemo rafiki yake kipenzi Mwanaisha Juma ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili katika shule ya sekondari Balang'dalalu, na kwa pamoja wanapambania ndoto zao, japo hadithi ya Mwanaisha iligubikwa zaidi na changamoto ya kiuchumi kwa familia yake kiasi cha kupata mlo mmoja tu kwa siku na jitihada zake binafsi zikamfanya kupata fursa hii baada ya kueleza changamoto yake kwa Mwalimu mkuu na kumuombea nafasi ya kulelewa kituoni hapo, kwa pamoja wanaamini kufanikiwa kwani wanafundishwa maadili mema na namna ya kukabiliana na changamoto.


"Mimi nilikuwa napata mlo mmoja tu kwa siku, hata shuleni nilikuwa sili kwakuwa wazazi walishindwa kulipia chakula, ndipo nikaamua kuzungumza na mwalimu mkuu ili aweze kunisaidia, na ninamshukuru sana kwani alinisaidia kuniombea nafasi kwenye kituo hichi cha Hossana na kwasasa naishi hapa nimepata marafiki kama Doreen na tunaamini tutatimiza ndoto zetu". Ameeleza Mwanaisha Juma rafiki yake Doreen Dastan

Kwenye vituo hivi vya kulelea watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu wapo wasimamizi wanaoishi na watoto na kuwahudumia mahitaji yao ya msingi ya kilasiku, ndivyo ilivyo pia katika kituo cha Hossana yupo mwanadada anayetambulika kwa jina la Annagress Justin anayefanya kazi ya kuwahudumia na kuwafundisha mambo mbalimbali ya kimaadili.

Annagress anasema ameanza kazi katika kituo hicho tangu mwaka 2021 na amewapokea watoto wengi ambao baada ya kufika katika kituo hicho walionesha mabadiliko makubwa ikiwemo kuwa na afya njema na furaha, kwani watoto wengi walikuwa wamedhoofu na wanamsongo mkubwa wa mawazo kutokana na yale waliyopitia huko nyumbani.

Ukiachilia mbali chakula na malazi Annagress anasema wanafundisha maadili na kumjua Mungu kupitia dini zao ili wafuate yale ambayo mwenyezi Mungu anaamuru kupitia vitabu vyake vitakatifu na zaidi kabisa ni kuhusu stadi za maisha kwani wanafanya kazi mbalimbali za mikono ikiwemo kupika, kuosha vyombo, kutunza bustani na kulima, yote haya ni kwa lengo la kuwajengea uimara wa kimwili na kiakili na kuujua uhalisia wa maisha na nafasi zao katika jamii na wanashirikiana vyema na maafisa ustawi ikiwemo kuwaletea miradi ya kuku na mbuzi.


"Watoto wengi wanaokuja hapa changamoto zao kubwa huko nyumbani ni wazazi kuwa walevi, akija nyumbani hamjali tena kama mtoto, ni kumchapa na adhabu nyingine zisizostahili, sisi kwanza sheria yetu ni kilasiku lazima tuungane pamoja na tusali, lakini pia siku za ijumaa kwa waislamu wanaenda msikitini na wakristo jumapili kanisani na pia tunawafundisha shughuli za mikono na tunamiradi ya kuku na mbuzi". Amesema Annagress mlezi wa watoto.

Annagress anasema wapo watoto wengi wenye uhitaji lakini wao kwa kushirikiana na maafisa ustawi wa jamii wanawasidia kufuatilia kwenye maeneo yao ili kugundua kama kuna watoto wenye changamoto na wanaandika barua ya kuomba nafasi ya malezi.

"sisi tunaletewa na maafisa ustawi wa jamii, afisa ustawi baada ya kujua changamoto ndiyo anamleta hapa na atapiga simu kuomba na tunashirikiana nao vizuri".Ameongeza Annagress mlezi wa watoto kituoni hapo.

Matokeo ya utafiti wa kitaifa wa ukatili dhidi ya watoto Tanzania (VACS) umeonesha kupungua kwa ukatili wa kisaikolojia, kwa wasichana umepungua kutoka 25% mwaka 2009 hadi kufikia 22% mwaka 2024 na kwa wavulana umepungua kutoka 31% mwaka 2009 hadi kufikia 16% mwaka 2024.

Takwimu hizi zinasadifiwa na maelezo ya afisa ustawi wa jamii wa Halmashauri ya mji wa Babati Agatha Patrice, ambaye amekiri kuwa uwepo wa vituo vya kulelea watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu umesaidia kupunguza ukatili kwa watoto.

"Tunaona wazi kuwa vituo vimetusaidia kutulelea watoto na vimesaidia kwa kiasi kikubwa sana kupunguza vitendo vya ukatili kwa watoto, kwani watoto wengi wanatoka kwenye familia zenye migogoro ya muda mrefu inayopelekea hata wazazi kuachana na kuwafanya watoto waishi katika mazingira magumu ya msongo wa mawazo kwasababu hakuna amani na utulivu nyumbani". Ameeleza Agatha Patrice afisa ustawi wa jamii halmashauri ya mji wa Babati.

Afisa ustawi Agatha Patrice ameongeza kuwa kwa sasa wanaendelea na jitihada za kubaini watoto wenye changamoto za ukatili kwenye jamii kwa kutumia utaratibu wa kupata taarifa mbalimbali kutoka kwenye mitaa na kata na kupitia kwa watu wanaoona familia zenye changamoto na watoto wanaothirika kama mabalozi na wenyeviti wa mitaa, na mara nyingi huwa wanafika ofisini na baada ya hapo wanaanza kufatilia na wakibaini huandika barua kwenye vituo kuomba nafasi.

"Utaratibu ambao tunautumia ni kupata taarifa mbalimbali kutoka kwenye kata na mitaa kupitia kwa watu wanaoona kabisa kwamba familia fulani watoto wanaathirika au kwa mabalozi na wenyeviti wa mitaa, kwahiyo tunavyopata hizo taarifa kama halmashauri tunachukua hatua ya kufika kwenye eneo husika tutawakuta hao watoto, tutaongea na majirani, tutamtafuta mzazi na tukijiridhisha tunaandika barua ya maombi kwenye hizi taasisi za kulelea watoto na tunawapeleka". Ameongeza Agatha Patrice afisa ustawi wa jamii halmashauri ya mji wa Babati.

Ushirikiano mzuri baina ya maafisa ustawi wa jamii na vituo vya kulele watoto yatima na wanaoishi kwenye mazingira magumu kwa kiasi kikubwa unaonekana kusaidia ustawi wa watoto kwenye jamii kwani mazingira bora, amani na utulivu ni nyenzo kubwa sana za kumupeusha mtoto na ukatili.

Kwa mujibu wa mtaalamu wa Saikolojia na Mhadhiri kutoka chuo kikuu cha Iringa kitivo cha Saikolojia Robert Lwiza anasema maendeleo ya mtoto huletwa na amani na utulivu, ambavyo vinamsaidia mtoto kujenga akili yenye afya, hisia zilizo imara, kujiamini na uwezo mzuri wa kujifunza na kuhusiana na wengine.

"Amani na utulivu humsaidia mtoto kujenga akili yenye afya, kujiamini, hisia zilizo imara na uwezo wa kuhusiana na wengine na kujifunza na hata uwezo kuzikabili changamoto na ndio maana huwa tunasisitiza sana umuhimu wa mazingira salama, yenye upendo na yasiyo na migogoro mikubwa katika malezi ya mtoto ili aepukane na ukatili wa kisaikolojia".Amesema Mwanasaikojia Robert Lwiza.

Mafanikio haya ya kupunguza ukatili kwa watoto yanakwenda sambamba na juhudi za wizara ya maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalumu, inayoongozwa na mwanamama shupavu Dkt Dorothy Gwajima ambayo inasamimia sheria, sera na miongozo mbalimbali inayohusu ustawi wa watoto hapa nchini Tanzania.

Na mara kadhaa kupitia majukwaa mbalimbali ametoa wito kwa jamii kuacha ukatili kwa watoto  na kutoa wito kwa wazazi na walezi kuwafundisha watoto bila kuwaletea madhara.


"Wapendwa walezi na walimu wa watoto wetu mashuleni, pamoja na kazi nzuri mnayofanya hima zingatieni kulea watoto pasipo kuwaletea madhara ya adhabu zilizo nje ya mwongozo, vinginevyo mtaendelea kuhatarisha ustawi wa watoto". Alisema Dkt Dorothy Gwajima waziri wa maendeleo ya jamii, jinsia, wanawake na makundi maalumu.

Kwasasa Doreen Dastan anamatumaini makubwa ya kutimiza ndoto zake za kuwa mwandishi bora wa habari ili aisaidie jamii kupaza sauti juu ya mambo ya ukatili na kuhakikisha jamii inakuwa sehemu salama na anaiomba serikali na wadau binafsi waendelee kuwashika mkono ili waendelee kusonga mbele.


Ama hakika mwanzo wa ngoma ni lele na hakuna marefu yasiyo na ncha na kufikia hapa ndio tamati ya makala hii, iliyoangazia ni kwa namna gani vituo vya kulele watoto yatima na wanaotoka kwenye mazingira magumu vinavyosaidia kupunguza ukatili kwa watoto, bila shaka umejifunza mengi, hadi wakati mwingine jina langu ni Linda Moseka.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

WIMBI LA WANAFUNZI, MBIO ZA MADARASA: TANZANIA INAVYOJIANDAA KWA ELIMU YA LAZIMA YA MIAKA 10

Jamii, serikali na wadau wa elimu wanavyoshirikiana kukabiliana na ongezeko la wanafunzi litakalotokana na wanafunzi wa darasa la sita na la saba kuingia kidato cha kwanza kwa pamoja mwaka 2028

Na John Walter – Manyara

"Wananchi wa Kata ya Magugu wakishiriki ujenzi wa madarasa ili kujiandaa na ongezeko la wanafunzi litakalotokana na utekelezaji wa sera mpya ya elimu."

Tanzania ipo katika kipindi muhimu cha mageuzi ya elimu yanayolenga kuhakikisha kila mtoto anapata fursa ya kujifunza kwa muda mrefu zaidi na kupata maarifa yanayomwandaa kukabiliana na mahitaji ya dunia ya sasa.

Kupitia Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, Toleo la 2023, serikali imefanya maboresho makubwa ya mfumo wa elimu kwa kuongeza elimu ya lazima kutoka miaka saba hadi miaka 10. Maboresho hayo yanalenga kuhakikisha watoto wengi zaidi wanapata elimu ya sekondari, kuimarisha usawa katika elimu na kuwajengea wanafunzi maarifa, ujuzi na stadi za maisha zitakazowawezesha kujitegemea.

Tofauti na mfumo wa zamani ambao ulitambua darasa la saba kama mwisho wa elimu ya lazima, mfumo mpya unapanua wigo huo hadi ngazi ya sekondari. Aidha, maboresho hayo yanaweka mkazo katika elimu ya ujuzi, ubunifu, ujasiriamali na matumizi ya maarifa katika kutatua changamoto za maisha badala ya kutegemea elimu ya taaluma pekee.

Hata hivyo, pamoja na matarajio makubwa ya sera hiyo, utekelezaji wake umeibua changamoto mpya inayohitaji maandalizi ya haraka ya miundombinu ya elimu.

Mwaka 2028, Tanzania itashuhudia hali ya kipekee ambapo wanafunzi wa darasa la sita wanaohitimu kupitia mfumo mpya na wanafunzi wa darasa la saba wanaomaliza mfumo wa zamani wataingia kidato cha kwanza kwa wakati mmoja. Hali hiyo inayojulikana kama “double cohort” inatarajiwa kuongeza kwa kiasi kikubwa idadi ya wanafunzi watakaojiunga na shule za sekondari nchini.

Ongezeko hilo lina maana moja kubwa; hitaji la madarasa zaidi, walimu zaidi, vitabu zaidi na mazingira bora zaidi ya kujifunzia.

Bila maandalizi ya kutosha, shule nyingi zinaweza kukabiliwa na mrundikano wa wanafunzi madarasani, hali inayoweza kuathiri ubora wa elimu na ufanisi wa ufundishaji.

Katika maeneo mbalimbali nchini, maandalizi tayari yameanza. Miongoni mwa maeneo yanayoonesha mfano wa namna jamii inavyoweza kushiriki katika utekelezaji wa sera mpya ni Kata ya Magugu, Wilaya ya Babati mkoani Manyara.

Katika kata hiyo, mjadala wa elimu umehamia kwenye jambo moja kubwa; madarasa.

Si kwa sababu shule zimefungwa. Si kwa sababu wanafunzi wamepungua. Bali kwa sababu mwaka 2028 unakuja na changamoto ambayo haijawahi kushuhudiwa katika historia ya hivi karibuni ya elimu nchini.

Kwa mwanafunzi wa shule ya msingi, Shamila Juma, utekelezaji wa sera mpya una maana moja kuu; watoto wengi zaidi watapata nafasi ya kuendelea na elimu ya sekondari.

"Elimu ya sekondari ni muhimu kwa sababu inamfanya mtu aweze kujitambua na kujitegemea," anasema.

Mawazo hayo yanaungwa mkono na mwenzake John Bayyo ambaye anaamini elimu ya sekondari ndiyo daraja la kuwapa vijana stadi za maisha na kuwaandaa kwa maisha ya baadaye.

Lakini wakati wanafunzi wakiona fursa, viongozi wa elimu wanaona changamoto kubwa inayohitaji maandalizi ya haraka.

Katika Shule ya Sekondari Magugu Day yenye wanafunzi zaidi ya 1,000, tayari dalili za changamoto hiyo zinaonekana.


Mkuu wa shule hiyo, Revokati Kimario, anasema shule hiyo kwa sasa ina upungufu wa madarasa saba.

Anabainisha kuwa mwaka 2026 shule ilipokea wanafunzi 338 wa kidato cha kwanza. Hata hivyo, makadirio yanaonesha kuwa mwaka 2028 shule hiyo inaweza kupokea wanafunzi zaidi ya 600.

Hii ni ongezeko la zaidi ya asilimia 77 ndani ya kipindi cha miaka miwili.

Kwa lugha rahisi, kama maandalizi hayatafanyika mapema, wanafunzi wengi zaidi wataingia katika madarasa yale yale yaliyopo sasa.

Matokeo yake yanaweza kuwa mrundikano wa wanafunzi, kupungua kwa ufanisi wa ufundishaji, changamoto za usimamizi wa masomo na mazingira magumu ya kujifunzia.

Tatizo hilo si la Magugu pekee.


Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Mji wa Babati, Paskalina Lowekelo, anasema halmashauri hiyo ina upungufu wa madarasa 60.

Kwa mujibu wake, changamoto hiyo imekuwa sehemu ya mjadala katika vikao vya wadau wa elimu vinavyoangalia namna ya kujiandaa na ongezeko la wanafunzi linalotarajiwa.

"Baadhi ya madarasa yatakayobaki wazi katika shule za msingi yanaweza kutumika kwa muda. Pia tumekuwa tukijadili namna ya kutumia uwezo uliopo katika baadhi ya shule za sekondari binafsi zenye wanafunzi wachache ili kupunguza shinikizo la wanafunzi watakaoingia kidato cha kwanza," anasema.

Kauli hiyo inaonesha kuwa changamoto ya mwaka 2028 haiwezi kutatuliwa na taasisi moja pekee, bali inahitaji ushirikiano wa serikali, sekta binafsi na jamii.

Lakini kinachoifanya Magugu kuwa mfano wa kipekee si ukubwa wa changamoto, bali namna wananchi walivyoamua kuikabili.

Afisa Mtendaji wa Kata ya Magugu, Mary Simba, anasema kata hiyo inatarajiwa kuwa na upungufu wa vyumba 25 vya madarasa ifikapo mwaka 2028.

Kata hiyo inayojumuisha shule za sekondari za Magugu, Matufa, Gichameda na Sarame ndiyo kata kubwa zaidi katika Wilaya ya Babati.

Badala ya kusubiri kila kitu kifanywe na serikali, wananchi waliamua kuchukua hatua.

Kupitia mikutano ya vijiji iliyoandaliwa na Kamati ya Maendeleo ya Kata, wakazi walikubaliana kuchangia shilingi 10,000 kwa kila kaya ili kusaidia ujenzi wa madarasa.

Uamuzi huo unaweza kuonekana mdogo kwa mtu wa nje, lakini ndani yake umebeba ujumbe mkubwa; jamii imeanza kuiona sera ya elimu kama jukumu lake pia.

Diwani wa Kata ya Magugu na Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Kata, Stanley Charles, anasema michango hiyo ilianza Mei 15 na itaendelea hadi Julai 2026 huku ujenzi ukitarajiwa kuanza mwezi Agosti.

Anasema viongozi wa kata wameamua kuanza maandalizi mapema ili ifikapo mwaka 2028 changamoto ya madarasa isiwe kubwa kama inavyohofiwa sasa.

Kwa zaidi ya kaya 5,102 zilizopo Magugu, mchango huo unaweza kuzalisha nguvu kubwa ya kifedha kwa ajili ya maandalizi ya mwaka 2028.

Kwa sasa baadhi ya wazazi tayari wanashiriki katika ujenzi hadi kufikia hatua ya upauzi wa majengo ambapo boma moja linagharimu takribani shilingi milioni 12.5.

Kasimu Bakari ni miongoni mwa wananchi waliounga mkono mpango huo.

Kwake, elimu si jukumu la serikali pekee.

"Hakuna ombi hapa. Lazima tujenge kwa ajili ya watoto wetu. Watoto ni wetu," anasema.

Naye Mwanahamisi Hussein anaunga mkono jitihada hizo lakini anashauri kuwe na uratibu mzuri wa michango ya maendeleo.

"Tuko tayari kuchanga, lakini michango mingine ipunguzwe ili wananchi wabaki na nguvu ya kushiriki katika ujenzi wa madarasa," anasema.

Maoni hayo yanaonesha kuwa wananchi wako tayari kushiriki katika utekelezaji wa sera mpya mradi washirikishwe na waone matokeo ya michango yao.

Katika ngazi ya taifa, serikali imeendelea kusisitiza kuwa utekelezaji wa sera hiyo unaenda sambamba na maandalizi ya miundombinu na rasilimali watu.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, amesema mwaka 2027/2028 wanafunzi wa darasa la sita na darasa la saba wataingia sekondari kwa pamoja kutokana na mabadiliko ya mfumo wa elimu.

Amesisitiza kuwa maandalizi ya mapema ni muhimu ili kukabiliana na changamoto za madarasa, walimu na miundombinu mingine inayohitajika katika utekelezaji wa sera hiyo.

Katika kuimarisha utekelezaji wa mtaala mpya, serikali pia inatarajia kuajiri walimu 4,000 wa masomo ya biashara ili kuwajengea wanafunzi maarifa ya ujasiriamali na kuwawezesha kujitegemea baada ya masomo yao.

Hatua hiyo inaendana na lengo kuu la maboresho ya elimu; kuhamisha msisitizo kutoka elimu ya taaluma pekee kwenda elimu inayojenga ujuzi, ubunifu na uwezo wa kujiajiri.

Katika Shule ya Sekondari Kiru, maandalizi ya utekelezaji wa sera mpya tayari yanaonekana.


Mkuu wa shule hiyo, Isaack Makena, anasema serikali imejenga madarasa matano ya ziada, imetoa vitabu 1,100 vya mtaala mpya ulioboreshwa na kuongeza walimu watano.

Kwa mtazamo wake, mtaala mpya utawasaidia wanafunzi kujifunza kwa vitendo zaidi na kuwawezesha kujiandaa vyema kwa maisha ya baadae.

Mtazamo huo unaungwa mkono na mchambuzi wa masuala ya elimu, Lucas Alphonce, ambaye anaamini Tanzania imefika wakati wa kufanya mageuzi hayo ili kuendana na nchi nyingine zilizotangulia katika mfumo huo.

Anasema maboresho hayo yanaweza kusaidia kuandaa vijana wenye uwezo mkubwa wa kujitegemea na kushiriki katika maendeleo ya uchumi wa taifa.

Kwa upande wake, Mkuu wa Taasisi ya Mafunzo ya Sayansi za Afya Haydom, Bathomolayo Madangi, anasema mtaala mpya unapaswa kuendelea kuzingatia stadi za maisha, ujasiriamali na uwezo wa wanafunzi kujiajiri.

Anaamini mafanikio ya sera mpya hayatapimwa kwa idadi ya wanafunzi wanaohitimu pekee, bali kwa uwezo wao wa kutumia maarifa waliyojifunza kutatua changamoto za maisha.

Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2023 imekusudia kuhakikisha kila mtoto anapata fursa ya elimu kwa usawa na kwa muda mrefu zaidi.

Lakini sera yoyote, hata ikiwa nzuri kiasi gani, haiwezi kufanikiwa bila ushiriki wa jamii.

Mfano wa Magugu unaonesha kuwa mafanikio ya sera hayawezi kutegemea serikali pekee. Yanahitaji ushiriki wa wazazi, viongozi wa jamii, sekta binafsi na wadau wa maendeleo.

Wakati wengine wakisubiri kuona nini kitatokea mwaka 2028, wananchi wa Magugu tayari wanachanga fedha, wanajenga madarasa na wanashiriki katika kupanga mustakabali wa watoto wao.

Pengine mafanikio makubwa ya sera hii hayatakuwa idadi ya madarasa yatakayojengwa au walimu watakaoajiriwa.

Mafanikio yake yatakuwa pale ambapo wananchi wataacha kuiona elimu kama jukumu la serikali pekee na kuanza kuiona kama uwekezaji wao wenyewe.

Katika Kata ya Magugu, safari hiyo tayari imeanza kwa shilingi elfu kumi tu kutoka kila kaya, lakini thamani yake inaweza kuwa kubwa zaidi kuliko fedha hizo; ni uwekezaji katika kizazi kijacho cha Tanzania.

 

Semina yafichua ukatili wa kingono unaowakabili wafanyakazi wa nyumbani"


Wafanyakazi wa nyumbani wameibua   wanaokumbana nao wanapotekeleza majukumu yao katika nyumba wanazofanyia kazi, wakisema vitendo hivyo vinahatarisha usalama wao, vinadhalilisha utu wao na kuathiri afya zao ya kimwili na kisaikolojia.

Changamoto hiyo imeelezwa wakati wa semina ya kuwajengea uwezo wafanyakazi wa majumbani kuhusu haki zao,katika Mradi unaotekelezwa na Chama Cha Wafanyakazi ‘CWM’Jimboni Morogoro ’’Wape wafanyakazi wa majumbani fursa ya kupata mafunzo ya kuwaongezea ujuzi” ambapo washiriki wametaka hatua madhubuti kuchukuliwa ili kuwalinda dhidi ya vitendo vya unyanyasaji vinavyofanyika katika mazingira ya kazi.

Veronica Jonas mfanyakazi wa nyumbani amesema alianza kufanya kazi za nyumbani tangu mwaka 2020 akiwa mkoani Kigoma,amesema kazi za nyumbani zina changamoto nyingi anakabiliana nazo kuhakikisha malengo yake yanatimia na faida pia ni nyingi kwa sababu kazi hiyo inampatia kipato kukidhi mahitaji yake.

Aidha amesema kuwa miongoni mwa changamoto alizowahi kukutana nazo kupitia kazi yake  ni baba mwenye nyumba kumtaka kimapenzi, hali iliyomlazimu kuacha kazi kwa ajili ya kulinda usalama wake na kuepusha fedheha kwa mama mwenye nyumba na jamii kwa ujumla.

Hata hivyo amesema kuwa licha ya uzoefu wake kazini hakuwahi kujua namna ya kupigania haki zake inapotokea hali ya kudhulumiwa, kwa hiyo kupitia mafunzo hayo amejifunza kwamba wafanyakazi wa nyumbani wana haki kama wafanyakazi wengine pamoja na kuzijua sheria zinazowalinda ikiwemo suala la mkataba wa ajira.

’’Kiukweli kwenye suala la haki nilikuwa sijui lolote, kwa mfano changamoto yangu ya kutakwa kimapenzi na baba mwenye nyumba,sikudai chochote zaidi ya kutumia mbinu mbadala ya kukimbia na kutoroka lakini nimetambua kuwa tuna sheria zinazotulinda, nami nitaelimisha wenzangu wanaofanya kazi hizi’’ amesema Veronica.

Hata hivyo ameshauri waajiri wapewe elimu zaidi kupata uelewa ili kuondoa dhana ya kuajiri wafanyakazi wa nyumbani kwa mazoea wakiamini kwamba mfanyakazi wa ndani anachohitaji ni pesa tu na kusahau kwamba utu ni muhimu kuliko pesa yenyewe,akishauri serikali isaini mkataba kwa sababu wafanyakazi hao wameteseka kwa muda mrefu.

’’Niwaombe waajiri wetu watimize wajibu wao kwetu, kama wao wanavyopigania kuoanda vyeo na mshahara mzuri kazini kadhalika nasi pia tunaomba watuthamini, wanapoenda kazini wanatuacha nyumbani tukifanya kazi zao, kama wanavyochukia rushwa ya ngono kazini nasi pia tunachukia hivyo hivyo,walitambue hilo nasi tuna haki zetu’’amefafanua Veronica

Naye Witnes Joseph alianza kufanya kazi za nyumbani tangu mwaka 2020 baada yaya wazazi wake kuachana na familia kuachwa kwa bibi, ilimlazimu kufanya kazi hizo ili kupata fedha ya kumsaidia mdogo wake kuendelea na  masomo ambaye kwa sasa yuko kidato cha tatu

Ameeleza kuwa yeye mwenyewe ameishia darasa la saba alitamani aendelee kusoma lakini hakufanikiwa baada ya kukosa mtu wa kumsaidia, kwa hiyo ataendelea kufanya kazi za nyumbani mpaka pale mdogo wake atakapotimiza ndoto zake za elimu.

Licha ya kulipwa mshahara mdogo Witnes amebeba mzigo mkubwa wa majukumu, mbali na kumsaidia mdogo wake lakini pia anamsaidia mjomba wake ambaye kwa sasa yuko chuo kikuu, furaha yake ni kuona ndoto za watu hao zinatimia.

’’Mjomba wangu anakaribia kumaliza chuo mwaka huu, mara nyingi akiwa na shida ananitafuta namsaidia,mtoto wa bibi yangu na mtoto wa dada yangu naye yuko chuo akiwa na shida ananitafuta kama ninacho nawapa’’

Ndoto ya Witnes ilianza kuzima ghafla pale ilipoanza kujitokeza changamoto ya kutakwa kimapenzi na watoto wa mwajiri wake,ikamlazimu kuacha kazi na kuja Mkoani Morogoro kutafuta kazi ambapo kwa sasa anaishi kwa amani na upendo kama mtoto wa familia.

Ameongeza kuwa fursa ya mafunzo iliyoandaliwa na CWM kushirikiana na Chuo cha Veta Mikumi masomo hayo yatamsaidia kuongeza ujuzi,kumwendeleza mdogo wake elimu ya juu, naye akiwa ni miongoni mwa kundi la kwanza linalotarajia kuanza rasmi mafunzo ya ufundi juni 15 mwaka huu.

DC CHATO :AFDP NI MKOMBOZI WA UCHUMI WA WANANCHI





Na; Mwandishi wetu – Chato


Mkuu wa Wilaya ya Chato Mhe. Louis Peter Bura Amepongeza Programu ya kuendeeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) inayoratibiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge Uratibu na Wenye Ulemavu kwa Uratibu wa Kituo cha kuendeleza ukuzaji Viumbemaji Rubambagwe Kilichopo wilayani Chato Mkoani Geita kinachosimamiwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Ametoa Pongezi hizo Tarehe 10 Juni 2026 Wilayani Chato alipofanya ziara maalum ya kutembelea kituo hicho akiwa pamoja na timu ya wataalam waliokutana katika Wilaya hiyo wakiwa katika kazi maalum ya kufanya mapitio ya mpangokazi wa Program hiyo.





Mkuu wa Wilaya Bura, alisema kuwa Wilaya yake inawajibu wa kutoa elimu kwa wafugaji kupitia kituo cha Rubambagwe hivyo amewaasa wataalam kutoka katika sekta zinazotekeleza mradi kufanya kazi kwa ushirikianao na Wilaya hiyo, ili kuweza kuleta matokeo chanya katika uchumi wa Wilaya na Taifa kwa Ujumla na Kuongeza mnyororo wa thamani.





“Tutakuwa tunazalisha vifaranga vya samaki pale, haitatosha hiyo pia tutakuwa tunazalisha vyakula vya samaki, na hayo yote yamenipa mimi wakati mzuri na sababu ya kujifunza haya yote, na tunashukuru mradi huu kwenda kwa kasi na ni wakati sasa wa kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja . “Alibanisha



Sambamba na hilo Mkuu huyo wa Wilaya alisisitiza ushirikishwaji mzuri baina ya sekta zinazotekeleza Programu hiyo nchini pamoja na Wilaya husika.’katika dhana nzima ya ushirikishwaji kuna mambo mengi ambayo Wilaya inaweza kuyasimamia na kuyatekeleza kwa ukaribu zaidi, hapa Chato wananchi wanajihusisha Zaidi na uuzaji wa samaki tuna soko kubwa la samaki hapa linaitwa Chato beach, wananchi wanapata chakula na pia wanauza sehemu nyingine nje ya Chato.’ Alifafanua.





Kwa upande wake Mratibu wa Programu Hiyo kutoka Ofisi ya waziri Mkuu Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Bw. Salimu Mwinjaka alisema pamoja na mambo Mengine kwa upande wa bahari kuu, Progamu hiyo inakusudia kujenga viwanda vya samaki Tanzania Zanzibar katika eneo la Fungurefu na Wilayani Kilwa Mkoani Lindi na kuweza kukabili hali ya upotevu wa mazao ya samaki baada ya kuvuna kwa kujenga vyumba vya ubaridi vya kuhifadhi mazao ya uvuvi, mitambo wa kuzalisha barafu, vichanja na mahema yakukaushia dagaa au samaki kwa kutumia mionzi ya jua.




Akiongelea kuhusu ufugaji samaki, Bw. Mwinjaka alisema kupitia progamu hiyo kuna vituo vinne ambavyo vipo chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi ambavyo ni Pamoja na vituo vya kuendeleza ukuzaji viumbemaji cha Rubambagwe kilichopo Wilayani Chato, Mwamapuli Wilayani Igunga, Kingolwira Wilayani Morogoro na kituo cha Ruhila Wilayani Songea.





Akiongea katika ziara hiyo, Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bi Mkomanile Mahundi alisema kituo cha Kuendeleza Ukuzaji Viumbemaji Rubambagwe kitakuwa na kazi ya kuzalisha na kusambaza vifaranga bora vya samaki aina ya sato na kambale, pamoja na kutoa mafunzo kwa wakuzaji viumbemaji katika maeneo ya mikoa ya Geita, Mwanza, Kagera, Shinyanga, Simiyu na Mara.





Aliongeza kusema pia, baada ya kituo kukamilika kitakuwa na uwezo wa kuchakata chakula cha samaki ambapo itapelekea wigo wa kuongeza ajira kwa wanawake, vijana na watu wenye mahitaji maalum.

“Wizara ya Mifugo na uvuvi kupitia Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP) itawezesha uwepo wa dirisha maalum katika taasisi za kifedha kama vile Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) kwa kuwawezesha wakuzaji viumbemaji kupata mkopo yenye riba nafuu ya pembejeo na zana za ukuzaji viumbemaji.” Alisem



Ujenzi wa Kituo hicho cha Rubambagwe umefikia Asilimia 85 mpaka sasa ambapo umehusisha Jengo la utawala, karakana, nyumba za wafanyakazi jengo la kitotoleshi cha samaki, ujenzi wa mabwawa ya kufugia samaki, chanzo cha maji yaani tenki maalum la kutunza maji, kuchuja na kusafirisha maji hayo kwenda kwenye mabwawa ya kufugia samaki, kitotoleshi pamoja na maeneo mengine yanayotumia maji kituoni hapo.

DAWASA, JIJI, TARURA WAZIBUA MITARO YA MAJI TAKA INAYOZUNGUKA SOKO LA KARIAKOO.


Shirika la Masoko ya Kariakoo kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Dar es Salaam (DAWASA), Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) na Halmashauri ya Jiji ya Dar es Salaam wameshirikiana kuzibua mitaro ya maji taka inayozunguka Soko Kuu la Kariakoo.

Akizungumza baada ya zoezi la uzibuaji wa mitaro hiyo, Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo, CPA. Ashraph Abdulkarim amesema zoezi hilo linafanyika kufuatia maelekezo aliyoyatoa Mkuu wa Wilaya ya Ilala Mhe. Edward Mpogolo kuwa taasisi hizo zikutane na kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo na kuondoa kero kwa wananchi.

CPA. Abdukarim amemshukuru na kumpongeza Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam, Elihuruma Mabelya na wakuu wa taasisi hizo kwa namna waliyoshughulikia changamoto hiyo na kutuma wataalam wao kufika katika maeneo hayo, kitendo ambacho kwa pamoja kimefanikisha kutekelezeka kwa maagizo ya Mhe. Mkuu wa Wilaya.

Amesema shirika litaendelea kushirikiana na mamlaka hizo kuhakikisha kuwa maeneo yanayolizunguka soko yanakuwa safi muda wote japo ambalo litachangia kuzuia kutokea kwa magonjwa ya mlipuko na pia wafanyabiashara kufanya biashara katika mazingira safi na ya kuvutia.

Soko Kuu la Kariakoo limejipambanua kwa usafi ambapo limeweka wafanya usafi katika maeneo ya kutolea huduma kitu kilichofanya soko hilo liwe safi na nadhifu muda wote huku likiwa na idadi kubwa ya wafanyabiashara pamoja na wateja wanaoingia kila siku.

Wednesday, June 10, 2026

DKT. MAULID: UONGOZI WA KIMKAKATI NI MSINGI WA MAFANIKIO YA SEKTA YA ELIMU


Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt Maulid J. Maulid leo umefungua Mafunzo ya Uongozi wa Kimkakati (Strategic Leadership) kwa viongozi wa shule za sekondari wa Manispaa ya Shinyanga, yakiwakutanisha washiriki 44 wakiwemo Wakuu wa Shule za Sekondari 22 na Makamu Wakuu wa Shule 22. 

Mafunzo haya yanatolewa na ADEM kwa kushirikiana na African Centre for School Leadership (ACSL) kupitia VVOB kwa kufadhiliwa na Mastercard Foundation.

Akifungua mafunzo hayo, Mtendaji Mkuu wa ADEM, Dkt. Maulid J. Maulid, alisisitiza umuhimu wa uongozi wa kimkakati katika kuimarisha utendaji wa taasisi za umma na kufanikisha malengo ya maendeleo ya sekta ya elimu.

“Uongozi wa kimkakati ni nyenzo muhimu katika kuhakikisha taasisi za umma zinafikia malengo yake kwa ufanisi. Viongozi wanapaswa kuwa na uwezo wa kutazama mbele, kupanga kwa weledi na kusimamia rasilimali zilizopo ili kuleta matokeo chanya kwa taasisi wanazoziongoza,” alisema Dkt. Maulid.

Aidha, Dkt. Maulid alieleza kuwa mafunzo hayo yanatekelezwa kwa kutumia mfumo wa kisasa wa ufundishaji unaowapa washiriki fursa ya kujifunza kwa vitendo, kubadilishana uzoefu na kupata maarifa yatakayowawezesha kukabiliana na changamoto za kiuongozi katika mazingira yao ya kazi.

“Mafunzo haya yanaendeshwa kwa mfumo wa kisasa utakaohakikisha kunakuwa na mawasiliano ya mara kwa mara, lengo kuu likiwa ni kutoa nafasi kwa washiriki kutoa mrejesho kwa wazeshaji kuhusiana na maendeleo ya utekelezaji wa mada. Tunatarajia washiriki wote watatumia kikamilifu fursa hii kujifunza na kujijengea uwezo zaidi,” aliongeza.

Katika hatua nyingine, Mtendaji Mkuu huyo alibainisha kuwa washiriki watakaofanya vizuri katika mafunzo hayo watatambuliwa na kutunukiwa vyeti, hatua inayolenga kuongeza motisha na kuhamasisha ushiriki wenye tija katika mchakato mzima wa kujifunza.

Sambamba na hilo, Dkt. Maulid alisisitiza umuhimu wa ufuatiliaji wa utekelezaji wa maarifa na ujuzi unaotolewa katika mafunzo hayo, akieleza kuwa mafanikio ya programu hiyo yatapimwa kupitia mabadiliko chanya yatakayoonekana katika usimamizi na utendaji wa shule husika.

CBE YAHUISHA MITAALA TISA KUENDANA NA TEKNOLOJIA NA MAHITAJI YA SOKO LA AJIRA


Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kipo katika mchakato wa kupitia na kuhuisha mitaala tisa ya masomo ili iendane na mabadiliko ya sayansi na teknolojia, Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 (Toleo la 2023), pamoja na mahitaji ya sasa ya soko la ajira nchini.

Akizungumza Juni 10, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wa wadau uliowakutanisha zaidi ya taasisi 40, Mkuu wa Chuo cha CBE, Prof. Edda Tandi Lwoga, amesema maboresho hayo yanalenga kuhakikisha chuo kinazalisha wahitimu wenye ujuzi unaokidhi mahitaji ya dunia ya sasa na ya baadaye.

Prof. Lwoga amesema hatua hiyo pia inalenga kukiandaa chuo kuwapokea wanafunzi wanaotoka katika mfumo mpya wa elimu ya sekondari unaosisitiza zaidi amali na umahiri, hivyo kuhitaji mitaala inayozingatia maendeleo ya teknolojia na mahitaji ya sekta mbalimbali za uchumi.

Mkutano huo ulihusisha wanataaluma kutoka vyuo mbalimbali, wawakilishi wa Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), wawakilishi wa shule za sekondari pamoja na wadau wa elimu kutoka sekta za umma na binafsi.

Ameeleza kuwa mapitio hayo pia yanazingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050, inayolenga kujenga uchumi shindani unaotegemea maarifa, ubunifu na matumizi ya teknolojia.

Mitaala inayofanyiwa mapitio ni pamoja na Banking and Finance, Accounting and Finance, Accounting and Taxation, Digital Marketing, Business Administration, Finance and Economics, Bachelor Degree in Business Studies, Bookkeeping na Master of Science in IT Project Management.

Katika maboresho hayo, CBE imejumuisha masuala ya Akili Mnemba (AI) katika masomo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), huku masomo ya bima yakiongezwa katika programu za fedha ili kuimarisha uelewa wa wanafunzi kuhusu sekta hiyo inayokuwa kwa kasi.

Uongozi wa chuo umesisitiza kuwa ushirikishwaji wa wadau, hususan waajiri, katika mchakato wa kuandaa mitaala hiyo utasaidia kuzalisha wahitimu wenye ushindani katika soko la ajira, wenye uwezo wa kujiajiri, kuajiri wengine na kuchangia maendeleo ya uchumi wa taifa.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...