Tuesday, September 30, 2025

RAIS SAMIA ALETA MWANGA WA ELIMU KWENYE VIJIJI KAHAMA

 

Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu akimshukuru Rais Samia kwa kuiwezesha Manispaa ya Kahama kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo ya elimu

Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari ya Amali Lowa

Na Neema Nkumbi – Kahama


Ni sauti zilizobeba furaha na shukrani, Sauti za baraka baada ya wananchi wa Kahama kuhakikishiwa kesho yenye mwanga wa elimu bora na mafanikio.


Hii ni ishara ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuwaletea wananchi maendeleo.


Katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, utekelezaji wa ilani umejidhihirisha katika sekta za Elimu, Afya, Maji, Barabara, Masoko, Nishati pamoja na utoaji wa mikopo kwa Vijana, Wanawake na Wenye Ulemavu.


Sekta ya Elimu: Ndoto zinazotimia


Moja ya mafanikio makubwa ni ujenzi wa shule mpya, zikiwemo Shule ya Sekondari Amali Lowa na Wendele, zilizopunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kufuata elimu.


Shija Butemi, mwanafunzi wa Amali Lowa, anakumbuka changamoto walizopitia kabla ya shule hiyo kujengwa:


"Mwanzoni tulisoma Sekondari ya Nyandekwa, Tulikuwa tunapata tabu kubwa, hasa sisi wasichana, Mara nyingi tulitembea kwa miguu, na wakati mwingine tulilazimika kuomba msaada kwa bodaboda ambao walituuliza 'mnatupa nini?' Hali hii ilisababisha baadhi ya wenzetu kushawishika vibaya na kuishia kupata mimba, Tunamshukuru Rais Samia kwa kutujengea shule ya karibu, sasa tunafika mapema na masomo yamekuwa rahisi."


Kephline Ezekiel, mwanafunzi wa Sekondari ya Wendele, anaongeza:


"Awali tulikuwa tukisafiri kutoka kijiji cha Tumaini hadi Sekondari ya Ngogwa, umbali mrefu uliotusababisha uchovu na kushuka ufaulu, Shule hii mpya imetupunguzia changamoto hizo, Naomba wazazi waache kuwazuia watoto wao waende shule; elimu ndiyo urithi wa kweli."


Shija Bundala, mwanafunzi mwingine wa Amali Lowa, pia anawataka wenzake walioacha shule kwa sababu ya umbali warejee sasa kwa kuwa shule ipo jirani.


Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Shule ya Amali Lowa, Mwalimu Ezekia Ngabo, anasema shule hiyo ilianza rasmi Julai 28, 2025 ikiwa na wanafunzi 47 (wavulana 13 na wasichana 34) na walimu 9 pamoja na mlinzi mmoja.




"Shule hii ina mikondo miwili: wa jumla na wa amali (elimu ya vitendo), Kupitia mkondo wa amali, hasa somo la kilimo, tunawajengea wanafunzi stadi za maisha zitakazowawezesha kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji."




Mtazamo wa Viongozi


Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu, anabainisha kuwa mafanikio haya ni matunda ya ushirikiano kati ya Serikali Kuu na Halmashauri:




"Tunamshukuru Rais Samia kwa kutuwekea mazingira bora ya ukusanyaji mapato na kutupatia fedha za maendeleo. Tulipokea zaidi ya shilingi bilioni 1.2 kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za Wendele na Amali Lowa, zikiwa na madarasa, jengo la utawala, maabara na vyoo, Ujenzi umekamilika na wanafunzi wameanza kusoma, Huu ni ushahidi wa dhamira ya serikali kuwekeza kwenye elimu bora."


Masudi ameongeza kuwa miradi mingine ya maendeleo katika sekta za afya, barabara na maji imeendelea kuipamba Manispaa ya Kahama, na kuimarisha ustawi wa wananchi.


Hitimisho


Wananchi wa Kahama sasa wananufaika moja kwa moja na miradi ya elimu, afya, na miundombinu, matunda ya Ilani ya CCM na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita.


Changamoto bado zipo, kama vile mahitaji ya walimu na vifaa vya kisasa vya kujifunzia, lakini matumaini yamejengeka, Ndoto za watoto wa vijijini kupata elimu bora sasa zinageuka kuwa uhalisia.


Jitokeze kushiriki Uchaguzi Mkuu wa 2025 kwa amani na utulivu ili miradi ya maendeleo iendelee.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu akimshukuru Rais Samia kwa kuiwezesha Manispaa ya Kahama kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo ya elimu
Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari ya Amali Lowa
Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari Wendele
Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani
Shija Butemi mwanafunzi wa Amali Lowa, akiishukuru selikali ya Rais Samia kwa kuwajengea shule karibu na maeneo ya nyumbani kwao
Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani

Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani

Source

CMSA Yaipongeza Tanga Saruji kuzindua Mauzo ya Hisa Stahiki za Bilioni 204

Kampuni ya Tanga Saruji imeweka historia mpya katika masoko ya mitaji nchini Tanzania kwa kuzindua rasmi mauzo ya Hisa Stahiki zenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 204. Hii ni mara ya kwanza kwa kampuni nchini kutoa hisa stahiki za thamani kubwa kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), hatua inayotajwa kuwa ya kimkakati katika kuimarisha uwekezaji na kuongeza thamani kwa wanahisa.


Akizungumza katika uzinduzi huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama aliipongeza Bodi na Menejimenti ya Kampuni ya Saruji Tanga kwa uongozi thabiti, ujasiri na maono ya kimkakati yaliyopelekea mageuzi makubwa ya kiutendaji ndani ya kampuni hiyo.

"CMSA tunaridhishwa na hatua za mabadiliko ya kimkakati yanayoendelea katika kampuni hii, ikiwa ni pamoja na kupunguza mikopo ya kigeni, kuongeza mapato na faida ya kampuni, na kutoa fursa zaidi za uwekezaji kwa wananchi," alisema CPA Mkama

Hisa hizi stahiki zinauzwa kwa wanahisa wa sasa wa Kampuni ya Tanga Saruji kwa bei ya shilingi 1,600 kwa hisa moja, ambayo ni punguzo la asilimia 38.2 ukilinganisha na bei ya soko ya shilingi 2,590 kwa hisa moja. Kiasi cha hisa kinachotolewa ni 127,342,090, katika uwiano wa hisa mbili kwa kila hisa moja anayomiliki mwekezaji kwa sasa.

Aidha Utoaji huo wa hisa umetajwa kuwa umekidhi kikamilifu matakwa ya Sheria ya Masoko ya Mitaji na Dhamana, Sura ya 79 ya Sheria za Tanzania pamoja na Kanuni zake, baada ya kupokea idhini rasmi kutoka CMSA.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, ongezeko la thamani ya hisa za Kampuni ya Saruji Tanga limekuwa kubwa kwa kipindi cha muda mrefu – kutoka shilingi 300 mwaka 2002 hadi shilingi 2,590 kwa hisa moja mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 763.3.

"Tunaipongeza Kampuni ya Tanga Saruji  kwa mafanikio haya makubwa. Hili ni somo na mfano kwa kampuni nyingine zilizo orodheshwa katika soko la hisa kuendelea kuboresha ufanisi na utawala bora," aliongeza CPA Mkama.

Aidha, alieleza kuwa mafanikio ya Tanga Cement  ni uthibitisho wa nafasi muhimu ya masoko ya mitaji katika kukuza uchumi wa Taifa, kwa kutoa mitaji ya muda mrefu kwa kampuni, kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhamasisha umiliki wa pamoja wa rasilimali za uzalishaji.

Pia CPA Mkama amesisitiza kuwa mafanikio hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (TDV 2050), ambayo inalenga kuifikisha Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati wa juu na kufikia Pato la Taifa la Dola Trilioni 1 ifikapo mwaka 2050.

Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) pia imepongeza wadau waliohusika katika mchakato wa maandalizi ya Waraka wa Matarajio, akiwemo mshauri kiongozi wa kifedha iTrust Finance Limited, Mshauri wa Kisheria Joachim & Jacobs Attorneys, pamoja na wakaguzi Deloitte & Touche, kwa weledi wao mkubwa uliofanikisha hatua hii muhimu.

Mchakato wa mauzo ya hisa hizo unatarajiwa kufungwa Oktoba 24, 2025, na wanahisa wametakiwa kuchangamkia fursa hiyo adhimu ya kuongeza uwekezaji wao kwa bei ya punguzo.

"Napenda kutoa wito kwa wanahisa wote kutumia fursa hii kununua hisa stahiki, ili kuimarisha uwekezaji wao na kuwa sehemu ya mafanikio endelevu ya kampuni hii ya kihistoria," aliongeza

CPA Mkama pia amezitaka kampuni nyingine katika sekta binafsi na umma kutumia kikamilifu masoko ya mitaji kama chanzo mbadala cha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, badala ya kutegemea mikopo ya gharama kubwa.

 








Friday, September 19, 2025

MWANA FA KUSHUGHULIKIA MAWASILIANO YA SIMU JIMBO LA MUHEZA





Na Mwandishi Wetu, Muheza

MGOMBEA ubunge Jimbo la Muheza kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Hamis Mwinjuma maarufu MwanaFA amesema katika miaka mitano ijayo atahakikisha anaongeza minara ya simu ili Jimbo la Muheza liweze kuwa na mawasiliano katika maeneo ambayo yana changamoto hiyo.


Akizungumza katika mkutano wa kampeni uliofanyika katika kata ya Kwezitu tarafa ya Amani, MwanaFA alikiri kwamba yapo maeneo katika Jimbo hilo, yana changamoto ya ukosefu wa mawasiliano.



"Katika miaka mitano ijayo tutaimarisha mawasiliano ya simu...Moja ya mambo yanayonisikitisha ni kufika baadhi ya maeneo kwenye Jimbo la Muheza ikawa simu haiwezi kushika mawasiliano, huwezi kupigiwa simu," alisema na kuongeza,

"Tunachotaka kufanya ni kuhakikisha tunaongeza minara ya simu ili kuongeza kiwango cha upatikanaji wa mawasiliano kwa wananchi wetu,".



MwanaFA ambaye ni Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, alisema kuwa katika kipindi cha mwaka 2020-2025 Jimbo hilo lilipata minara Saba ambayo kutokana na jiografia ya Jimbo hilo, bado haijakidhi mahitaji ya mawasiliano katika maeneo mengi kutokana na hali hiyo.

Hivyo, alisema anakwenda kuzifanyia kazi kuhakikisha minara ya simu inaongezeka na hali ya mawasiliano inazidi kuimarika katika Jimbo hilo.



"Sitaki kuahidi mambo mengi na nikashindwa kuyatekeleza lakini niwahakikishie jambo moja changamoto zote za kata ya Kwezitu, Jimbo la Muheza kwangu ni kipaumbele...Miaka mitano hii nimejua kona zote za kutatua changamoto zilizopo katika Jimbo letu," alisema.

Aliwaomba wananchi wa Kwezitu kufanya kazi mbili ambazo ni kwenda kupiga kura Oktoba 29 na kuwachagua wagombea wa CCM ili waweze kumalizia kazi ambazo wamezifanya katika miaka mitano iliyopita.



Alisema wananchi wa Kwezitu wanakila sababu za kumchagua Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwakuwa ameleta fedha nyingi katika kata hiyo na Jimbo zima la Muheza.

Rais ameleta fedha nyingi katika miradi ya afya, elimu, maji, barabara na miradi mingine hivyo anastahili kupigiwa kura nyingi katika Jimbo letu.

"Nichagueni na Mimi miaka mitano hii nimeisema wilaya hii, hatuwezi kusema matatizo yetu yote tumeyamaliza bali dhamira yetu ni ya dhati kwakuwa kila sekta tumeigusa," alisema na kuwaomba wananchi wa kata hiyo kumchagua Mch. John Mzalia awe diwani wa kata hiyo.



Akiomba kura kwa wananchi wa kata hiyo Mgombea udiwani Mch Mzalia alisema kuwa kata hiyo imepata miradi mingi kuliko wakati wowote ule ikiwemo miradi ya Elimu, afya, barabara na huduma za jamii.

"Tumepata mradi wa Boost ambao shule yetu ya Kwezitu imekuwa nzuri mno hadi watoto wetu wanasoma kwenye shule ya vioo wakati mwingine wanachungulia kwenye madirisha hayo kama watoto wa Kihindi," alisema na kuwaomba wananchi hao wawachague wagombea wa CCM.

Katibu wa CCM wilaya ya Muheza Simon Leng'ese amewataka viongozi wa CCM wa ngazi zote za kata hiyo kuhakikisha wanatoka na kwenda kwa wananchi kuomba kura za wagombea wa CCM ili kukifanya chama hicho wagombea wake kupata kura za kishindo.



"Viongozi wa kata, matawi, mashina, mabalozi mtoke kwenda kuomba kura kwa wananchi katika maeneo yenu, haya ni maagizo nawapa mwende kukifanya chama chetu na wagombea wetu waweze kupata kura nyingi," alisema Leng'ese.

Meneja wa kampeni wa mgombea wa Jimbo la Muheza Aziza Mshakang'oto ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM wilaya ya Muheza (UVCCM), amewataka wananchi wa kata ya Kwezitu wasifanye makosa kwa kuwachagua wagombea wa upinzani kwakuwa hawana jipya.

Alisema CCM imekuja na ilani ambayo kwa wilaya ya Muheza imekuwa na miradi mingi ya maendeleo katika Jimbo hilo hivyo wasifanye makosa katika uchaguzi huo.

Mwisho

Thursday, September 18, 2025

SERIKALI YA AUSTRIA KUFADHILI MIRADI YA UMEME TANZANIA




📌 Ni inayozalisha umeme kutokana na Jua; Takataka

📌 Ufadhili huo ni kupitia Benki ya UniCredit ya Austria

📌 Serikali ya Tanzania yaahidi ushirikiano

Serikali ya Austria kupitia Benki ya UniCredit  imeahidi kuipatia fedha Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kiasi cha Euro Milioni 20 sawa na takribani Shilingi bilioni 60 kwa ajili ya Utekelezaji wa miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia jua na takataka.

Hayo yamesemwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Merl Solar Technologies GmbH, Mha. Hannnes Merl alipofanya mazungumzo na Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Mha. Felchesmi Mramba Septemba 17, 2025 pembeni ya  Mkutano Mkuu wa 69 wa Shirika la Kimataifa la nguvu za Atomic unaoendela Jijini Vienna, Austria.

Ili kuanza utekelezaji wa miradi hiyo, Mhandisi Mramba  ameikaribisha kampuni hiyo nchini Tanzania ili kukutana na wataalam na kuanza  kufanya maandilizi stahiki ya miradi hiyo mipya ya kuzalisha umeme  huku akiahidi kutoa ushirikiano katika kufanikisha Utekelezaji wa miradi hiyo.

Mha. Felchesmi Mramba ameeleza kuwa kampuni ya Merl  imeshatekeleza miradi mbalimbali ya umeme wa jua nchini akisema "kampuni hii imetekeleza  miradi ya umeme katika vijiji kumi (10) katika kipindi cha mwaka 2015 hadi 2017".

Ametaja miradi hiyo kuwa  ni ya makontena 14 ya kuzalisha umeme kwa kutumia nishati ya jua katika Wilaya za Kongwa  mkoani Dodoma, Mlele mkoani Katavi, pamoja na Uyui mkoani Tabora ambapo mradi huo uligharimu kiasi cha  shilingi bilioni 16.2.

Ameongeza kuwa miradi hiyo imewezdsha kuzipatia umeme nyumba na makazi 812, nyumba za Ibada 27, Shule 6 na Vituo vya Afya 8.

Mha. Mramba ameishukuru Serikali ya Austria kwa kutekeleza miradi hiyo kwa ufanisi pamoja na nia ya Serikali ya Austria kuendeleza ushirikiano na Serikali ya Tanzania katika utekelezaji wa Mkakati Mahususi wa Nishati (National Energy Compact) unaolenga kupeleka umeme kwa watanzania wote ifikapo mwaka 2030 kupitia mpango wa misheni 300.
 
Kikao kati ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Kampuni ya Merl kimefanyika 
 katika Ofisi za Ubalozi wa Tanzania Mjini Vienna nchini Austria na kuhudhuriwa na Balozi wa Tanzania na Mwakilishi wa Kudumu nchini Austria Balozi. Naimi S. Aziz pamoja na Kamishna wa Umeme na Nishati Jadidifu,  Mha. Innocent Luoga.

Tuesday, September 9, 2025

Ajali ya Malori Kona ya Sigino Yaendelea Kugharimu Maisha


Na John Walter-Babati

Kona ya Sigino, maarufu kwa kuwa tishio kwa madereva wa magari ya mizigo, imeendelea kuwa chanzo cha maafa baada ya ajali mbaya kutokea tena alfajiri ya Septemba 8, 2025.

Tukio hilo limetokea majira ya saa sita usiku, ambapo gari aina ya Scania lenye namba za usajili T 859 ASR lililokuwa limebeba mazao mbalimbali ikiwemo mahindi, mbaazi na dengu, lilishindwa kudhibiti mwendo na kupinduka katika Kijiji cha Sigino, wilayani Babati, mkoani Manyara. 

Gari hilo lilikuwa likitokea Wilaya ya Hanang' kuelekea mkoani Arusha.

Kwa mujibu wa taarifa za Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara, Dkt. Mathias Kimaro, walipokea mwili wa mwanaume mmoja aliyefariki dunia pamoja na majeruhi wawili wanaume, ambao hali zao zinaendelea kuimarika.

Mwenyekiti wa Kitongoji cha Sigino Chini, Victor Mollel, amesema eneo hilo limekuwa likisababisha ajali mara kwa mara kutokana na kona kali na mteremko mkali, hasa kwa magari ya mizigo yanayopoteza breki. 

Ameiomba serikali kuweka vizuizi au kuchukua hatua madhubuti ili kuokoa maisha na mali za wananchi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Sigino, Manfred Sumaye, amesema makumi ya maisha yamepotea katika eneo hilo kwa miaka mingi, huku malalamiko ya wananchi yakipuuzwa na mamlaka husika. 

"Tumekuwa tukipeleka maombi yetu mara kwa mara, lakini hatua madhubuti bado hazijachukuliwa,  ajali ya jana imetokea majira ya saa sita usiku na imeacha simanzi kubwa," amesema Sumaye.

Miongoni mwa majeruhi wa ajali hiyo ni Faustin Nada, mkazi wa Alosabida aliyekuwa akisafiri kuelekea Arusha na mzigo huo. 

Zakayo Ibrahim mkazi wa Gehandu Hanang',  alieleza kuwa baada ya ajali alipigiwa simu na Faustin akiomba msaada, akaanza safari ya kuja Babati lakini alikuta akiokolewa na watu waliokuwa wakishirikiana na jeshi la Zimamoto na uokoaji majira ya saa 12 asubuhi akiwa hoi huku akidai ana njaa kali kwa sababu tangu jana hakuwa amekula.

Eneo la kuanzia Singu kuelekea Sigino linatajwa kuwa hatari zaidi kutokana na mteremko mkali na kona zinazohitaji uangalizi wa hali ya juu. 

Madereva wengi wa malori makubwa hutegemea breki za upepo ambazo mara nyingine hushindwa kufanya kazi, na kufikia daraja la Sigino ambapo maafa hutokea.

Licha ya mafunzo na maonyo kwa madereva, Kona ya Sigino imeendelea kuwa "mwiba mkali" kwa usalama barabarani – ikipoteza maisha ya watu, kuacha wengine na ulemavu wa kudumu, na kuisababishia jamii hasara kubwa kutokana na magari na mizigo kuharibika.


Sunday, September 7, 2025

DC MSANDO ARIDHISHWA UZALISHAJI MAJI RUVU JUU, ATOA MAAGIZO DAWASA.


Mkuu wa Wilaya ya Ubungo (DC), Mheshimiwa Albert Msando amefanya ziara katika mtambo wa uzalishaji maji Ruvu Juu kwa lengo la kuona na kujiridhisha hali ya uzalishaji wa maji katika mtambo huo ambao unahudumia sehemu kubwa ya Wilaya ya Ubungo.

Katika ziara yake hiyo aliyoambatana na Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Ubungo pamoja na watendaji wa DAWASA, DC Msando ameridhishwa na hali ya uzalishaji maji huku akitoa maagizo kwa DAWASA kutatua changamoto zilizopo kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji.

"Tumefika hapa Ruvu Juu na tumejiridhisha uzalishaji wa maji upo vizuri, tunafahamu kulikuwa na matengenezo yanaendelea na kusababisha baadhi ya maeneo kukosa maji tumeona matengenezo yamekamilika na huduma inarejea kwa wananchi," amesema Msando

Msando ametoa maagizo kwa watendaji wa DAWASA hasa waliopo Wilaya ya Ubungo kuhakikisha maji yanayozalishwa yanawafikia wananchi bila kikwazo na kutoa taarifa kwa wakati pale panapotokea changamoto yeyote ya huduma lakini zaidi wanaopata maji kwa migao wajue siku gani wanapata na ratiba hiyo isimamiwe bila kupindishwa.

"Nirudie kusema tena, swala la upotevu wa maji halikubaliki, Serikali inatumia gharama kubwa kuchakata maji haya mpaka yanapomfikia mteja uwekezaji huu lazima uthaminiwe na tusimamie vyema kila mwananchi apate maji," amesema Msando.

Meneja wa Mtambo wa uzalishaji maji Ruvu Juu, Mhandisi Juma Kasekwa amesema kwasasa hali ya uzalishaji imerejea katika hali ya kawaida na maeneo yaliyokuwa hayapati maji, huduma inaendelea kuimarika.

"Katika hali ya kuboresha uzalishaji maji katika mtambo wetu wa Ruvu Juu, Serikali imetupatia zaidi ya Shilingi bilioni 1 kununua pampu mbili mpya ambazo ni mategemeo yetu mpaka ifikapo mwezi Novemba tutakua tumezifunga na Kuongeza uzalishaji wa maji," amesema Kasekwa.
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...