Friday, May 29, 2026

MADIWANI WAASWA KUWA CHACHU YA MAENDELEO KISHAPU NA KUEPUKA MGONGANO WA MASLAHI

 Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga

Na Stella Herman,Shinyanga

Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Peter Masindi, amewataka madiwani kusimamia kwa umakini miradi ya maendeleo katika maeneo yao huku akisisitiza kuwa wao ndiyo wawakilishi wa wananchi na nguzo muhimu ya maendeleo ya Taifa.

Akizungumza  wakati wa mafunzo ya kuwajengea uwezo madiwani kuhusu kujiepusha na vitendo vya rushwa, kubaini mianya ya rushwa pamoja na kuwakumbusha maadili na wajibu wao, Masindi amesema viongozi hao wanapaswa kuwa chachu ya mabadiliko kwa kuwajibika ipasavyo katika maeneo wanayoyaongoza.

Amesema wananchi wanawategemea madiwani kuwasimamia na kuwawakilisha vizuri, hivyo wanapaswa kuangalia changamoto zilizopo katika kata zao na kuchukua hatua kwa wakati ili kuhakikisha maendeleo yanapatikana.

“Wananchi watawapima baada ya miaka mitano kwa kazi mtakazozifanya, Maendeleo ya kata yanawategemea ninyi, msipofanya maamuzi sahihi kata zenu haziwezi kupata maendeleo,” amesema Masindi.

Aidha amewataka madiwani kufanya kazi kwa kuzingatia maadili, nidhamu pamoja na kutunza siri za vikao na majukumu yao, akieleza kuwa dhamana waliyopewa ni kubwa ndiyo maana Serikali imeamua kutoa mafunzo hayo ili kuwakumbusha wajibu wao kwa wananchi.

Kwa upande wake, Mwendesha Mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu ambaye pia ni wakili  Maximilian Kyabona, amewaasa madiwani kujiepusha kutanguliza maslahi binafsi mbele na kusahau kuwa wao ni wawakilishi wa wananchi.

Kyabona amesema madiwani ndiyo watakaowezesha Halmashauri ya Kishapu kupata maendeleo iwapo watawajibika ipasavyo, kupinga rushwa na kufichua mianya yote inayoweza kusababisha miradi ya maendeleo kushindwa kutekelezwa.

Alitaja baadhi ya mambo ambayo madiwani wanapaswa kuyaepuka kuwa ni pamoja na kubadili vifungu vya matumizi ya fedha, kuchukuliana posho pamoja na kujihusisha na zabuni mbalimbali zinazoweza kuleta mgongano wa maslahi.


Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kishapu Josephat Limbe akizungumza wakati wa mafunzo kwa madiwani yaliyotolewa na TAKUKURU
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kishapu Atuganile Stephen akifuatilia mafunzo ya madiwani
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Peter Masindi akifungua mafunzo ya madiwani wa Halmashauri hiyo yakuwajengea uwezo katika masuala ya maadili,rushwa na kukumbushwa wajibu wao ambayo yametolewa na Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga

Mwendesha mashitaka wa TAKUKURU Mkoa wa Simiyu Maximilian Kyabona akitoa elimu ya masuala ya rushwa na maadili kwa madiwani wa Halmashauri ya Kishapu
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kishapu Josephat Limbe akizungumza wakati wa mafunzo kwa madiwani yaliyotolewa na TAKUKURU
Mkuu wa TAKUKURU Wilaya ya Kishapu Atuganile Stephen 
amesema mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha madiwani wajibu wao pamoja na suala la maadili katika kusimamia miradi na kujiepusha kutanguliza mbele maslahi yao binafsi badala ya kuwatumikia wananchi waliowachagua.

Thursday, May 28, 2026

Mkuu wa JKT awataka wahitimu kidato cha sita 2026 waliochaguliwa, kujiunga na mafunzo ya JKT kwenye makambi waliyopangiwa

 



Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa JKT Meja Jenerali Rajab Mabele amewataka Vijana waliohitimu kidato cha Sita kwa Mwaka 2026 ambao wamechaguliwa kujiunga na Mafunzo ya JKT kwa Mujibu wa sheria kujiunga na mafunzo hayo katika makambi waliyochaguliwa kuanzia juni mosi, hadi juni 7, 2026.

Akizungumza Wilayani Chamwino Mkaoni Dodoma kwa niaba ya Mkuu wa JKT, Mkuu wa Tawi la Utawala JKT Brigedia Jenerali Hassan Mabena amesema majina ya vijana wote waliohitimu kidato cha sita kwa Shule za Sekondari Tanzania Bara na Visiwani waliochaguliwa wanatakiwa kujiunga na mafunzo hayo.

Amesema orodha kamili ya majina ya vijana hao, makambi JKT waliyopangiwa, Maeneo ya Makambi hayo yalipo na vifaa wanavyotakiwa kwenda navyo inapatikana katika tovuti ya JKT ambayo ni www.jkt.mil.tz.



Amesema ilikufahamu kambi kijana aliyopangiwa atatakiwa kuingiza jina la shule au namba ya shule aliyohitimu kidato cha sita, mbele ya jina la shule ataona neno lililoandikwa waliochaguliwa ambapo akichagua neno hilo ataona majina ya waliochaguliwa kujiunga na mafunzo ya JKT kwa mujibu wa sheria kwa mwaka 2026 na kambi aliyopangiwa.

Amesema ili kuona majina yote ya vijana na kambi walizopangiwa mtumiaji atapakua JKT PDF 2026 iliyopo juu kulia katika ukurasa huo.

Ameongeza kuwa Mkuu wa JKT Meja Jenerali Rajabu Mabele anawakaribisha vijana wote waliohitimu kidato cha sita kwa mwaka 2026 ili waweze kujiunga na vijana wenzao katika kujengewa uzalendo, kufundishwa nidhamu, ukakamavu, umoja wa kitaifa, stadi za kazi, stadi za maisha na utayari wa kulijenga na kulitumikia taifa.

Katika hatua nyingine amebainisha kuwa kwa wahitimu wenye ulemavu wa kuonekana kwa macho wataripoti katika kambi ya Ruvu JKT iliyopo Mlandizi Mkoani Pwani ambayo ina miondombinu ya kuwahudumia watu hao.

Wednesday, May 27, 2026

HAKUNA NYONGEZA YA MUDA KWA MKANDARASI WA UJENZI WA BARABARA KAHAMA KUPITIA MRADI WA TACTIC - PROF. SHEMDOE

Na OWM - TAMISEMI, Kahama

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM-TAMISEMI) Mhe. Prof. Riziki Shemdoe amesema Serikali haitomuongezea muda Mkandarasi M/s China Civil Engineering Construction Corporation wa kukamilisha miradi ya ujenzi wa barabara na mitaro katika Manispaa ya Kahama, inayotekelezwa kupitia Mradi wa Uendelezaji Miundombinu ya Miji Tanzania (TACTIC) kwani ubovu wa miundombinu ya barabara imekuwa ni kero ya muda mrefu kwa wananchi wa manispaa hiyo.

Prof. Shemdoe amesema hayo leo Mei 27, 2026 Katika Manispaa ya Kahama wakati wa hafla ya Utiaji Saini wa Mkataba wa Umaliziaji wa Ujenzi wa Barabara na Mitaro kupitia Mradi wa TACTIC, iliyofanyika katika eneo la Phantom kwenye manispaa hiyo.  

“Ninamueelekeza Mkandarasi Kampuni ya M/s China Civil Engineering Construction Corporation kumaliza ujenzi ndani ya muda ulioanishwa katika mkataba ambao wameusaini leo, hakutakuwa na nyongeza ya muda,” amesisitiza Prof. Shemdoe.

Sanjari na hilo, Prof. Shemdoe amemtaka Mtaalamu Mshauri kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama  pamoja na TARURA katika kuhakikisha mikataba iliyosainiwa inatekelezwa kikamilifu na  inakamilika ndani ya muda uliopangwa na kwa ubora uliokubalika ili thamani ya fedha ionekane.

Prof. Shemdoe ameanisha kuwa Mei 27, 2026 imekuwa ni siku yenye furaha kwani kitendo cha kusainiwa kwa mikataba hiyo kinasadifu nia ya dhati ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwaboreshea miundombinu ya barabara wananchi wa Kahama, na kuongeza kuwa kama lilivyo jina lake amekuwa ni suluhu ya changamoto iliyokuwa ikiwakabili wananchi wa Manispaa ya Kahama.

“Tumeshuhudia utiaji saini wa mradi huu mkubwa wa zaidi ya Shilingi Bilioni 25 ambazo Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameridhia zitumike kujenga miundombinu ya barabara katika Manispaa ya Kahama, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2025 hivyo tunamshukuru sana na kumuahidi kwamba ofisi yangu itasasimamia kikamilifu utekelezaji wa mkataba huo,” amesema Prof. Shemdoe.

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita amesema Manispaa ya Kahama inatekeleza mradi wa TACTIC kwa awamu mbili, awamu ya kwanza inahusisha ujenzi wa barabara za katikati ya mji (Central Business District (CBD) zenye urefu wa Kilomita 12.3 na barabara ya eneo la Zongomela kilomita tatu (3)  pamoja na ujenzi wa  mfereji wa maji ya mvua wa Chelsea – Lyazungu,  Shunu – Magobeko (Standalone Storm Water Drain).

Mhe. Mhita amesema kwamba, awamu ya pili ya utekelezaji wa mradi wa TACTIC katika Manispaa ya Kahama utahusisha ujenzi wa kituo cha mabasi Mbulu (Mbulu Bus Terminal), Soko la Sango (Sango Market) na Kituo kidogo cha mabasi cha Zongomela (Zongomela Mini Bus Stand).

Naye, Mratibu wa Miradi ya Ushirikiano na Benki ya Dunia  Mhandisi Humprey Kanyenye wa TARURA amesema kuwa, Mkandarasi  ambaye ni Kampuni ya M/s China Civil Engineering Construction Corporation anakwenda kutekeleza mradi huu katika Manispaa ya Kahama kwa gharama ya Shilingi za kitanzania Bilioni  25,547,162,432.04 bila VAT, na utatekelezwa kwa muda wa miezi nane (8) kuanzia  Juni 01, 2026 hadi Januari 31, 2027.















BARRICK NORTH MARA YAZINDUA KLINIKI AWAMU YA PILI YA UTATUZI WA MIGOGORO VIJIJI 11 VINAVYOZUNGUKA MGODI

Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele, akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa kliniki ya kusikiliza na kushughulikia malalamiko ya wananchi dhidi ya Mgodi wa Barrick North Mara.
Meneja wa Idara ya Mahusiano ya Mgodi wa Dhahabu wa Barrick North Mara, Francis Uhadi, akizungumza wakati wa uzinduzi wa kliniki hiyo.
Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Meja Edward Gowele na viongozi wa Barrick wakiwa katika picha ya pamoja na wadau wengine baada ya uzinduzi wa awamu ya pili ya Kiliniki ya Kusikiliza na Kushughulikia Malalamiko ya Wananchi.

****
Mgodi wa Barrick North Mara umezindua kliniki ya awamu ya pili maalum ya kusikiliza malalamiko , kero na migogoro ya wananchi ili kupata utatuzi wa kudumu kwenye vijiji 11 vinavyozunguka mgodi huo kwa ajili ya kuendelea kuboresha mahusiano kati ya mgodi na jamii.


Kliniki hiyo ya malalamiko inatoa fursa ya kuwakutanisha wananchi wanaozunguka mgodi huo na kutoa nafasi ya majadiliano ya kina, uwazi, kuboresha mahusiano ya kuaminiana na uwajibikaji kati ya jamii, mgodi na serikali na kuhakikisha malalamiko yanachukuliwa, yanapitiwa , kuweka kwenye kumbukumbu na hatimaye kushughulikiwa.

Kliniki hiyo inayojumuisha wajumbe kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Mgodi wa Barrick North Mara, Tume ya Haki za binadamu na utawala wa bora , asasi za kiraia- mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja na wadau wengine, inalenga kuimarisha mahusiano kati ya mgodi na wananchi wa vijiji vinavyozunguka eneo hilo ili kuwezesha uwekezaji endelevu wenye maslahi mapana kwa wilaya , Mkoa na taifa kwa ujumla.

Akizungumza kwenye uzinduzi wa kliniki hiyo ya pili katika kijiji cha Mjini Kati kilichopo Nyamongo, Wilayani Tarime, Mkuu wa Wilaya hiyo, Meja Edward Gowele alisema hatua hiyo itasaidia kupunguza na hatimaye kumaliza malalamiko na migogoro kati ya mgodi na jamii inayozunguka mgodi huo.

“Niupongeze mgodi wa Barrick North Mara kwa kufanya kliniki kwa awamu ya pili ni hatua kubwa na ni matumiani yangu kuwa itapunguza malalamiko na migogoro. Ili kujenga jamii ya amani na utulivu lazima tusikilizane na kutatua migogoro iliyopo,” alisema.

Meja Gowele alitumia nafasi hiyo pia kutoa wito kwa wanavijiji kujitokeza kuwasilisha malalamiko yao kwenye kliniki hiyo ili yapatiwe utatuzi kwa maendeleo na ustawi wa pande zote mbili.

Aidha, aliitaka kamati ya kliniki hiyo na viongozi wa vijiji kuhakikisha wananchi wanapata taarifa kwa wakati kuhusu mikutano ya kusikiliza na kupokea malalamiko yao itakayofanyika katika kila kijiji.

“Nimezindua rasmi kliniki hii, ipite kila kijiji na kusikiliza kila mwananchi mwenye malalamiko bila ubaguzi wala upendeleo,” Meja Gowele alisisitiza.

Ili kuongeza uwazi, uwajibikaji na ushiriki mpana wa wadau wote, klinki hiyo ina kamati inayojumuisha wafanyakazi wa mgodi, madawati ya malalamiko kutoka ofisi za Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, asasi za kiraia na wawakilishi wa jamii.

Gowele alisisitiza kwamba kwa watu waliopo ndani ya eneo la leseni ya Barrick North Mara kutii sheria bila shuruti na kuondoka ili kutokwamisha shughuli za mgodi huo.

Pamoja na mambo mengine , Mkuu wa Wilaya hiyo aliwataka watendaji wa Halmashauri ya Tarime kutoa ushirikiano kwenye miradi ya kimkakati katika wilaya hiyo ikiwemo ujenzi wa soko la dhahabu la Nyamongo na ujenzi wa stendi ya kisasa ya Nyamwaga.

“Nimeelezwa kwamba ili miradi hiyo iweze kuendelea ni lazima hati za maeneo husika zipatikane kwa wakati, watendaji hakikisheni unakamilisha taratibu zote zinazohitajika bila kuchelewesha maendeleo” , aliongeza.

Alisisitiza kwamba kukamilika kwa miradi hiyo ni hatua muhimu yenye kutia matumaini na kuongeza mahusiano mazuri kati ya wananchi na mgodi.

Akizungumza kwenye uzinduzi rasmi wa kliniki hiyo Mkoa Mara , Wilaya ya Tarime, Tarafa ya Nyamongo , Meneja Uhusiano wa Jamii wa Mgodi wa Barrick North Mara, Franscis Uhadi alisema kwamba mahusiano kati ya mgodi na wananchi umezidi kuimarika ila bado kuna changamoto ambazo zinahitaji utatuzi wa kudumu ili kurahisisiha shughuli za uchimbaji na kuboresha mahitaji ya wananchi kupitia sheria na kanuni ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Alisema kwamba moja ya changamoto inayoendelea kujitokeza ni malipo ya fidia kwa wananchi akisema kwamba baadhi ya wananchi kwenye jamii kuendelea kugoma malipo ya fidia kwa kudai kwamba hajaridhishwa.

“Wananchi 728 walifanyiwa tathimini katika eneo la Nyabirama na malipo yao yapo tayari , kati yao 667 wamepokea fidia na kupisha shughuli za mgodi huku 61 wakiendelea kusubiri ambapo watu 44 ni wa familia moja,” alisema Uhadi.

Uhadi alisema kwamba mgodi wa umeendelea kutekeleza miradi ya jamii kupitia kanuni na sheria za Uwajibikaji kwa Jamii (CSR) ambapo miradi 103 imepagwa kutekelezwa mwaka huu na huku 70 ikiwa tayari imekamilika na mengine ikiwa kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji.

Alisema kwamba kliniki hiyo itazunguka kwenye vijiji vyote 11 vinavyozunguka mgodi huo ili kuwafikia wananchi moja kwa moja na kuweza kutatua changamoto zao moja kwa moja.

Kwa upande wake, Mwenyekiti mpya wa Kamati ya Maendeleo ya Jamii (CDC) katika mgodi wa Barrick North Mara, Bogomba Rashid, alisema hatua hiyo ya kusikiliza na kutatua migogoro itasaidia pia kuharakisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika vijiji vinavyozunguka mgodi huo.

“Tukimaliza migogoro ambayo haina sababu ya kuwepo tutaendelea kufanya shughuli za maendeleo zaidi katika maeneo yetu,” alisema Bogomba ambaye pia ni Diwani wa Kata ya Kemambo.

Baadhi ya wananchi waliohudhuria shughuli hiyo ya uzinduzi wa kliniki walipongeza hatua hiyo ya mgodi wa Barrick North Mara kwa sababu itapunguza migogoro na kupanua wigo wa ushirikiano na kukuza mahusiano kati ya mgodi na jamii.

Mkazi wa Kijiji cha Kewanja , Mwita Omahe alisema kwamba pamoja na kuimarika kwa mahusiano kati ya jamii na mgodi ila bado kuna changamoto ya barabara mbovu za mitaa ambazo zinahitaji kushughulikiwa.

Katika awamu ya kwanza ya kliniki hiyo iliweza kuwafikia wananchi zaidi ya 1,688 na kero zilizopokelewa zilikuwa 137.

Vijiji vinavyozuguka mgodi huo ambavyo vitanufaika na kliniki hiyo ya wiki moja ni Mjini kati, Nyangoto, Kewanja, Matongo, Nyabichune, Kerende, Nyakunguru, komarera, Genkuru, Msege na Nyamwaga.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...