Wednesday, July 2, 2025

JUMBE AREJESHA FOMU YA UBUNGE SHINYANGA MJINI... "ZOEZI LIMEENDA VIZURI, CCM IMEWEKA MAZINGIRA BORA KWA WATIA NIA"

Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mhandisi James Jumbe Wiswa leo Julai 2, 2025 amerejesha fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho kugombea Ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Akizungumza mara baada ya kurejesha fomu katika ofisi za CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhandisi Wiswa amesema zoezi la uchukuaji na urejeshaji wa fomu limeenda vizuri na kwa utulivu mkubwa bila changamoto yoyote.


"Leo nimekuja kwa mara ya pili, hatua ya kwanza ilikuwa ni uchukuaji wa fomu, nimejaza fomu, na leo ni siku ya urejeshaji. Tumekamilisha hatua ya awali ya uchukuaji na urejeshaji wa fomu. Zoezi limeenda vizuri. Kimsingi, mimi binafsi na wala sijasikia kwa mtu mwingine kama kulikuwa na changamoto yoyote katika hatua hii," amesema Mhandisi Jumbe.

Mhandisi Jumbe amepongeza uongozi wa CCM Wilaya kwa kuweka mazingira rafiki kwa watia nia na wagombea, akieleza kuwa taratibu zimekuwa rahisi na hazichukui muda mrefu.


"Unapofika kuchukua fomu unapewa control number, unalipia, unakabidhiwa fomu na kuendelea na ujazaji na uwasilishaji. Niwapongeze Mwenyekiti wa Chama, Katibu, Sekretarieti na watumishi wengine kwa maandalizi bora," ameongeza.

FAHAD AJITOSA UBUNGE SHINYANGA MJINI KUPITIA CCM: AVUNJA UKIMYA TETESI ZA ACT-WAZALENDO

Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Fahad Gulamhafiz Mukadam akionesha fomu kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini

Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

 Mtoto wa mwanasiasa mkongwe na Meya mstaafu wa Manispaa ya Shinyanga, Mzee Gulamhafiz Mukadam, bwana Fahad Gulamhafiz Mukadam, ameibuka hadharani na kutangaza rasmi nia ya kugombea Ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Akizungumza leo Julai 2, 2025 mara baada ya kuchukua fomu ya kuomba ridhaa ya chama hicho, katika ofisi za CCM wilaya ya Shinyanga Mjini, Fahad amesema ameamua kutumia haki yake ya kikatiba na ya msingi kama mwanachama wa CCM mwenye sifa stahiki, ili kuchangia maendeleo ya wananchi wa Shinyanga kupitia nafasi ya ubunge.

"Mimi ni mtoto wa Shinyanga. Nimechukua fomu kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi kugombea ubunge Jimbo la Shinyanga Mjini. Kama ilivyo taratibu za chama chetu, kila mwenye sifa ana haki ya kugombea. Nimetumia haki yangu ya kikatiba na natamani kushirikiana na wana Shinyanga kuleta maendeleo," amesema Fahad.

Aidha, Fahad ameweka wazi kuwa amechukua hatua hiyo kama sehemu ya kutekeleza dhamira yake ya kweli ya kuwatumikia wananchi, huku akimpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweka mazingira ya wazi ya kisiasa nchini.
"Kupitia uongozi wa Rais Samia, kila mmoja ameruhusiwa kusema. Mengi yamesemwa kuhusu mimi, lakini leo nimeamua kuzungumza kwa vitendo. Nipo katika ofisi za CCM, chama chenye misingi, imani na miundo imara ya kuleta maendeleo kwa Watanzania," ameongeza.

Avunja Ukimya Kuhusu Tuhuma za ACT-Wazalendo

Fahad pia ametumia nafasi hiyo kukanusha vikali taarifa zilizoenea kwenye mitandao na midomo ya watu kwamba anapanga kugombea ubunge kupitia Chama cha ACT-Wazalendo.

"Wapo wanaosema nagombea kupitia ACT-Wazalendo. Pamoja na heshima kubwa niliyonayo kwa vyama vya upinzani, sijawahi kutamka wala kufikiria jambo hilo. Ni minong'ono tu ya watu, nami leo nimejibu kwa vitendo kwa kuchukua fomu kupitia CCM," amesema.

Tetesi hizo zilianza kusambaa kwenye duru za kisiasa zikidai kuwa maandalizi ya Fahad kugombea kupitia ACT-Wazalendo . 
Hata hivyo, kwa hatua ya kuchukua fomu ya CCM, mambo yamewekwa wazi.

Kwa kufanya uamuzi huo, Fahad Gulamhafiz Mukadam amejiunga na orodha ya makada kadhaa wa CCM waliokwisha tangaza nia ya kuwania ubunge Shinyanga Mjini, huku ushindani ukiendelea kupamba moto kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 2025.


Tuesday, July 1, 2025

Naibu waziri Sillo awajulia hali majeruhi ajali ya Same.


Na John Walter -Kilimanjaro 

Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Daniel Sillo, amefika katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC, Hospitali ya Mawenzi, na Hospitali ya Wilaya ya Same leo Juni 29, 2025, kwa ajili ya kuwapa pole na kuwajulia hali majeruhi wa ajali iliyotokea jana Juni 28, 2025, Wilayani  Same, mkoani Kilimanjaro.

Ajali hiyo iliyohusisha basi la Kampuni ya Chanel One na gari dogo aina ya Coaster (Rosa) imesababisha vifo vya watu 38 na kujeruhi watu wengine 30. Mhe. Sillo ameeleza masikitiko yake kutokana na tukio hilo na kutoa pole kwa familia zilizopoteza wapendwa wao, huku akiwatakia majeruhi uponaji wa haraka.

Katika ziara hiyo, Mhe. Sillo ameambatana na Kamanda wa Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani Tanzania, SACP William Mkonda, pamoja na Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, CP Awadhi Juma ambapo wametembelea pia eneo la tukio iliyotokea ajali hiyo

Aidha, Naibu Waziri Sillo ametoa wito kwa Madereva wote kuzingatia Sheria za usalama barabarani na kuwa waangalifu wakati wote ili kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.

Mhe. Sillo ameongeza kuwa Serikali kupitia Vyombo vya Usalama itaendelea kuchukua hatua kali kwa wote watakaokiuka Sheria na Kanuni za Usalama Barabarani, ikiwa ni pamoja na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara wa magari ya abiria pamoja na kutoa elimu kwa Madereva.


Picha mbalimbali wakati alipowatembelea majeruhi na eneo la tukio.










Wednesday, June 25, 2025

RAIS SAMIA AMEWEKA ALAMA KWA WATUMISHI WA MAGEREZA ARUSHA, AWAGAWIA MITUNGI 528




📌Nishati safi ya kupikia ni endelevu

📌Yaelezwa ni salama na mkombozi wa mazingira

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameacha  alama mkoani Arusha kwa kugawa mitungi ya gesi 528 na majiko yake kwa watumishi wa jeshi la magereza mkoani ili kuhamasisha matumizi ya nishati safi na salama nchini. 

Hayo yamebainishwa leo Juni 25, 2025 na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu wakati wa  uzinduzi wa kugawa  majiko ya gesi kwa watumishi wa magereza iliyofanyika gereza kuu mkoani Arusha. 

"Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan  ndiye kinara wa nishati safi ya kupikia nchini ambaye anaendelea kuhamasisha taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 kutumia nishati safi na salama," Amesema. 

Ameongeza kuwa, Serikali imeendelea kuhamasisha na kuwataka watanzania wote kuhakikisha wanatumia nishati safi ya kupikia kama njia mahususi ya kutunza na kulinda mazingira na pia kuokoa uharibifu wa misitu

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mha. Hassan Saidy amewaeleza watumishi wa magereza kuwa nishati safi ni salama kwa Taifa kwa kuwa inaondoa magonjwa yanayosababishwa na matumizi ya nishati isiyo safi na salama ya kuni na mkaa

"Ndugu zangu watumishi wenzangu, nawasihi sana kutumia nishati safi na salama katika matumizi yenu kwa sababu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka fedha nyingi ili kila mtanzania atumie nishati safi ya kupikia kuliko kutumia kuni na mkaa," Ameongeza Mha. Saidy.

Akizungumzia kuhusu Mkakati wa Taifa wa Mawasiliano wa Nishati safi ya kupikia ameeleza kuwa, lengo kuu la mkakati huo ni kuongeza uelewa wa wananchi na taasisi kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia na malengo mengine mahususi ni kuandaa na kutekeleza kampeni maalum za uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi. 

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Magereza mkoa wa Arusha, ACP Prosper Kapinga ameipongeza REA kwa tukio hilo muhimu la kugawa mtungi wa gesi na majiko ya sahani mbili na kusema kuwa inaonesha kwa vitendo juhudi za Serikali katika kuboresha maisha ya wananchi kupitia Nishati Safi ya Kupikia.

Source

Wakulima Babati Wavutwa Kulima Karanga Baada ya Utafiti wa TARI


Na John Walter -Babati 

Wakulima wa Wilaya ya Babati, hususan wa ukanda wa Mbugwe mkoani Manyara, wameonyesha mwitikio mkubwa katika kulima zao la karanga kufuatia utafiti uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) kupitia kituo chake cha Naliendele.

Utafiti huo umebainisha kuwa mazingira ya eneo hilo yanafaa kwa kilimo cha karanga na kwamba zao hilo lina soko la uhakika, hatua ambayo imewapa matumaini wakulima na kuchochea hamasa ya kulima kwa tija.

Mtafiti kutoka TARI Naliendele, Bw. Anthony Bujiku, amesema Tanzania ipo katika nafasi nzuri kwenye uzalishaji wa karanga ukilinganisha na mataifa mengine ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Ameeleza kuwa Tanzania ina takribani hekta milioni tatu zenye rutuba zinazofaa kwa kilimo cha karanga, lakini kwa sasa ni hekta milioni moja na nusu pekee ndizo zinazotumika.

"Tunayo ardhi ya kutosha na mbegu bora, hivyo tunawahimiza wakulima watumie mbegu zilizofanyiwa utafiti ili kuongeza tija," amesema Bw. Bujiku.

Mkulima kutoka Kijiji cha Kiru, Jitu Vrajilal Son, ambaye shamba lake limehusika moja kwa moja kwenye utafiti wa mbegu bora za karanga, amesema kuwa TARI imekuwa mkombozi mkubwa kwao.

 "Tulikuwa tukipanda kienyeji, lakini sasa tunatumia mbegu bora na teknolojia ya kisasa, matokeo ni mazuri na ya kutia moyo," amesema kwa furaha.

Wakulima wengine waliopata nafasi ya kushiriki kwenye mafunzo na majaribio ya kilimo hicho wamesema utafiti uliofanywa na TARI umewapa matumaini makubwa na wameiomba Serikali kuendeleza utafiti kama huo kwenye mazao mengine pia, ili kuinua kilimo kwa ujumla.

Serikali kupitia wizara husika inaendelea kutuma wataalamu wake katika maeneo mbalimbali ili kufanya tafiti zaidi kuhusu zao hilo, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuongeza uzalishaji na kuhakikisha wakulima wanapata mazao yenye tija na soko la uhakika.

Kwa hatua hii, Babati inaelekea kuwa miongoni mwa maeneo muhimu ya uzalishaji wa karanga nchini, na mfano wa kuigwa kwa maeneo mengine ya Tanzania.

TRA SHINYANGA YATOA ELIMU YA KODI KWA WANACHUO CHA UFUNDI STADI VETA


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) mkoa wa Shinyanga imeendesha semina ya elimu ya ulipaji kodi kwa wanachuo wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuwajengea uelewa vijana kuhusu umuhimu wa kulipa kodi kwa maendeleo ya nchi.

Semina hiyo imefanyika leo Juni 25, 2025 katika Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) Shinyanga kilichopo manispaa ya Shinyanga.

Akizungumza wakati wa semina hiyo, Afisa wa kodi kutoka TRA Shinyanga Semeni Mbeshi, amesema lengo ni kuwajengea msingi mzuri wa kizalendo vijana wanaotarajia kuingia kwenye soko la ajira na kujiajiri baada ya kuhitimu masomo yao.

Ameongeza kuwa elimu hiyo ni endelevu na inalenga kujenga taifa la watu waaminifu katika ulipaji wa kodi, huku akisisitiza matumizi ya IFD kwa wafanyabiashara na kutoa na kudai risiti pindi wanaponunua bidhaa.

"Haki ya mlipa kodi ni kuaminiwa pindi anapofika kwenye ofisi za TRA kwa ajili ya kufanyiwa makadilio yanayoendana na biashara yake, ni wajibu wa kila mfanyabiashara kutoa taarifa ya ufanyaji wa biashara kwa mamlaka ya mapato TRA, utoaji wa risiti za IFD zinasaidia kuweka rekodi sahihi ya kumbukumbu ya biashara kwa muda wa miaka 5, lakini kodi hiyo inakwenda moja kwa moja kwenye mfuko wa serikali na kuwezesha maendeleo kwenye taifa letu", amesema Semeni Mbeshi.

Kwa upande wake, Mkufunzi katika Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) Shinyanga, Emili Shirima amesema vitendo vya baadhi ya watu kutumia vishoka kujipatia huduma za kikodi si sahihi na ni hatari kwa uchumi wa taifa, alisema na kuwataka wanachuo kujiepusha na tabia hizo mara watakapoingia kwenye shughuli za uzalishaji mali.

Baadhi ya wanachuo walioshiriki mafunzo hayo wameishukuru TRA kwa kuwapa elimu hiyo muhimu, wakisema itawasaidia  mara baada ya kuhitimu na kuanzisha biashara au shughuli za kujitegemea na kuo ngeza kuwa sasa anaelewa kwamba ulipaji wa kodi unasaidia huduma za jamii kama afya, elimu na miundombinu.

Afisa wa kodi kutoka TRA Shinyanga Semeni Mbeshi akizungumza wakati wa mafunzo hayo.






Baadhi ya wanafunzi walioshiriki mafunzo hayo.































 

Tuesday, June 24, 2025

SERIKALI YAZIDI KUHAMASISHA NISHATI SAFI, YATOA MITUNGI 225 KWA WATUMISHI GEREZA KUU MAWENI



📌Shilingi bilioni 35 kupeleka nishati safi magereza yote nchini

📌Mitungi ya gesi 653 kupatiwa watumishi magereza Tanga

📌Mha. Saidy asisitiza uhamasishaji wa matumizi ya nishati safi

Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imeendelea kuwezesha, kuhamasisha na kutoa elimu kuhusu umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia kwa watumishi wa magereza na wananchi ili kufikia malengo yaliyoainishwa kwenye mkakati wa kitaifa wa matumizi ya nishati safi ya kupikia (2024 – 2034).

Hayo yamebainishwa leo Juni 24, 2025 na Mwenyekiti wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Mhe. Balozi Meja Jenerali Mstaafu Jacob Kingu wakati wa uzinduzi wa kugawa majiko ya gesi kwa watumishi wa magereza iliyofanyika Gereza Kuu la Maweni jijini Tanga. 

"Hii yote ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jumhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhusu taasisi zote zinazohudumia watu zaidi ya 100 zihame kutoka katika matumizi ya nishati chafu na kuhamia katika nishati safi ya kupikia, " Ameongeza. 

Vile vile ameongeza kuwa, Magereza yote ya mkoa wa Tanga tayari yanatumia makaa ya mawe ya Rafiki Briquette unaozalishwa na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO). 

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa REA Mha. Hassan Saidy amewataka watumishi wa magereza kuendelea kuhamasisha na kutoa elimu kuhusu matumizi na umuhimu wa nishati safi ya kupikia ili kuifanya nishati hiyo kuwa endelevu, pia ni chachu kwa wananchi katika kufikia malengo yaliyoainishwa kwenye mkakati wa kitaifa.

Amesema kuwa, gharama ya mradi wote ni zaidi ya shilingi Bilioni 35.2 ambapo Wakala wa Nishati Vijijini unatoa ruzuku ya shiling bilioni 26.5 Sawa na asilimia 75.4 ya gharama ili kuwezesha utekelezaji wake.

Kwa upande wake, ACP Nade Baynit, Kaimu Mkuu wa Magereza Mkoa wa Tanga ameishukuru REA kwa kuwezesha watumishi magereza kutumia nishati safi ya kupikia. Aidha, amewakata watumishi hao kuchangamkia fursa hiyo inayotolewa na REA kwa watumishi wa magereza kwa kujipatia mtungi wa gesi na majiko ya gesi ya sahani mbili  bure na waeendelee kuwa mabalozi wa nishati hiyo kwa wananchi.

Naye, Mratibu wa nishati safi kutoka kampuni ya Lake Gas Ltd Bw. Ramadhani Siasa amesema watatekeleza mradi huo kwa kuzingatia makubaliano ya Mkataba wa kusambaza mitungi ya gesi ya kupikia pamoja na kutoa elimu, kuhamasisha wananchi ili kuchochea matumizi ya nishati hiyo.









Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...