Saturday, September 5, 2026

KABLA YA PENSHENI DAIMU SALUM MKWAWA ATOA SOMO LA KUWEKEZA MAPEMA KWA AJILI YA MAISHA BAADA YA KUSTAAFU

Hii ndio Royal Woodbridge Hotel iliyojengwa na kuwekezwa na mstaafu Daim Salum Mkwawa Hotel hii ipo  Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma mkabala na stendi ya Seedfarm njia inayokwenda Songea-Tunduru-LindiMuonekano wa ndani wa Hotel ya Royal Woodbridge iliyopo Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma inayomilikiwa na Daimu Salum Mkwawa


Hapa ni eneo la kupatia chai na chakula katika Hotel ya Royal Woodbridge iliyopo Seedfarm Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma

Na Regina Ndumbaro Songea-Ruvuma

Kustaafu kutoka kwenye ajira hakumaanishi mwisho wa uzalishaji au mchango wa mtu katika uchumi wa nchi, bali kunaweza kuwa mwanzo wa hatua nyingine ya maisha endapo mtumishi ataandaa mapema shughuli za kiuchumi zitakazomsaidia baada ya kuondoka kazini.

Hilo ni miongoni mwa masomo yanayoweza kupatikana katika safari ya Daimu  Salum Mkwawa, msomi na mwanazuoni aliyewahi kufanya kazi katika taasisi mbalimbali za Serikali na baadaye kuhudumu katika Umoja wa Mataifa (UN) kwa miaka 18.

Mkwawa, ambaye sasa ni mstaafu, anasema umuhimu wa kujiandaa kwa maisha baada ya kustaafu haupaswi kuanza siku mtu anapomaliza ajira, bali unapaswa kuanza mapema wakati bado ana nguvu, kipato na uwezo wa kupanga maisha yake ya baadaye.

Anaeleza kuwa yeye mwenyewe alianza kuanzisha miradi mbalimbali ya maendeleo tangu mwaka 1992, wakati bado akiwa katika ajira, ikiwa ni pamoja na miradi aliyoianzisha Dar es Salaam.

Safari yake ya kikazi ilimfikisha katika Wizara ya Kilimo na Kiwanda cha Sukari Kilombero, ambako anasema alipata pia uzoefu wa namna ya kutengeneza sukari.

Katika upande wa elimu, amesoma katika vyuo mbalimbali, vikiwemo Sokoine University of Agriculture (SUA) na Chuo Kikuu cha Manchester nchini Uingereza, kabla ya kuendelea na safari yake ya kitaaluma na kikazi.

Mwaka 1996, alifanya kazi na Umoja wa Mataifa hapa nchini kwa kipindi cha miaka 18, akihudumu kwa ukaribu zaidi na Serikali za Mitaa.

Baada ya mkataba wake nchini Tanzania kumalizika, Mkwawa anasema Umoja wa Mataifa ulimpa fursa ya kuendelea kufanya kazi nje ya nchi kutokana na uzoefu na umahiri aliokuwa ameonesha kazini.

Hata hivyo, aliamua kubaki Tanzania. Sababu mojawapo ilikuwa uwekezaji aliokuwa ameanza kuujenga nchini, pamoja na kuzingatia familia na umri ambao ulikuwa umeendelea kusogea.

Uamuzi huo ulimfanya aendelee na safari yake ya ujasiriamali, ikiwemo uwekezaji katika sekta ya hoteli.

Moja ya uwekezaji huo ni Royal Woodbridge Hotel, iliyopo Kata ya Seedfarm, Manispaa ya Songea, Mkoa wa Ruvuma.

Kwa Mkwawa, uwekezaji huo siyo tu shughuli ya kibiashara, bali ni sehemu ya namna mstaafu anaweza kuendelea kutumia uzoefu, mtaji na maarifa aliyoyapata katika maisha ya ajira kwa ajili ya kujenga uchumi wake na kuchangia uchumi wa jamii inayomzunguka.

Hoteli hiyo kwa sasa ina vyumba 20, ikiwa na matarajio ya kufikia vyumba 30, pamoja na mpango wa kuwa na eneo la kuogelea na ukumbi wa mikutano.

Pamoja na kutoa huduma za malazi, uwekezaji huo umewezesha ajira kwa vijana wa kike na wa kiume, huku hoteli ikinunua bidhaa za chakula kutoka kwa wajasiriamali na wafanyabiashara wa sokoni.

Kwa namna hiyo, shughuli za hoteli zinakuwa sehemu ya mnyororo wa kiuchumi unaowaunganisha mmiliki wa biashara, wafanyakazi, wakulima, wafanyabiashara wa masoko, wasambazaji wa bidhaa na Serikali kupitia mapato mbalimbali.

Mkwawa pia anasisitiza umuhimu wa rasilimali watu katika sekta binafsi, akisema wafanyakazi wanahitaji mafunzo ya mara kwa mara ili kuongeza uwezo wao na kuhakikisha wageni wanapata huduma bora.

Huduma zinazopatikana katika hoteli hiyo ni pamoja na chakula, usalama ndani na nje ya eneo la hoteli, CCTV camera, Wi-Fi ya bure, parking ya magari, restaurant na kifungua kinywa cha bure kwa wageni wanaolala hotelini hapo.

Pia, hoteli hiyo ina mazingira yanayovutia kwa ajili ya kupiga picha, hali ya hewa inayovutia na vyumba vinavyolenga kutoa viwango vya huduma vinavyolingana na thamani ya fedha anayolipa mgeni.

Mkwawa anasema usalama, chakula bora, malazi yenye viwango na huduma zinazokidhi mahitaji ya wageni ni sehemu muhimu ya uwekezaji katika sekta ya utalii na ukarimu.

Kwa upande mwingine, anaitaja Serikali kama mshirika muhimu katika mafanikio ya wafanyabiashara, akipongeza ushirikiano uliopo baina ya Serikali na sekta binafsi.

Anaiomba Serikali kuendelea kuangalia mazingira ya wafanyabiashara, hususan biashara changa, wakati wa ukusanyaji wa kodi, ili kuwe na mazingira ambayo Serikali inapata mapato na mfanyabiashara anaendelea kufanya biashara yenye faida na endelevu.

Kwa maoni yake, Serikali inapaswa pia kuwa mshauri wa wafanyabiashara na kuwasaidia kufikia huduma za mikopo kwa urahisi zaidi.

Mchango wa uwekezaji huo unaonekana pia katika mapato ya Serikali kupitia Manispaa ya Songea na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), huku ajira na ununuzi wa bidhaa kutoka kwa wajasiriamali wa eneo hilo ukiendelea kuongeza mzunguko wa fedha katika uchumi wa Songea.

Mkwawa anasema uzoefu wake ni ushahidi kwamba maandalizi ya maisha baada ya kustaafu yanaweza kufanyika hatua kwa hatua, badala ya kusubiri mtu aondoke kazini ndipo aanze kutafuta shughuli ya kumuingizia kipato.

Kwa wastaafu na watumishi wanaokaribia kustaafu, simulizi hii inaweza kuwa ukumbusho wa umuhimu wa kuanza mapema kupanga maisha ya baada ya ajira, ikiwa ni pamoja na kuwekeza katika shughuli halali na endelevu kulingana na uwezo na utaalamu wa mtu.

Hatua hiyo inaweza kusaidia kupunguza utegemezi wa pensheni pekee na kumwezesha mstaafu kuendelea kuwa mzalishaji, mwajiri na mshiriki wa shughuli za maendeleo katika jamii.

Kwa upande wa Mkoa wa Ruvuma, Mkwawa anasema uwekezaji katika huduma za malazi na biashara nyingine unaweza kusaidia kuongeza uwezo wa Songea kuhudumia wageni kutoka ndani na nje ya nchi.

Royal Woodbridge Hotel, iliyopo katika Kata ya Seedfarm, Manispaa ya Songea, kando ya barabara kuu ya Songea–Tunduru–Lindi, ni miongoni mwa uwekezaji unaoonesha namna sekta binafsi inavyoweza kushiriki katika kutoa huduma, ajira na kuchochea shughuli za kiuchumi.

Mkwawa anawakaribisha wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, mikoa jirani ya Tanzania pamoja na wageni kutoka nje ya nchi wanaofika Songea kutumia huduma zinazopatikana katika hoteli hiyo na kujionea wenyewe namna huduma zinavyotolewa.

Pia anasema hoteli hiyo inawezesha usafiri wa ndani ya Mkoa wa Ruvuma kwa wageni wanaohitaji huduma hiyo.

Ujumbe mkubwa unaotokana na safari yake ni kwamba maandalizi ya kustaafu yanapaswa kuanza kabla ya kustaafu. Kwa mtumishi mwenye uwezo na mpango, ajira inaweza kuwa chanzo cha mtaji wa kuanzisha uwekezaji wa baadaye, huku uzoefu wa kazi ukiwa rasilimali muhimu katika kusimamia biashara na kutoa mchango zaidi kwa jamii.

Kwa Taifa, simulizi kama hii inaendelea kuonesha umuhimu wa kuimarisha mazingira ya uwekezaji wa ndani ili wastaafu, wafanyakazi na wajasiriamali waweze kutumia maarifa, uzoefu na mitaji yao kujenga biashara, kutoa ajira na kuongeza shughuli za uzalishaji nchini.

BANDARI YA DAR ES ALAAM KUPANUA UWEZO KUPITIA MIRADI MIKUBWA




Na Sheila Ahmadi, Dar esalaam

Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati katika Bandari ya Dar es Salaam, inayolenga kuongeza uwezo wa kuhudumia mizigo, kuimarisha ufanisi wa bandari na kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kutoka bandarini kwenda maeneo mbalimbali nchini na nje ya Tanzania.

Akizungumza Jijini Dar es salaam na Wanahabari Mara baada ya Kukagua miradi ya kimkakati kwenye bandari ya Dar esalaam Mkurugenzi wa huduma za uhandisi wa bandari Hiyo Mhandisi Erick Madinda, amesema kuwa utekelezaji wa miradi hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kufanya maboresho makubwa katika sekta ya bandari ili kuongeza uwezo wa kupokea na kuhudumia mizigo kwa wakati, pamoja na kuimarisha ushindani wa Bandari ya Dar es Salaam katika ukanda wa Afrika Mashariki.

eneo la Malindi ni miongoni mwa maeneo yanayofanyiwa maboresho kupitia mradi wa upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam ambao unajumuisha ujenzi na uboreshaji wa Gati, maeneo ya magari ambapo Mradi huo unagharimu zaidi ya Shilingi bilioni 5.44.

Madinda alisema Kurasini Logistics Centre ni miongoni mwa miundombinu muhimu inayojengwa kwa ajili ya kupokea na kuhifadhi mizigo kabla ya kukamilishwa kwa taratibu za kisheria na baadaye kusafirishwa kwenda maeneo mbalimbali ndani na nje ya Tanzania.

Aidha kituo hicho chenye ukubwa wa takribani mita za mraba 200,000 kitakuwa na uwezo wa kuhudumia zaidi ya makontena 14,000, jambo litakalosaidia kupunguza muda wa mizigo kukaa katika yadi za bandari na kuongeza kasi ya utoaji wa mizigo.

“Kurasini Logistics Centre itaunganishwa na reli za Standard Gauge Railway (SGR) na Meter Gauge Railway (MGR), ili kuwezesha mizigo kusafirishwa moja kwa moja kutoka bandarini kwenda maeneo mbalimbali kwa njia ya reli,” alisema Madinda"

Katika hatua nyingine Madinda Ameongeza kuwa Bandari ya Dar es Salaam kwa sasa inapokea takribani tani milioni 33.7 za mizigo kwa mwaka, huku Serikali ikiendelea kuboresha miundombinu ya barabara na reli pamoja na mifumo ya usafirishaji wa mizigo ili kuongeza ufanisi na kupunguza msongamano wa malori.

Hata hivyo ziara hiyo ilihusisha ukaguzi wa ujenzi wa Single Receiving Terminal (SRT), mradi unaolenga kuboresha upokeaji na usafirishaji wa mafuta kutoka bandarini.

Mradi huo unatarajiwa kurahisisha upokeaji wa mafuta kutoka kwenye meli na kupunguza gharama za uendeshaji. Unajumuisha matanki 15 kwa ajili ya kuhifadhi dizeli na petroli.

Kwa upande wake Mhandisi Mshauri wa mradi huo, Jamal Mluma, alisema ujenzi wa SRT umefikia asilimia 52.8 na unagharimu Sh bilioni 678.6.

Vilevile mradi huo utakapokamilika utakuwa na mfumo wa kisasa wa kuhifadhi mafuta kwa muda mfupi na kutumia teknolojia za kisasa katika uendeshaji wake. Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwaka 2027.

Naye Makamu wa Rais wa Serikali ya Wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ( UDSM) Kareen Marry, alisema ziara hiyo imewapa fursa ya kujionea kwa vitendo utekelezaji wa miradi ya Serikali, akieleza kuwa hatua hizo zinaonyesha dhamira ya Serikali ya kuboresha huduma za bandari na kupunguza changamoto ya foleni pamoja na muda wa meli na malori kukaa bandarini.








Thursday, September 3, 2026

Iran yashambulia kambi za kijeshi za Marekani Kuwait


Kumekuwa na ripoti za mashambulizi ya makombora na ndege zisizo na rubani za Iran kwenye kambi za Marekani huko Kuwait

Saa moja baada ya jeshi la Kuwait kutangaza katika taarifa kwamba mifumo yake ya ulinzi wa anga ilikuwa imeshirikishwa ili kurudisha kutungua mashambulizi ya ndege zisizo na rubani na makombora yanayotoka Iran, shirika la habari la Tasnim, karibu na Walinzi wa Mapinduzi, liliandika: "Kambi za Marekani huko Kuwait zilishambuliwa na makombora na ndege zisizo na rubani za Iran."

Shirika la habari halikutoa maelezo zaidi kuhusu tukio hilo, na CENTCOM - Amri Kuu ya jeshi la Marekani - bado haijajibu ripoti hizo.

Udhibiti mkali katika nchi za Ghuba ya Uajemi umefanya iwe vigumu sana kwa vyombo vya habari kupata ufikiaji wa moja kwa moja kwenye maeneo yaliyoshambuliwa, na Marekani imeweka vikwazo kwenye uchapishaji wa picha za setilaiti za maeneo haya.

Siku ya Jumatano, Tasnim ilichapisha picha za angani zinazohusishwa na mashambulizi yake ya Jumanne kwenye kambi za Marekani huko Jordan, ikidai kuonyesha athari zilizoachwa na mashambulizi haya.

Saturday, August 29, 2026

NDEJEMBI AAPISHWA IKULU! RAIS SAMIA ASEMA 'NAFASI IMEKABIDHIWA KWA KIJANA KAWATUMIKIE WATANZANIA BILA KUJALI TOFAUTI ZAO'

 Na Janeth Raphael - MichuziTv -Ikulu Chamwino


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema uamuzi wa kumteua Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ulizingatia sifa, uzoefu na uwezo wake wa kubeba dhamana kubwa ya uongozi wa taifa.

Rais Samia amesema nafasi hiyo imekabidhiwa tena kwa kijana, akimtaka Ndejembi kutumia fursa hiyo kujifunza, kukua kiakili na kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii na uaminifu kwa maslahi ya Watanzania.

Akizungumza leo, Agosti 29, 2026, katika hafla ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema uamuzi wa kumrudisha kijana katika nafasi hiyo ulifanyika kwa kauli moja.

“Kwa kauli moja tuliamua kuirudisha nafasi ya Makamu wa Rais kwa vijana na tuendelee kulea. Imetoka kwa kijana na tumeirudisha kwa kijana. Tunakuomba kijana (Ndejembi) ukakue sio kwa umri bali ukakue kiakili, tumekupa majukumu makubwa ni imani yangu utaweza,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema Ndejembi alipata uungwaji mkono wa wabunge kwa kauli moja kutokana na sifa alizonazo zinazomfanya astahili kushika nafasi hiyo.

“Wabunge walimpitisha Deogratius Ndejembi kwa kauli moja kwa kuzingatia sifa za Makamu wetu wa Rais,” amesema.

Amesema kabla ya kufikia nafasi ya Makamu wa Rais, Ndejembi amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na katika sekta binafsi, akieleza kuwa uzoefu huo utakuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

“Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi, kabla ya wadhifa huu, ulishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi. Sina shaka kwamba uzoefu huo utakusaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hii uliyopewa,” amesema Rais Samia.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hakuna shule maalumu inayomwandaa mtu kuwa Makamu wa Rais, bali uwezo wa kutekeleza majukumu hayo unajengwa kupitia sifa binafsi, bidii, weledi, nidhamu pamoja na utayari wa kujifunza na kusimamia utekelezaji wa majukumu.

Amesema sifa hizo zitamsaidia Ndejembi kutekeleza ipasavyo dhamana aliyopewa na taifa.

Rais Samia pia amesema uzoefu wa Ndejembi ndio uliowafanya viongozi kutokuwa na kusita katika kupitisha jina lake wakati wa kutafuta mtu wa kujaza nafasi hiyo.

“Kwa uzoefu huo ndio maana wakati tunatafuta mtu wa kujaza nafasi hii, hatukusita hata kidogo kupitisha jina lako. Hivyo ni matamanio na matarajio yetu sote Watanzania utalitumikia vyema, kwa utii, uaminifu, utu, busara, uzalendo, hekima, maarifa na uzoefu ulio nao, ukimtanguliza Mungu mbele na kwa maslahi ya taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amemtaka Ndejembi kwenda kuwatumikia Watanzania wote bila kujali tofauti zao, akisisitiza umuhimu wa kiongozi kuweka mbele maslahi ya taifa.

“Nenda ukawatumikie Watanzania bila kujali tofauti zao,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema serikali ina kazi kubwa ya kutekeleza ahadi zilizowekwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, sambamba na kuanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Amesema dira hiyo imebeba matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi, hivyo utekelezaji wake unahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora.

“Ili tuweze kutekeleza haya yote kwa maslahi ya wananchi wetu na taifa kwa ujumla, tunahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora,” amesema.

Uapisho wa Ndejembi unafungua rasmi ukurasa mpya katika safari yake ya uongozi wa kitaifa, huku akianza kutekeleza majukumu ya Makamu wa Rais chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan
















WANANCHI MATONGO NA NYANGOTO KUELIMISHWA KUHUSU UTHAMINI WA FIDIA NORTH MARA


NYAMONGO, MARA

Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, kupitia wataalamu kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, imefanya kikao na Kampuni ya Barrick North Mara Gold Mine pamoja na viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto, kwa lengo la kujadili maandalizi ya utoaji elimu kwa wananchi kuhusu zoezi la uthamini wa fidia linalohusishwa na upanuzi wa shughuli za Mgodi wa North Mara.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Diwani wa Kata ya Matongo, Mhe. Godfrey Mwita, amewataka viongozi wa Vijiji vya Matongo na Nyangoto kushirikiana kwa karibu na wataalamu pamoja na wadau wote wanaohusika katika mchakato huo, akieleza kuwa wananchi wa maeneo hayo wanatarajiwa kuguswa na upanuzi wa shughuli za mgodi.

Kwa upande wake, Meneja wa Mahusiano wa Kampuni ya Barrick, Bw. Francis Uhadi, amesema kampuni hiyo iko tayari kuanza mchakato huo kwa haraka, huku akisisitiza dhamira ya kampuni kuhakikisha haki na maslahi ya wananchi yanazingatiwa na kulindwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.

Akifafanua hatua zinazofuata, Mthamini Kiongozi kutoka Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, FRV. Baraka D. Mollel, amesema kikao hicho ni sehemu ya hatua muhimu kuelekea kuanza mchakato wa uthamini, baada ya hatua za awali zilizofanyika kwa kushirikisha Wizara ya Madini, ikiwemo tafiti na maandalizi mbalimbali.

Amesema hatua hizo zinalenga kuhakikisha zoezi la uthamini linafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, pamoja na kuwezesha wananchi kupata taarifa sahihi kuhusu mchakato huo.

Naye Mtunzaji wa Bwawa la Mgodi, Bw. Majuto Kipande, ameeleza kuwa, tafiti za awali zilizofanyika wakati wa uanzishwaji wa mgodi zilionesha kuwa shughuli za uzalishaji zingefikia ukomo mwaka 2027. Hata hivyo, amesema tafiti zinazoendelea hivi sasa zinaonesha uwezekano wa uzalishaji kuendelea hadi kati ya mwaka 2031 na 2040.

Kwa mujibu wa Kipande, hali hiyo imeongeza umuhimu wa upanuzi wa bwawa la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu kutokana na bwawa linalotumika sasa kutaraji kufikia ukomo wa matumizi mwaka 2031.

Ameongeza kuwa, ujenzi wa bwawa jipya la kutunza mabaki ya uchenjuaji wa dhahabu unapaswa kukamilika kabla ya mwaka 2031, ili kuwezesha shughuli za mgodi kuendelea bila kuathiriwa na ukomo wa uwezo wa bwawa linalotumika sasa.

Mchakato wa uthamini unalenga kuhakikisha wananchi watakaoguswa na eneo la upanuzi wanapatiwa elimu na taarifa sahihi kuhusu hatua zinazochukuliwa, huku zoezi la uthamini wa fidia likitekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu za nchi.



















Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...