Tuesday, August 28, 2018

Watumishi wa Umma Wapigwa Marufuku Kutumia Mitandao ya Kijamii


Serikali imezuia matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watumishi wa umma wakati wa kazi kwa madai yanaathiri kasi ya mtandao wa intaneti ya serikali, na kudai kuwa watumishi wengi wanapoteza muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii kuliko kutekeleza majukumu yao. 

Taarifa iliyotolewa leo na katibu mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Dkt. Laurean Ndumbaro kwa taasisi zote za umma, imeonya juu ya matumizi mabaya ya mitandao ya mawasiliano ya serikali na kwamba, hatua hiyo imelenga kudhibiti matumizi ya mitandao. 

"Kasi ya mtandao wa serikali inapungua kutokana na matumizi makubwa ya mitandao ya kijamii hususan inayopakua video, mfano 'YouTube' na hivyo kusababisha watumishi wengine wanaotumia mtandao wa intaneti wa Serikali katika kutekeleza majukumu yao kuathirika," imesema barua hiyo. 

Aidha,  Menejimenti ya Utumishi imezitaka taasisi zenye mahitaji maalumu ya matumizi ya mitandao ya kijamii wakati wa saa za kazi, kuwasilisha maombi yao kwa katibu mkuu wa utumishi yakiambatana na sababu za maombi hayo. 

Kwa mara kadhaa, serikali imekuwa ikitoa miongozo ya matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano kwa taasisi za serikali ikiwemo kukataza matumizi ya mitandao kupitia intaneti ya serikali muda wa kazi. 
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...