Wednesday, May 27, 2026

HAKUNA NYONGEZA YA MUDA KWA MKANDARASI WA UJENZI WA BARABARA KAHAMA KUPITIA MRADI WA TACTIC - PROF. SHEMDOE

Na OWM - TAMISEMI, Kahama

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali haitomuongezea muda Mkandarasi M/s China Civil Engineering Construction Corporation wa kukamilisha miradi ya ujenzi wa barabara na mitaro katika Manispaa ya Kahama, inayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kwani ubovu wa miundombinu ya barabara imekuwa ni kero ya muda mrefu kwa wananchi wa manispaa hiyo.

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Mei 27, 2026 Katika Manispaa ya Kahama wakati wa hafla ya Utiaji Saini wa Mkataba wa Umaliziaji wa Ujenzi wa Barabara na Mitaro kupitia Mradi wa TACTIC, iliyofanyika katika eneo la Phantom kwenye manispaa hiyo.  

“Ninamueelekeza Mkandarasi Kampuni ya M/s China Civil Engineering Construction Corporation kumaliza ujenzi ndani ya muda ulioanishwa katika mkataba ambao wameusaini leo, hakutakuwa na nyongeza ya muda,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemtaka Mtaalamu Mshauri kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama  pamoja na TARURA katika kuhakikisha mikataba iliyosainiwa inatekelezwa kikamilifu na  inakamilika ndani ya muda uliopangwa na kwa ubora uliokubalika ili thamani ya fedha ionekane.

Prof. Shemdoe ameanisha kuwa Mei 27, 2026 imekuwa ni siku yenye furaha kwani kitendo cha kusainiwa kwa mikataba hiyo kinasadifu nia ya dhati ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwaboreshea miundombinu ya barabara wananchi wa Kahama, na kuongeza kuwa kama lilivyo jina lake amekuwa ni suluhu ya changamoto iliyokuwa ikiwakabili wananchi wa Manispaa ya Kahama.

“Tumeshuhudia utiaji saini wa mradi huu mkubwa wa zaidi ya Shilingi Bilioni 25 ambazo Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia zitumike kujenga miundombinu ya barabara katika Manispaa ya Kahama, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2025 hivyo tunamshukuru sana na kumuahidi kwamba ofisi yangu itasasimamia kikamilifu utekelezaji wa mkataba huo,” amesema Prof. Shemdoe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita amesema Manispaa ya Kahama inatekeleza mradi wa TACTIC kwa awamu mbili, awamu ya kwanza inahusisha ujenzi wa barabara za katikati ya mji (Central Business District (CBD) zenye urefu wa Kilomita 12.3 na barabara ya eneo la Zongomela kilomita tatu (3)  pamoja na ujenzi wa  mfereji wa maji ya mvua wa Chelsea – Lyazungu,  Shunu – Magobeko (Standalone Storm Water Drain).

Mhe. Mhita amesema kwamba, awamu ya pili ya utekelezaji wa mradi wa TACTIC katika Manispaa ya Kahama utahusisha ujenzi wa kituo cha mabasi Mbulu (Mbulu Bus Terminal), Soko la Sango (Sango Market) na Kituo kidogo cha mabasi cha Zongomela (Zongomela Mini Bus Stand).

Naye, Mratibu wa Miradi ya Ushirikiano na Benki ya Dunia  Mhandisi Humprey Kanyenye wa TARURA amesema kuwa, Mkandarasi  ambaye ni Kampuni ya M/s China Civil Engineering Construction Corporation anakwenda kutekeleza mradi huu katika Manispaa ya Kahama kwa gharama ya Shilingi za kitanzania Bilioni  25,547,162,432.04 bila VAT, na utatekelezwa kwa muda wa miezi nane (8) kuanzia  Juni 01, 2026 hadi Januari 31, 2027.















BARRICK NORTH MARA YAZINDUA KLINIKI AWAMU YA PILI YA UTATUZI WA MIGOGORO VIJIJI 11 VINAVYOZUNGUKA MGODI

Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kliniki ya kusikiliza na kushughulikia malalamiko ya wananchi dhidi ya Mgodi wa Barrick North Mara.
Meneja wa Idara ya Mahusiano ya Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Francis Uhadi, akizungumza wakati wa uzinduzi wa kliniki hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele na viongozi wa Barrick wakiwa katika picha ya pamoja na wadau wengine baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya Kiliniki ya Kusikiliza na Kushughulikia Malalamiko ya Wananchi.

****
Mgodi wa Barrick North Mara umezindua kliniki ya awamu ya pili maalum ya kusikiliza malalamiko , kero na migogoro ya wananchi ili kupata utatuzi wa kudumu kwenye vijiji 11 vinavyozunguka mgodi huo kwa ajili ya kuendelea kuboresha mahusiano kati ya mgodi na jamii.


Kliniki hiyo ya malalamiko inatoa fursa ya kuwakutanisha wananchi wanaozunguka mgodi huo na kutoa nafasi ya majadiliano ya kina, uwazi, kuboresha mahusiano ya kuaminiana na uwajibikaji kati ya jamii, mgodi na serikali na kuhakikisha malalamiko yanachukuliwa, yanapitiwa , kuweka kwenye kumbukumbu na hatimaye kushughulikiwa.

Kliniki hiyo inayojumuisha wajumbe kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Mgodi wa Barrick North Mara, Tume ya Haki za binadamu na utawala wa bora , asasi za kiraia- mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na wadau wengine, inalenga kuimarisha mahusiano kati ya mgodi na wananchi wa vijiji vinavyozunguka eneo hilo ili kuwezesha uwekezaji endelevu wenye maslahi mapana kwa wilaya , Mkoa na taifa kwa ujumla.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa kliniki hiyo ya pili katika kijiji cha Mjini Kati kilichopo Nyamongo, Wilayani Tarime, Mkuu wa Wilaya hiyo, Meja Edward Gowele alisema hatua hiyo itasaidia kupunguza na hatimaye kumaliza malalamiko na migogoro kati ya mgodi na jamii inayozunguka mgodi huo.

“Niupongeze mgodi wa Barrick North Mara kwa kufanya kliniki kwa awamu ya pili ni hatua kubwa na ni matumiani yangu kuwa itapunguza malalamiko na migogoro. Ili kujenga jamii ya amani na utulivu lazima tusikilizane na kutatua migogoro iliyopo,” alisema.

Meja Gowele alitumia nafasi hiyo pia kutoa wito kwa wanavijiji kujitokeza kuwasilisha malalamiko yao kwenye kliniki hiyo ili yapatiwe utatuzi kwa maendeleo na ustawi wa pande zote mbili.

Aidha, aliitaka kamati ya kliniki hiyo na viongozi wa vijiji kuhakikisha wananchi wanapata taarifa kwa wakati kuhusu mikutano ya kusikiliza na kupokea malalamiko yao itakayofanyika katika kila kijiji.

“Nimezindua rasmi kliniki hii, ipite kila kijiji na kusikiliza kila mwananchi mwenye malalamiko bila ubaguzi wala upendeleo,” Meja Gowele alisisitiza.

Ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki mpana wa wadau wote, klinki hiyo ina kamati inayojumuisha wafanyakazi wa mgodi, madawati ya malalamiko kutoka ofisi za Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, asasi za kiraia na wawakilishi wa jamii.

Gowele alisisitiza kwamba kwa watu waliopo ndani ya eneo la leseni ya Barrick North Mara kutii sheria bila shuruti na kuondoka ili kutokwamisha shughuli za mgodi huo.

Pamoja na mambo mengine , Mkuu wa Wilaya hiyo aliwataka watendaji wa Halmashauri ya Tarime kutoa ushirikiano kwenye miradi ya kimkakati katika wilaya hiyo ikiwemo ujenzi wa soko la dhahabu la Nyamongo na ujenzi wa stendi ya kisasa ya Nyamwaga.

“Nimeelezwa kwamba ili miradi hiyo iweze kuendelea ni lazima hati za maeneo husika zipatikane kwa wakati, watendaji hakikisheni unakamilisha taratibu zote zinazohitajika bila kuchelewesha maendeleo” , aliongeza.

Alisisitiza kwamba kukamilika kwa miradi hiyo ni hatua muhimu yenye kutia matumaini na kuongeza mahusiano mazuri kati ya wananchi na mgodi.

Akizungumza kwenye uzinduzi rasmi wa kliniki hiyo Mkoa Mara , Wilaya ya Tarime, Tarafa ya Nyamongo , Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mgodi wa Barrick North Mara, Franscis Uhadi alisema kwamba mahusiano kati ya mgodi na wananchi umezidi kuimarika ila bado kuna changamoto ambazo zinahitaji utatuzi wa kudumu ili kurahisisiha shughuli za uchimbaji na kuboresha mahitaji ya wananchi kupitia sheria na kanuni ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Alisema kwamba moja ya changamoto inayoendelea kujitokeza ni malipo ya fidia kwa wananchi akisema kwamba baadhi ya wananchi kwenye jamii kuendelea kugoma malipo ya fidia kwa kudai kwamba hajaridhishwa.

“Wananchi 728 walifanyiwa tathimini katika eneo la Nyabirama na malipo yao yapo tayari , kati yao 667 wamepokea fidia na kupisha shughuli za mgodi huku 61 wakiendelea kusubiri ambapo watu 44 ni wa familia moja,” alisema Uhadi.

Uhadi alisema kwamba mgodi wa umeendelea kutekeleza miradi ya jamii kupitia kanuni na sheria za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ambapo miradi 103 imepagwa kutekelezwa mwaka huu na huku 70 ikiwa tayari imekamilika na mengine ikiwa kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji.

Alisema kwamba kliniki hiyo itazunguka kwenye vijiji vyote 11 vinavyozunguka mgodi huo ili kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuweza kutatua changamoto zao moja kwa moja.

Kwa upande wake, Mwenyekiti mpya wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii (CDC) katika mgodi wa Barrick North Mara, Bogomba Rashid, alisema hatua hiyo ya kusikiliza na kutatua migogoro itasaidia pia kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika vijiji vinavyozunguka mgodi huo.

“Tukimaliza migogoro ambayo haina sababu ya kuwepo tutaendelea kufanya shughuli za maendeleo zaidi katika maeneo yetu,” alisema Bogomba ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kemambo.

Baadhi ya wananchi waliohudhuria shughuli hiyo ya uzinduzi wa kliniki walipongeza hatua hiyo ya mgodi wa Barrick North Mara kwa sababu itapunguza migogoro na kupanua wigo wa ushirikiano na kukuza mahusiano kati ya mgodi na jamii.

Mkazi wa Kijiji cha Kewanja , Mwita Omahe alisema kwamba pamoja na kuimarika kwa mahusiano kati ya jamii na mgodi ila bado kuna changamoto ya barabara mbovu za mitaa ambazo zinahitaji kushughulikiwa.

Katika awamu ya kwanza ya kliniki hiyo iliweza kuwafikia wananchi zaidi ya 1,688 na kero zilizopokelewa zilikuwa 137.

Vijiji vinavyozuguka mgodi huo ambavyo vitanufaika na kliniki hiyo ya wiki moja ni Mjini kati, Nyangoto, Kewanja, Matongo, Nyabichune, Kerende, Nyakunguru, komarera, Genkuru, Msege na Nyamwaga.

WADAU MBALIMBALI WAALIKWA KUCHANGIA BIL.3 KWA AJILI YA UNUNUZIBWA VIFAA VYA TAASISI YA MOYO KCMC.

 


NA REBECCA DUWE TANGA 


Hospitali ya Rufani KCMC ,imetangaza kuwa imeanza ujenzi wa Taasisi ya Moyo KCMC ili kusadia na kupunguza gharama inayotokana na safari ya umbali mrefu na foleni ya huduma kwa Wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete JKCI wakiwemo wale wanaosafirishwa nje ya Nchi .


Sambamba na wadau wa Maendeleo Mkoa wa Tanga wanatarajiwa kusaidia kuchangia kiasi cha Sh.Bil 3 kwaajili ya ununuzi wa vifaa kati ya Bil.25 zinazohitajika katika ujenzi wa Hospitali hiyo ambapo mpaka sasa kiasi cha Sh.22 Bil kimeshapatikana kutoka kwa Wadau wa Maendeleo nje ya Nchi.



Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ,Mkuu wa Mkoa wa Tanga Dkt.Batilda Buriani, alisema ujenzi wa Taasisi hiyo unakwenda kuwasaidia wakazi wa Mikoa ya Kanda ya kaskazini Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara kuwapunguzia gharama kubwa wanayotumia ya kwenda katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete JKCI pamoja na kuokoa gharama kubwa,


"Ujenzi wa Taasisi hii ya magonjwa ya moyo utawasaidia wakazi wa Tanga na Mikoa ya Kanda ya kaskazini lakini pia hata watu wengine kutoka Mikoa mingine ya jirani, kwasasa Wagonjwa wa moyo wanalazimika kusafiri hadi jijini Dar e S salaam katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete JKCI lakini wengine wanapata rufani yakwenda nje ya Nchi, lakini ujio wa Taasisi hiyo utaongeza upana wa huduma za moyo Nchini na kupunguza idadi ya Wagonjwa katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete JKCI" Alisisitiza Dkt.Batilda


Dkt.Batilda alisema asilimia 60 ya Wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete JKCI wanatoka Kanda ya kaskazini na kuwataka wadau wa Maendeleo mkoani Tanga kujitokeza kwa wingi May 30 kwenye harambee na wadau wa Maendeleo ukumbi wa Tanga Beach resort ili kuchangia pamoja na kupea fursa za ujenzi wa Taasisi ya moyo KCMC,


"Niwaombe sana wadau wa Maendeleo Mkoa wa Tanga tujitokeze kwa wingi kwenye harambee maalumu ili tuweze kuchangia ujenzi wa Taasisi ya moyo KCMC,lakini pia kwa wale ambao hawatoweza kufika naomba tujitokeze kwa michango"Balozi Batilda 


Kwa upande wake afisa miradi na mipango wa KCMC Emanuel Biyanchi alisema kuputia hafla hiyo wadau watapata taarifa sahihi kuhusu fursa kwenye sekta ya Afya uwekezaji,huduma za Afya miradi ya maendeleo na maeneo ya mashirikiano ya kibiashara na kijamii ndani KCMC na taasisi zake.


Aliongeza kusema kuwa sekta ya Afya si tu eneo huduma pekee bali ni fursa kwa wawekezaji , ajira,ubunifu na Tahiti na maendeleo ya jamii.


samabamba na hayo alisema hafla hiyo itatoa nafasi majadiliano yankaribu kati y wadau, wawekezaji Viongozi na Taasisi mbalimbali kuhusu namna bora ya kushirikiana kati ya miradi ya maendeleo inayolenga kuboresha huduma za Afya na ustawi wa jamii.

Wednesday, May 20, 2026

KAPINGA AIPONGEZA SBC KWA KUONGEZA UWEZO WA UZALISHAJI


NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Viwanda na Biashara, Mhe. Judith Kapinga, amewahimiza wawekezaji na wafanyabiashara nchini kuhakikisha wanalinda haki na usalama wa watumiaji kwa kuzingatia kanuni bora za uzalishaji kuanzia ununuzi wa malighafi, usafirishaji hadi uchakataji wa bidhaa ili kuzalisha bidhaa zenye viwango vya juu vya ubora vinavyokidhi matakwa ya walaji.

Waziri Kapinga ameyasema hayo leo Mei 20, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa upanuzi wa kiwanda cha kutengeneza vinywaji baridi cha SBC Tanzania (PEPSI).

Aidha, amewataka wawekezaji na wafanyabiashara kuendelea kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ili kuhakikisha uzalishaji wenye tija unaowanufaisha wao binafsi pamoja na Taifa kwa ujumla.

“Endeleeni kutekeleza maelekezo mnayopewa na mamlaka za usimamizi zilizowekwa pamoja na kulipa kodi kwa hiari ili kuiwezesha Serikali kuendelea kutoa huduma bora na kuleta maendeleo kwa wananchi,” amesema Waziri Kapinga.

Sambamba na hilo, amezitaka mamlaka zote za usimamizi nchini kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uaminifu na uadilifu wa hali ya juu ili kurahisisha shughuli za uwekezaji na uzalishaji nchini.

Amesema ni muhimu mamlaka hizo kuweka mazingira rafiki yatakayowawezesha wawekezaji na wafanyabiashara kutimiza matakwa ya kisheria bila vikwazo, kupitia utoaji wa elimu, ufuatiliaji na ukaguzi wa mara kwa mara katika viwanda na biashara mbalimbali.

“Katika kutekeleza majukumu yenu hakikisheni hamuweki vikwazo kwa wawekezaji, bali mnaendelea kutoa elimu na kufanya ukaguzi ili kuona sheria, kanuni na taratibu zinafuatwa ipasavyo,” amesema.

Waziri Kapinga amesema Serikali inaendelea kujizatiti katika kuhakikisha uwepo wa mazingira wezeshi kwa wawekezaji kupitia maboresho ya sera, maendeleo ya miundombinu pamoja na ushirikiano endelevu na sekta binafsi kwa lengo la kuvutia uwekezaji na kuongeza ushindani wa bidhaa za Tanzania katika masoko ya ndani na nje ya nchi.

Aidha, amepongeza uongozi wa SBC Tanzania Ltd kwa dhamira yao ya kupanua uwezo wa uzalishaji, kuongeza ajira na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Wilaya ya Temeke na Taifa kwa ujumla.

Amesema uwekezaji huo unaendana na dira ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda wenye ushindani, unaozalisha ajira, kuongeza thamani ya bidhaa na kuchochea ukuaji endelevu wa uchumi.

“Mchango wa SBC Tanzania Limited katika uchumi wetu ni mkubwa kwani kampuni hiyo inachangia takribani shilingi bilioni 150 kila mwaka kupitia kodi za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja, hali inayoiwezesha Serikali kuendelea kutoa huduma muhimu za kijamii na kuendeleza miundombinu,” ameeleza Waziri Kapinga.

Ameongeza kuwa kampuni hiyo kwa sasa inatoa ajira za moja kwa moja kwa zaidi ya wafanyakazi wa kudumu 1,500 sambamba na ajira nyingi zisizo za moja kwa moja kupitia mnyororo wake wa usambazaji, sekta ya usafirishaji pamoja na viwanda saidizi.



Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa SBC Tanzania Ltd, Ziad El Khalil, amesema upanuzi wa kiwanda hicho unalenga kuongeza uwezo wa uzalishaji ili kukidhi mahitaji ya soko pamoja na kuendelea kuchangia maendeleo ya uchumi wa nchi.

Amesema wataendelea kushirikiana na serikali katika kuhakikisha wanazalisha bidhaa zilizobora na zinazokidhi matakwa ya viwango.

Tuesday, May 19, 2026

CGP KATUNGU - MAFUNZO YA MFUMO WA 'GAMIS' NI UTEKELEZAJI WA MAAGIZO YA RAIS DKT SAMIA




Na. Sgt. Geofrey Jacka - DODOMA

Kamishna wa Sheria na Uendeshaji wa Magereza, CP.
Nicodemus Tenga, kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Magereza Tanzania, CGP. Jeremiah Yoram Katungu, Mei 19, 2026 amefungua Mafunzo ya Mfumo wa Usimamizi wa Mali za Kudumu za Serikali (GAMIS), akieleza kuwa kufanyika kwa mafunzo hayo ni utekelezaji wa Maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.

CP. Tenga amesema, katika kuhitimisha Mafunzo ya Uongozi kwa Maafisa Magereza, Mei 9, 2026 Ukonga Dar Es Salaam, Rais Dkt. Samia, aliekeleza Jeshi la Magereza kutumia TEHAMA katika utendaji wake ili kuongeza ufanisi na uwazi serikalini na kuendana na kasi ya mabadiliko ya Teknolojia.

Aidha, CP. Tenga, amesema ni matarajio ya Jeshi baada ya mafunzo hayo, wataalamu wa ununuzi watakuwa na maarifa mapya ya kutumia mfumo wa GAMIS na kuwaongezea uelewa wa Sheria na Kanuni za usimamizi wa mali za kudumu za Serikali, kuongeza uwajibikaji, kuboresha utunzaji wa kumbukumbu na kuimarisha usimamizi wa rasilimali za Serikali ikiwemo uhamishaji, uazimishaji na uondoshaji wa mali.

"Ndugu washiriki, majukumu ya ugavi ni mhimili muhimu katika utendaji wa Jeshi, ufanisi wa kazi zenu una mchango mkubwa katika kuhakikisha upatikanaji wa vifaa na huduma muhimu kwa wakati, uwazi na kwa kuzingatia thamani ya fedha, hivyo niwatake muwe makini wakati wote wa mafunzo ili yaweze kuwa na tija" alisema CP. Tenga

Akitoa taarifa ya mafunzo, Mkuu wa Kitengo cha Ununuzi Jeshi la Magereza, ACP Henry Masawe amesema, Jeshi la Magereza lina jukumu la kutunza na kuhifadhi vifaa na mali zote za kudumu kwa ufanisi na kufuatilia utunzaji sahihi wa kumbukumbu zake hadi pale zitakapo ondoshwa.

Aidha ACP. Masawe, amesema lengo la mafunzo hayo ni kuwawezesha wagavi kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yao kufuatilia na kusimamia mali zote za kudumu za Serikali kwa kutumia mfumo.

Mafunzo hayo ya siku nne ya GAMIS, yanafanyika katika Ukumbi wa Rugimbana jijini Dodoma, yakiweka msisitizo kuwa matumizi ya mifumo ya kisasa ni sehemu muhimu ya kuimarisha uwajibikaji, uwazi na ufanisi katika utendaji wa Jeshi la Magereza.

Sunday, May 17, 2026

HISTORIA NA MAFANIKIO YA TANZANIA PRISONS SC YAWEKWA WAZI KWA MASHABIKI, JIJINI DODOMA



Na. Ssgt Mawazo Mtondo - Dodoma.

Mkuu wa Sehemu ya Huduma kwa wafungwa (OMS)Jeshi la Magereza, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP) Emmanuel Malisa, leo Mei 17, 2026 ameongoza kikao cha wadau, marafiki na wapenzi wa timu ya Tanzania Prisons FC, ambapo amewasisitiza kuendelea kudumisha ushirikiano, umoja na mshikamano kati ya mashabiki, wachezaji, viongozi wa timu pamoja na viongozi wakuu wa Jeshi la Magereza, kwa lengo la kuimarisha maendeleo na mafanikio ya klabu hiyo.

Aidha, SACP. Malisa amesisitiza umuhimu wa mshikamano na kujitolea kwa kila mdau katika kuhakikisha timu hiyo inaendelea kufanya vizuri ndani na nje ya uwanja. Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Makao Makuu ya Jeshi la Magereza Msalato, Jijini Dodoma.

Akisoma wasilisho la rasimu ya katiba ya matawi ya marafiki wa Tanzania Prisons Sports Club, Mrakibu Mwandamizi wa Jeshi la Magereza (SSP) Bakari Sudi alisema Jeshi la Magereza lina timu inayoshiriki Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara pamoja na timu nyingine mbalimbali zinazoshiriki michezo tofauti ikiwemo riadha, mpira wa wavu, mpira wa kikapu, netiboli, mieleka, judo, magongo, vishale na ngumi.

SSP. Sudi, pia alieleza historia ya mafanikio ya Tanzania Prisons SC, akibainisha kuwa timu hiyo iliwahi kutwaa ubingwa wa Kombe la Muungano mwaka 1999, mashindano yaliyokuwa yakizikutanisha timu bora kutoka Tanzania Bara na Zanzibar kwa lengo la kupata mwakilishi wa Tanzania katika michuano ya kimataifa.

Kutokana na mafanikio hayo, Tanzania Prisons SC ilipata nafasi ya kushiriki michuano ya CAF Champions League mwaka 2000 ambapo iliishia hatua ya awali. Aidha, klabu hiyo pia ilishiriki michuano ya CAF Confederation Cup mwaka 2005 na 2009, na katika misimu yote miwili iliaga mashindano hayo katika hatua za mwanzo.

Tanzania Prisons SC ni moja ya klabu zinazojivunia kuwa na mashabiki wengi nchini, ambapo wengi huamini kuwa baada ya klabu za Simba SC na Yanga SC, Tanzania Prisons SC ni miongoni mwa timu inayofuatia kwa kuwa na wapenzi na mashabiki wengi wa soka hapa nchini.




Kwa sasa Tanzania Prisons SC ipo katika nafasi ya 15 kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na pointi 17 baada ya kucheza michezo 23, huku ikiendelea kupambana kujinasua kutoka maeneo ya chini ya msimamo na kusaka matokeo bora katika michezo iliyosalia ya msimu huu.



Saturday, May 16, 2026

WADAU WA SIASA WATAKA MARIDHIANO KUNUSURU NCHI

Katibu Mkuu wa Chama cha Maendeleo ya Uma (Chauma) na aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi wa mwaka 2025, Salum Mwalimu, ametoa wito wa kuwepo kwa klasi katika kupatikana kwa maridhiano yanahitajika kwa dharura na kuonya kuwa mtu yeyote mwenye nia ya kutaka yaliyotokea Oktoba 29 yajirudie hatakuwa miongoni mwa Watanzania na anapaswa kukataliwa. 

Mwalimu ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam wakati wa mjadala wa kitaifa kuhusu hatima ya nchi ulioandaliwa na Chama cha ACT Wazalendo. 

.Mwalimu alieleza kuwa kila mtu anajua kilichotokea siku hiyo ya uchaguzi, ikiwemo mauaji na uwepo wa changamoto kubwa ya ajira kwa vijana, lakini akasisitiza kuwa kikwazo kikubwa kwa sasa imekuwa ni wanasiasa kushindana maneno majukwaani na kuonyesha umahiri wa kusema badala ya kugusa kiini cha tatizo na kutoa majawabu ya kuivusha nchi.

Kutokana na hali hiyo, Salum Mwalimu alimpongeza Mwenyekiti wa ACT Wazalendo, Othman Masoud Othman, kwa kuitisha mjadala huo na kumtaka asione aibu kusimamia jawabu aliloliwasilisha kupitia kijitabu chake kilichosisitiza haja ya kuanzisha jukwaa la majadiliano ya kitaifa yatakayoongozwa na misingi ya ukweli, haki na uwajibikaji. 

Mwalimu alimshauri Othman kuchukua uongozi na kuunda kamati itakayojumuisha watu mbalimbali ili kuanzisha jukwaa hilo, si kama mwenyekiti wa chama bali kama kiongozi mwandamizi wa kisiasa atakayeungwa mkono na vyama vingine, kwa lengo la kupata ukweli na kuweka mifumo ya jinsi viongozi wa kisiasa wanavyopaswa kuwajibika.

Kwa upande wake, mwandishi na mchambuzi wa masuala ya siasa, Ezekiel Kamwaga, alisema kuwa nchi inahitaji utashi wa kisiasa kabla ya kuanza kuzungumza ukweli, huku akionya kuwa viongozi wengi wa sasa wanaonekana kuwa wepesi kukimbilia mitandao ya kijamii badala ya kuonyesha uongozi thabiti. 

Kamwaga alifafanua kuwa kiongozi mzuri ni yule anayesimama mbele na kuwa tayari kupokea lawama au kuzomewa, lakini anakaa nyuma wakati wa kupokea sifa, sifa ambayo kwa sasa inaonekana kupotea miongoni mwa viongozi.

Naye mwanasiasa Odero Odero aliwataka viongozi wa upinzani kuacha kulia na badala yake watafute suluhu ya kweli kwa kukabiliana na Rais Samia Suluhu Hassan kwenye meza ya mazungumzo. 

Odero aliwashauri viongozi hao akiwemo Othman Masoud, Zitto Kabwe, na John Heche kuondoa tabia ya kuogopana na kujificha kwani Rais Samia ni kama dada na mama yao, na njia pekee ya kuifikisha nchi mbali ni kukaa naye meza moja ili kieleweke. 

Suala hili la maridhiano ni sehemu ya falsafa ya uongozi ya Rais Samia kupitia '4R' zake ambazo ni Maridhiano, Ustahmilivu, Mabadiliko na Kujenga upya, ambapo hivi karibuni aliahidi kuunda kamati ya maridhiano baada ya kupokea ripoti ya Tume ya Kuchunguza Matukio Wakati na Baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.

SWICA YAIBUA MATOKEO CHANYA KISESA


Na Beatus Maganja , Dodoma

Mbunge wa Jimbo la Kisesa, Mhe. Musa Godfrey Mbunga, ameipongeza Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuanzisha utaratibu wa Uwekezaji Mahiri wa maeneo ya uhifadhi ujulikanao kama Special Wildlife Investment Concession Areas (SWICA), akisema mfumo huo umeleta manufaa makubwa kwa wananchi wanaoishi jirani na Hifadhi ya Maswa mkoani Simiyu.

Mhe. Mbunga alitoa pongezi hizo bungeni jijini Dodoma tarehe 15 Mei, 2026 wakati wa mjadala wa Bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2026/2027.

Amesema utekelezaji wa utaratibu huo umewezesha wananchi wa maeneo mbalimbali ndani ya jimbo lake kunufaika moja kwa moja na mapato yatokanayo na uwekezaji unaofanyika katika maeneo ya uhifadhi.

“Wizara imeanzisha utaratibu wa Uwekezaji Mahiri (SWICA), na utaratibu huu umesaidia sana wananchi kunufaika na uwekezaji unaofanyika kwenye Hifadhi ya Maswa,” alisema Mhe. Mbunga.

Mbunge huyo alieleza kuwa kupitia mfumo huo, jimbo la Kisesa limepokea takribani shilingi milioni 973 zilizosaidia utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo tofauti ya jimbo hilo.

Alifafanua kuwa kijiji cha Matale kilipokea zaidi ya shilingi milioni 390 zilizotumika kujenga zahanati, nyumba za watumishi pamoja na wodi ya wazazi.

Aidha, alisema maeneo ya Ng’hanga na Bulyandulu kila moja lilipata shilingi milioni 181 zilizosaidia ujenzi wa nyumba za watumishi, huku Mbugayabang’hya ikinufaika na shilingi milioni 216 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya wananchi.

Mhe. Mbunga amesema mafanikio hayo yanaonesha namna Serikali inavyoendelea kuhakikisha wananchi wanaozunguka maeneo ya uhifadhi wananufaika na rasilimali za taifa kupitia uwekezaji wenye tija.

“Ni lazima kuishukuru Serikali kwa hatua hizi ambazo zimeendelea kuleta maendeleo kwa wananchi wetu,” alisisitiza.

Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii inayoongozwa na Mhe. Waziri Dkt . Ashatu kijaji (Mb) imeendelea kusisitiza ushirikishwaji wa wananchi katika shughuli za uhifadhi na uwekezaji ili kuhakikisha rasilimali za maliasili zinachangia maendeleo ya jamii pamoja na uchumi wa Taifa.

Friday, May 15, 2026

WANAWAKE WAPEWA ELIMU YA MLIPA KODI ILI KUICHANGAMKIA FURSA

 


NA REBECCA DUWE TANGA 


Wadau wa maendeleo wameombwa kushirikiana na Mamlaka ya mapato Tanzania TRA mkoa wa Tanga kutoa elimu kwa makundi ya wanawake ili waweze kuzikia fursa mbalimbali na hatimaye waweze kulipa kodi kwa maendeleo ya nchi.


Meneja wa Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga CPA Castro John ametoa kauli hiyo leo may 14, 2026 alipokuwa akifungua jukwaa la wanawake na kodi lililoandaliwa na Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Tanga na kufadhiliwa na shirika la GIZ lenye kauli mbiu isemayo "Wanawake na kodi nguzo ya maendeleo ya Taifa"


"Kwa wadau wetu wa taasisi za kifedha tunaomba muendelee kushirikiana nasi katika kuwawezesha wanawake ili kukuza biashara zao kwa misingi ya sheria na kodi" Amesema Meneja Castro 

Katika hatua nyingine Castro alisema Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA Mkoa wa Tanga, ina jukumu la  kutoa Elimu ya mlipakodi pamoja na fursa mbalimbali zinazowazunguka Wanawake Wafanyabiashara na Wajasiriamali ili kumuwawezesha kutanua uelewa juu ya mifumo na Sheria za Kodi Nchini.


"TRA inatambua mchango wa Wanawake katika ulipaji wa Kodi na kwasasa Wanawake wamekuwa mstari wa mbele katika ulipaji wa Kodi Nchini,hivyo naomba muendelee kuwa mstari wa mbele katika ulipaji wa Kodi ili tulijenge Taifa letu"Aliongeza Castro 


Castro aliwataka Wanawake kuendelea kudumisha nidhamu ya ulipaji wa Kodi Nchini nakwamba Mamlaka hiyo ipo tayari wakati wowote kutoa msaada kwa mfanyabiashara anayepitia changamoto yoyote,


"Niwaombe muendelee kudumisha nidhamu ya ulipaji wa Kodi mliyonayo ili tuondoe usumbufu wowote unaoweza kujitokeza endapo mtu atakwepa kulipa Kodi,TRA ipo tayari wakati wowote kutoa msaada kwa mfanyabiashara anayepitia changamoto yoyote, niwaombe ukiwa na changamoto yoyote tuambie tukusaidia usikae nayo alafu baadae unakuja kulalamika" Alisisitiza Castro 


Kwaupande wake,Naibu Katibu wa Jumuiya ya Nchini Wafanyabiashara, Ismail Masoud aliwataka watumishi wa TRA kuwasaidia kutoa Elimu Wafanyabiashara mkoani Tanga ili kuondoa kasoro nyingi zinazowakabili Wafanyabiashara,


"Niwaombe TRA iendelee kutoa Elimu ya mlipakodi ili changamoto za Wafanyabiashara hususani zinazotokana na Elimu ziishe, lakini pia kwasisi Wafanyabiashara,tuache janja janja zakukwepa Kodi, tunataka twende pamoja ili tuweze kufanikisha dira ya Taifa 2050" Alisisitiza Masoud.


Kwa upande wake Afisa maendeleo mkoa wa Tanga Charles Mtali amesema wanawake wana mchango mkubwa wa maendeleo ya kiuchumi .

tofauti na wanaume hivyo wasipowezeshwa itakuwa ni vigumu nchi kufikia malengo yake.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...