Tuesday, October 28, 2025

REA YAPELEKA NEEMA NANYAMBA


-Umeme waibua fursa za kiuchumi

-Wananchi waishukuru Serikali na kuahidi kutunza miundombinu ya umeme

Wananchi wa Kitongoji cha Nyundo; Kijiji cha Nyundo B katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba Mkoani Mtwara wameishukuru na kuipongeza Serikali kwa kuwawezesha kubadili maisha yao kupitia mradi wa umeme uliotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA).

Wametoa shukrani hizo kwa nyakati tofauti kijijini hapo wakati wa Kampeni ya uhamasishaji wa Matumizi ya Umeme kwa ajili ya shughuli za kiuchumi inayotekelezwa na REA katika maeneo mbalimbali Nchini.

"Tunaishukuru Serikali kwa kutufikishia umeme ambao umebadilisha maisha ya wananchi wa hapa; umeme umekuja na fursa nyingi na wananchi hususan vijana wameutumia kuanzisha shughuli mbalimbali za kujiongezea kipato," alipongeza Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyundo B, Hassan Shamte.

Alisema hapo awali wananchi walijishughulisha zaidi na kilimo lakini baada ya kufikishiwa umeme wamebuni miradi mbalimbali inayowaingizia mapato ikiwemo saluni, biashara za vinywaji na shughuli za uchomeleaji yaani welding.

Kwa nyakati tofauti wananchi walipongeza na walifafanua shughuli mbalimbali wanazofanya hivi sasa kwa kutumia umeme ambazo wamesema zimewakwamua kimaisha.

"Umeme umenipa manufaa maana kabla ya umeme changamoto za kimaisha zilikuwa nyingi lakini sasa hivi nina mashine zangu za kunyolea nywele na wateja ni wengi, kazi hii imeniongezea sana kipato," alisema Ramadhan Yusufu Mkazi wa Nyundo.

Naye Hamis Mgulaga fundi uchomeleaji kijijini hapo alisema kupitia umeme ameweza kuendesha maisha yake sambamba na kusaidia wengine katika familia yake kujikwamua kimaisha.

Juma Makoka mkazi wa kitongoji cha Nyundo alisema umeme umefanya awe mtu maarufu kijijini hapo kwa kuanzisha shughuli za kuingiza nyimbo katika simu za wateja wake, kazi ambayo huifanya mida ya mchana baada ya kutoka shamba na nyakati ambazo hakuna shughuli za shamba.

"Umeme unifanya niwe mtu wa kujishughulisha zaidi, hapo kabla nilikuwa nilitoka shamba ni kukaa tuu bila kazi lakini baada ya kufika umeme nikabuni hii kazi na inanisaidia kuendesha maisha," alisema Makoka.

Katika kampeni hiyo ya REA, Wananchi waliohudhuria waliahidi kuwa walinzi wa miundombinu ya umeme na kuwa mabalozi kwa wengine kuhusu kuutumia umeme kujiletea maendeleo

Tuesday, October 14, 2025

RIDHIWANI APONGEZA MAFANIKIO YA ILANI YA CCM, AWASIHI WANANCHI WA BWILINGU KUICHAGUA TENA 2025




13 Oktoba 2025

📍Kata ya Bwilingu – Mdaula, Msolwa na Chalinze Mzee

🌍 Wilaya ya Chalinze, Mkoa wa Pwani

🆕Mgombea Ubunge wa Jimbo la Chalinze kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, ameendelea na ziara zake za kampeni kwa kufanya mikutano ya hadhara na wananchi wa kata ya Bwilingu, akitembelea maeneo ya Mdaula, Msolwa na Chalinze Mzee. Ziara hii ni sehemu ya jitihada za kuomba ridhaa ya wananchi wa Chalinze ili CCM iendelee kuongoza serikali kwa kipindi cha mwaka 2025 hadi 2030.

Katika mikutano hiyo, Mheshimiwa Kikwete amewapongeza wananchi kwa moyo wa uzalendo na mshikamano waliouonyesha kwa Chama Cha Mapinduzi kwa kipindi chote, na amewaomba kuendelea kuamini katika chama chenye historia ya kutekeleza ahadi zake kwa vitendo.

Akizungumza mbele ya maelfu ya wakazi wa maeneo hayo, amesema kuwa mafanikio yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ni matunda ya utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020–2025, chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

"Katika miaka minne pekee, Rais Samia amedhihirisha kuwa ni kiongozi shupavu na jemedari wa maendeleo ya wananchi. Ametekeleza ilani ya uchaguzi kwa umahiri, uaminifu na weledi mkubwa katika sekta zote ikijumuisha afya, elimu, miundombinu, maji na huduma za kijamii," alisema Mheshimiwa Ridhiwani.

Amewahakikishia wananchi kuwa CCM itaendelea kuwa jibu sahihi kwa changamoto zao, akisisitiza kuwa chama hicho kina watu, sera na uzoefu wa kutatua matatizo ya wananchi kwa wakati na kwa ufanisi.

Pia amewakumbusha wananchi kuwa tarehe 29 Oktoba 2025 ni siku muhimu ya kufanya maamuzi ya kulinda na kuendeleza mafanikio yaliyopatikana, kwa kumpigia kura mgombea wa CCM wa nafasi ya urais, ubunge na udiwani, ili kuhakikisha ushindi mkubwa kwa Chama Cha Mapinduzi.

#KaziNaUtuTunasongaMbele
#ChalinzeYaMaendeleo
#IlaniImetekelezwa
#RidhiwaniNiChaguoSahihi
#SamiaNiTumainiJipya
#CCMKweliInatekeleza
#MaendeleoKwaVitendo
#ChalinzeMpya2025



Sunday, October 12, 2025

Serikali yazindua mfumo wa kielektoniki ukaguzi wa vyombo vya Moto.


Na John Walter-Babati

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Usalama Barabarani amezindua mfumo mpya wa kielektroniki wa ukaguzi wa vyombo vya moto na utoaji wa stika za usalama barabarani, hatua inayolenga kuimarisha usalama na kupunguza ajali barabarani

Uzinduzi huo umefanyika katika Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani mkoani Manyara Oktoba 11, 2025 ambapo mfumo huo unatarajiwa kuondoa changamoto zilizokuwa zikijitokeza katika ukaguzi wa magari kwa kutumia stika za karatasi, na badala yake kurahisisha huduma kwa njia ya Kidigitali.

Mwenyekiti wa Baraza hilo Mhe. Sillo amesema kuwa mfumo huo wa MIMIS ni sehemu ya mageuzi makubwa yanayotekelezwa na Jeshi la Polisi kupitia Idara ya Mifumo ili kuhakikisha vyombo vyote vya moto vinakuwa salama kabla ya kutembea barabarani.

"Kupitia mfumo wa MIMIS, wamiliki wa Magari wataweza kuomba ukaguzi, kulipia na kupata stika zao za kielektroniki kwa urahisi zaidi. Hii ni hatua kubwa kuelekea matumizi ya Teknolojia katika kuhakikisha usalama wa wananchi barabarani." Amesema Sillo

Ameongeza kuwa Mfumo wa MIMIS utamuwezesha mmiliki wa chombo cha moto kuomba huduma hiyo akiwa popote, kisha kupeleka chombo chake kwa wakaguzi waliopo katika ofisi za Wakuu wa Usalama Barabarani wa Mikoa (RTOs) au Wilaya (DTOs) kwa tarehe na muda atakaochagua mwenyewe.

Kwa upande wake Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani SACP William Mkonda amebainisha kuwa elimu kuhusu matumizi ya mfumo huu mpya tayari imeanza kutolewa kupitia vyombo mbalimbali vya habari na Askari wa kikosi cha Usalama barabarani 

"Tumejipanga kikamilifu kuhakikisha wananchi wanauelewa mfumo huu na wanatumia fursa hii kuimarisha usalama wa vyombo vyao". Amesema SACP Mkonda

Uzinduzi wa mfumo wa MIMIS umekuja sambamba na maadhimisho ya Wiki ya Nenda kwa Usalama Barabarani, ambayo hutoa nafasi ya kukumbushana umuhimu wa kufuata sheria za usalama barabarani, kutoa elimu kwa watumiaji wa barabara, na kufanya ukaguzi wa vyombo vya moto.

Friday, October 10, 2025

Mgombea wa CCM Mabibo atangaza neema rukuki


MGOMBEA Udiwani wa Kata ya Mabibo, wilayani Ubungo, jijini Dar es Salaam,  kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Ashura Mohammed  Seg'ondo, amewataka wananchi katika kata hiyo kujitokeza kwa wingi Oktoba 29 mwaka huu kumpigia kura Mgombea  Urais  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan na yeye kwa nafasi ya udiwani  ili kuwaletea maendeleo ya haraka.

Aidha amewataka kumchagua Mgombea Ubunge  kwa tiketi ya CCM  katikaJimbo la Ubungo Profesa Kitila Mkumbo  hali itakayo harakisha maendeleo katika kata hiyo.

 Akihutubia mkutano wa kampeni  katika kata hiyo,  Ashura alisema akichaguliwa  kipaumbele chake cha kwanza ni kuhakikisha  anasimamia kikamilifu  ujenzi wa miundo mbinu.

"Miundombinu nimeigawanya katika sehemu  mbili. Barabara kuu na barabara za ndani. Katika Mtaa wa Jitegemee  mkandarasi  tayari  anaendelea na ujenzi wa Barabara ya Binti Kayenga. Nami kwa kushirikiana na nyie nitahakikisha kwa ujasiri wangu mkubwa kwa nguvu zangu zote mkandarasi afanye kazi kwa haraka kukamilisha ujenzi,"ameeleza  Ashura.

 Amebainisha,   Kata ya Mabibo, imejaaliwa viwanda  vikubwa hivyo  kwa kushirikiana na viongozi atahakikisha  kwa asilimia kubwa  wakazi wa kata hiyo watananufaika na  ajira.

"Pia katika sekta ya michezo nitahakikisha  tunashirikiana vyema  ili iwe fursa ya ajira kwa sababu Kata ya Mabibo ni  ni kitovu cha mchezo wa  ngumi.  Bondia Mfaume Mfaume anatoka katika   kata hiii,"ameeleza.

Kuhusu mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri , Ashura ameeleza atahakikisha inawasikia walengwa.

"Mikopo inakuja lakini haiwanufaishi walengwa. Nikichaguliwa nitahakikisha mikopo hii inawafikia walengwa. Inawanufaisha wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Kausha damu itakuwa baibai,"ameeleza mgombea huyo.

Amesema atafanya jitihada kuleta walimu wa vikoba kutoa elimu  kwa wananchi katika kata hiyo ili viinue uchumi hasa wawanawake.






Friday, October 3, 2025

TAMASHA LA SIKU YA WANA 'STAND UNITED" NI KESHO JUMAMOSI CCM KAMBARAGE



Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro ambaye ni mlezi wa Timu ya Stand United akizungumza na waandishi wa habari.

Na Marco Maduhu,SHINYANGA


WANANCHI na mashabiki wa soka mkoani Shinyanga wametakiwa kujitokeza kwa wingi kesho, kushuhudia Tamasha la Siku ya Wana, litakalofanyika Uwanja wa CCM Kambarage, ambapo kutakuwa na utambulisho wa wachezaji wapya wa Timu ya Stand United watakaoshiriki Ligi ya Championship msimu huu.


Wito huo umetolewa leo Oktoba 3,2025 na Mlezi wa Timu ya Stand United Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro,wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea kwenye Tamasha hilo hapo kesho,ambalo litafanyika katika Uwanja wa CCM Kambarage.
"Natoa wito kwa wananchi wa Shinyanga na wapenzi wote wa soko wajitokeze kwa wingi hapo kesho kwenye Tamasha la siku ya wana ili kutoa Motisha kwa Timu yao ya Stand United, na kuishuhudia ikishuka dimbani dhidi ya Timu ya Pamba Jijiji katika mchezo wao wa kirafiki,"amesema Mtatiro.


Aidha,amesema katika msimu uliopita wa Ligi ya Champioship,ambapo Timu hiyo ili cheza Playoff ili kufuzu kushiriki Ligi kuu, kwamba wamejifunza mengi na msimu huu wa Championship timu ambazo watakutananazo ni kichapo tu sababu wamejipanga vizuri.
Msemaji wa Timu ya Stand United Ramadhan Zorro,amesema wamefanya usajiri mzuri na wachezaji wao wana viwango bora kabisa na kwamba kwa uwezo walio nao lazima watarejea kucheza Ligi kuu.


Amesema katika mchezo wao kesho dhidi ya Pamba Jijiji kwenye Tamasha hilo, wataonyesha uwezo wa wachezaji wao huku akiionya Pamba ijiandae kubeba mzigo wa magoli sababu wapo kamili.
Naye Msemaji wa Timu ya Pamba Jijiji Moses William,wamesema Timu ya Stand United ni nzuri na kwamba wamejipanga vyema kupata ushindi kwenye Tamasha hilo na hawatakuwa na mzaha.


Kwa upande wake Mwenyekiti wa Tamasha hilo Chripin Kakwaya,amesema maandalizi ya Tamasha hilo yanaendelea vizuri, na kwamba wakati wa Tamasha hilo kutakuwa na burudani mbalimbali ambapo wataanza na Jonging kilomita 5,Mbio za Baiskeli na Burudani kutoka wa Wasanii.
Amesema, pia kutakuwa na michezo ya utangulizi kati ya timu ya Bajaji na Bodaboda, Soko Kuu na Soko la Majengo pamoja na Dabi ya Upongoji FC na Ibinzamata, na baada ya hapo Timu ya Stand United itashuka dimbani dhidi ya Pamba Jiji.


Ameongeza katika Tamasha hilo kutakuwa na viingilio ambapo mzunguko sh.3,000,VIP Sh.5000 na VVIP sh.10,000.


TAZAMA PICHA👇👇


Mwenyekiti wa Tamasha la siku ya wana Chripin Kakwaya akizungumza na waandishi wa habari.
Msemaji wa Timu ya Stand United Ramadhan Zorro akizungumza na waandishi wa habari.
Msemaji wa Timu ya Pamba Jijiji Moses William akizungumzia mchezo wao wa kesho dhidi ya Stand United.
Msemaji wa Timu ya Pamba Jijiji Moses William(kushoto)wakipongezana na Msemaji wa Timu ya Stand United Ramadhan Zorro.

Tuesday, September 30, 2025

RAIS SAMIA ALETA MWANGA WA ELIMU KWENYE VIJIJI KAHAMA

 

Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu akimshukuru Rais Samia kwa kuiwezesha Manispaa ya Kahama kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo ya elimu

Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari ya Amali Lowa

Na Neema Nkumbi – Kahama


Ni sauti zilizobeba furaha na shukrani, Sauti za baraka baada ya wananchi wa Kahama kuhakikishiwa kesho yenye mwanga wa elimu bora na mafanikio.


Hii ni ishara ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) na dhamira ya dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kuwaletea wananchi maendeleo.


Katika Halmashauri ya Manispaa ya Kahama, utekelezaji wa ilani umejidhihirisha katika sekta za Elimu, Afya, Maji, Barabara, Masoko, Nishati pamoja na utoaji wa mikopo kwa Vijana, Wanawake na Wenye Ulemavu.


Sekta ya Elimu: Ndoto zinazotimia


Moja ya mafanikio makubwa ni ujenzi wa shule mpya, zikiwemo Shule ya Sekondari Amali Lowa na Wendele, zilizopunguza kwa kiasi kikubwa changamoto ya wanafunzi kusafiri umbali mrefu kufuata elimu.


Shija Butemi, mwanafunzi wa Amali Lowa, anakumbuka changamoto walizopitia kabla ya shule hiyo kujengwa:


"Mwanzoni tulisoma Sekondari ya Nyandekwa, Tulikuwa tunapata tabu kubwa, hasa sisi wasichana, Mara nyingi tulitembea kwa miguu, na wakati mwingine tulilazimika kuomba msaada kwa bodaboda ambao walituuliza 'mnatupa nini?' Hali hii ilisababisha baadhi ya wenzetu kushawishika vibaya na kuishia kupata mimba, Tunamshukuru Rais Samia kwa kutujengea shule ya karibu, sasa tunafika mapema na masomo yamekuwa rahisi."


Kephline Ezekiel, mwanafunzi wa Sekondari ya Wendele, anaongeza:


"Awali tulikuwa tukisafiri kutoka kijiji cha Tumaini hadi Sekondari ya Ngogwa, umbali mrefu uliotusababisha uchovu na kushuka ufaulu, Shule hii mpya imetupunguzia changamoto hizo, Naomba wazazi waache kuwazuia watoto wao waende shule; elimu ndiyo urithi wa kweli."


Shija Bundala, mwanafunzi mwingine wa Amali Lowa, pia anawataka wenzake walioacha shule kwa sababu ya umbali warejee sasa kwa kuwa shule ipo jirani.


Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Shule ya Amali Lowa, Mwalimu Ezekia Ngabo, anasema shule hiyo ilianza rasmi Julai 28, 2025 ikiwa na wanafunzi 47 (wavulana 13 na wasichana 34) na walimu 9 pamoja na mlinzi mmoja.




"Shule hii ina mikondo miwili: wa jumla na wa amali (elimu ya vitendo), Kupitia mkondo wa amali, hasa somo la kilimo, tunawajengea wanafunzi stadi za maisha zitakazowawezesha kujiajiri na kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji."




Mtazamo wa Viongozi


Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu, anabainisha kuwa mafanikio haya ni matunda ya ushirikiano kati ya Serikali Kuu na Halmashauri:




"Tunamshukuru Rais Samia kwa kutuwekea mazingira bora ya ukusanyaji mapato na kutupatia fedha za maendeleo. Tulipokea zaidi ya shilingi bilioni 1.2 kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za Wendele na Amali Lowa, zikiwa na madarasa, jengo la utawala, maabara na vyoo, Ujenzi umekamilika na wanafunzi wameanza kusoma, Huu ni ushahidi wa dhamira ya serikali kuwekeza kwenye elimu bora."


Masudi ameongeza kuwa miradi mingine ya maendeleo katika sekta za afya, barabara na maji imeendelea kuipamba Manispaa ya Kahama, na kuimarisha ustawi wa wananchi.


Hitimisho


Wananchi wa Kahama sasa wananufaika moja kwa moja na miradi ya elimu, afya, na miundombinu, matunda ya Ilani ya CCM na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita.


Changamoto bado zipo, kama vile mahitaji ya walimu na vifaa vya kisasa vya kujifunzia, lakini matumaini yamejengeka, Ndoto za watoto wa vijijini kupata elimu bora sasa zinageuka kuwa uhalisia.


Jitokeze kushiriki Uchaguzi Mkuu wa 2025 kwa amani na utulivu ili miradi ya maendeleo iendelee.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Kahama, Masudi Kibetu akimshukuru Rais Samia kwa kuiwezesha Manispaa ya Kahama kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo ya elimu
Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari ya Amali Lowa
Muonekano wa madarasa ya shule ya sekondari Wendele
Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani
Shija Butemi mwanafunzi wa Amali Lowa, akiishukuru selikali ya Rais Samia kwa kuwajengea shule karibu na maeneo ya nyumbani kwao
Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani

Wanafunzi shule ya sekondari Wendele wakiwa darasani

Source

CMSA Yaipongeza Tanga Saruji kuzindua Mauzo ya Hisa Stahiki za Bilioni 204

Kampuni ya Tanga Saruji imeweka historia mpya katika masoko ya mitaji nchini Tanzania kwa kuzindua rasmi mauzo ya Hisa Stahiki zenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 204. Hii ni mara ya kwanza kwa kampuni nchini kutoa hisa stahiki za thamani kubwa kuwahi kushuhudiwa katika historia ya Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), hatua inayotajwa kuwa ya kimkakati katika kuimarisha uwekezaji na kuongeza thamani kwa wanahisa.


Akizungumza katika uzinduzi huo, Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama aliipongeza Bodi na Menejimenti ya Kampuni ya Saruji Tanga kwa uongozi thabiti, ujasiri na maono ya kimkakati yaliyopelekea mageuzi makubwa ya kiutendaji ndani ya kampuni hiyo.

"CMSA tunaridhishwa na hatua za mabadiliko ya kimkakati yanayoendelea katika kampuni hii, ikiwa ni pamoja na kupunguza mikopo ya kigeni, kuongeza mapato na faida ya kampuni, na kutoa fursa zaidi za uwekezaji kwa wananchi," alisema CPA Mkama

Hisa hizi stahiki zinauzwa kwa wanahisa wa sasa wa Kampuni ya Tanga Saruji kwa bei ya shilingi 1,600 kwa hisa moja, ambayo ni punguzo la asilimia 38.2 ukilinganisha na bei ya soko ya shilingi 2,590 kwa hisa moja. Kiasi cha hisa kinachotolewa ni 127,342,090, katika uwiano wa hisa mbili kwa kila hisa moja anayomiliki mwekezaji kwa sasa.

Aidha Utoaji huo wa hisa umetajwa kuwa umekidhi kikamilifu matakwa ya Sheria ya Masoko ya Mitaji na Dhamana, Sura ya 79 ya Sheria za Tanzania pamoja na Kanuni zake, baada ya kupokea idhini rasmi kutoka CMSA.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, ongezeko la thamani ya hisa za Kampuni ya Saruji Tanga limekuwa kubwa kwa kipindi cha muda mrefu – kutoka shilingi 300 mwaka 2002 hadi shilingi 2,590 kwa hisa moja mwaka 2025, sawa na ongezeko la asilimia 763.3.

"Tunaipongeza Kampuni ya Tanga Saruji  kwa mafanikio haya makubwa. Hili ni somo na mfano kwa kampuni nyingine zilizo orodheshwa katika soko la hisa kuendelea kuboresha ufanisi na utawala bora," aliongeza CPA Mkama.

Aidha, alieleza kuwa mafanikio ya Tanga Cement  ni uthibitisho wa nafasi muhimu ya masoko ya mitaji katika kukuza uchumi wa Taifa, kwa kutoa mitaji ya muda mrefu kwa kampuni, kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuhamasisha umiliki wa pamoja wa rasilimali za uzalishaji.

Pia CPA Mkama amesisitiza kuwa mafanikio hayo ni sehemu ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 (TDV 2050), ambayo inalenga kuifikisha Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati wa juu na kufikia Pato la Taifa la Dola Trilioni 1 ifikapo mwaka 2050.

Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA) pia imepongeza wadau waliohusika katika mchakato wa maandalizi ya Waraka wa Matarajio, akiwemo mshauri kiongozi wa kifedha iTrust Finance Limited, Mshauri wa Kisheria Joachim & Jacobs Attorneys, pamoja na wakaguzi Deloitte & Touche, kwa weledi wao mkubwa uliofanikisha hatua hii muhimu.

Mchakato wa mauzo ya hisa hizo unatarajiwa kufungwa Oktoba 24, 2025, na wanahisa wametakiwa kuchangamkia fursa hiyo adhimu ya kuongeza uwekezaji wao kwa bei ya punguzo.

"Napenda kutoa wito kwa wanahisa wote kutumia fursa hii kununua hisa stahiki, ili kuimarisha uwekezaji wao na kuwa sehemu ya mafanikio endelevu ya kampuni hii ya kihistoria," aliongeza

CPA Mkama pia amezitaka kampuni nyingine katika sekta binafsi na umma kutumia kikamilifu masoko ya mitaji kama chanzo mbadala cha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, badala ya kutegemea mikopo ya gharama kubwa.

 








Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...