Diwani wa Madukani jijini Dodoma, Profesa Davis Mwamfupe amechaguliwa kuwa meya baada ya kupigiwa kura zote 54 kwenye kikao cha baraza la madiwani halmashauri ya Jiji la Dodoma.
Katibu tawala wilaya ya Dodoma Mjini, Michael Maganga amesema Profesa Mwamfupe ameshinda kwa asilimia 100 na kwamba katika uchaguzi huo hakuwa na mpinzani.
Kwa ushindi huo msomi huyo anaendelea na wadhifa huo ambao alikuwa nao miaka mitano iliyopita.
Emmanuel Chibago, diwani wa Matumbulu amechaguliwa kuwa naibu Meya wa halmashauri hiyo.
Kwa pamoja viongozi hao wameomba ushirikiano wakiahidi kutekeleza majukumu yao kwa watu wa itikadi zote.
