Wednesday, July 16, 2025

‎Mwenge wazindua daraja la watembea kwa miguu Tipri Mbulu. ‎


Na John Walter -Mbulu

Mradi wa ujenzi wa daraja la watembea kwa miguu Tipri lililoko kata ya Gehandu, halmashauri ya mji wa Mbulu, umeleta afueni kubwa kwa wananchi takribani 3,995, wakiwemo wanafunzi ambao sasa wanaweza kuhudhuria masomo bila usumbufu wakati wote wa mwaka.

‎Akisoma taarifa ya mradi huo wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, Meneja wa TARURA wilayani Mbulu, Mhandisi Nuru Hondo, amesema kabla ya kujengwa kwa daraja hili, wanafunzi walikuwa wanakwamishwa na mvua kwa takribani miezi saba kila mwaka, jambo lililoathiri mahudhurio na maendeleo yao kielimu.

‎Ameeleza kuwa daraja hilo kutokana na uimara wake linaweza kudumu kwa miaka 70.

‎Mwenge wa Uhuru umepokelewa wilayani Mbulu kwa ziara ya kukagua, kutembelea, kuzindua na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi mbalimbali yenye thamani ya Shilingi bilioni 44, ikiwemo miradi ya afya, miundombinu ya barabara na miradi mingine ya maendeleo.

‎Miongoni mwa miradi hiyo ni daraja hili la Tipri, ambalo linaunganisha vijiji vya Tsawa na Tipri.

‎Kukosekana kwa daraja hilo kwa muda mrefu kulisababisha wananchi kupata changamoto kubwa katika kupata huduma muhimu, hasa wakati wa mvua ambapo mto huo ulikuwa unakuwa kikwazo kikubwa. Mradi huo umegharimu zaidi ya shilingi milioni 158.9.

‎Akizungumza kwenye eneo la mradi, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa mwaka 2025, Ismail Ali Ussi, ameipongeza halmashauri ya mji wa Mbulu kwa ubunifu na utekelezaji wa mradi huu muhimu.

‎Vilevile, ameishukuru kamati ya ulinzi na usalama kwa usimamizi mzuri wa fedha za mradi.

‎Mwenge wa Uhuru mwaka huu unaendelea na kaulimbiu isemayo: ‎"Jitokeze kushiriki uchaguzi mkuu wa mwaka 2025 kwa amani na utulivu."

Mwenge wa uhuru wazindua Mradi wa nishati mbadala Manyara Girls Sekondari



Na John Walter -Babati

Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Ali Ussi, amezindua mradi wa nishati mbadala katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Manyara wenye thamani ya shilingi milioni 21.9.

‎Mradi huo unalenga kurahisisha upikaji wa chakula kwa wanafunzi pamoja na kutunza mazingira kwa kupunguza ukataji miti ovyo.

‎Kiongozi huyo amesema ni jitihada za Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya nchi na kulinda afya za Wananchi.

‎Akisoma taarifa kwa Kiongozi wa mbio za Mwenge wa uhuru Kitaifa, Mkuu wa shule ya Manyara Girls, Bi. Gisella Msofe, amesema mradi huo wa gesi safi ya kupikia utapunguza muda wa kuandaa chakula na kuchangia jitihada za shule katika uhifadhi wa mazingira.

‎Baadhi ya wanafunzi akiwemo Sabrina Msangi, Faith Flavian na Sharon Msangi, wameishukuru serikali kwa mradi huo, wakieleza kuwa sasa watakuwa na muda zaidi wa kusoma badala ya kutumia muda mwingi kutafuta kuni, pamoja na kulinda afya zao kutokana na kupunguza moshi unaotokana na kuni na mkaa.

‎Mradi huo ni sehemu ya mpango wa serikali wa kuhamasisha wananchi kuachana na matumizi ya mkaa na kuni ili kulinda mazingira, ambapo serikali imeanza na taasisi zinazolisha watu kuanzia 100 na imekuwa ikitoa mitungi ya gesi kwa bei ya ruzuku ya shilingi 17,500.


Source

Gwajima: CCM Sihami, Tunabanana Mpaka Kieleweke



"Mimi bado ni mwanachama wa Chama cha Mapinduzi na nitaendelea kuwepo. Mimi sihami, CCM nipo sana, tunabanana humu humu ndani mpaka paeleweke pakae vizuri. CCM ni chama cha kidemokrasia kama ilivyo madhumuni ya katiba yake." - Askofu Josephat Gwajima


Tuesday, July 15, 2025

Mchambuzi Hans Rafael Amchana MO Dewji Vibaya: Asitufanye Sisi Watoto

 

Mchambuzi Hans Rafael Amchana MO Dewji Vibaya: Asitufanye Sisi Watoto


Binafsi nimemsikiliza Tajiri ila sıjaona utofauti wa kile alichoongea msimu uliopita na leo.

1. Mo anasema ametoa zaidi ya Tsh 80b,inawezekana ni kweli Ila atwambie na Yeye Simba imemtengenezea kiasi gani?….maana kila mwaka anatumia Brand ya Simba kutangaza bidhaa zake.


2. Mo amesema kila mwaka anatoa hela ya usajili ila mambo yamezidi kuwa yale yale kila mwaka Simba wanasajili Wachezaji 17 na mwisho wa Msimu wanakata 14 je Mo haoni pale Simba kuna shida ya utendaji? Kwani asiwaondoe viongozi wote wanaosajili…..? na kuajiri watu wapya wa mpira kama (Technical Director na Drector of football) ili wasimamie vizuri project na Pesa zake? Kwanini ameendelea kuwakumbatia viongozi wale wale ambao kila msimu wanafuja pesa zake kwa kusajili Wachezaji wa kawaida?


Binafsi nadhani hakuna tajiri mjinga ambae kila mwaka atakubali kupoteza hela Yake Kama hapati faida……Mo amekomaa na Simba coz anapata faida,biashara zake zinaenda,Simba ni Brand kubwa ambayo kila tajiri nchini anatamani kuitumia leo asitufanye sisi kama watoto😄


Ifike Muda matamko yakome,vitendo viongee,Simba kabla ya kupata hela ya Mo wanahitaji mfumo mpya wa katiba na viongozi Ila hawa wa Sasa sioni wakifanya Jambo

Mo Dewji : Toka Mwaka 2018 Hadi Leo Nimetumia Bilioni 87 Kwa Ajili ya Simba



"Kuanzia mwaka 2018 hadi leo nimewekeza shilingi Bilioni 45 kwa ajili ya mishahara, usajili, maandalizi ya Timu na mahitaji mengine ya uendeshaji, pia nimechangia shilingi Bilioni 20 kama sehemu ya ununuzi wa hisa asilimia 49 ndani ya Simba Sports Club na mara nyingi nimekuwa nikitoa msaada nje ya mfumo rasmi, kila palipojitokeza uhitaji wa dharura kuanzia mwaka 2017 hadi 2024 nimetumia takribani Bilioni 22 katika misaada ya dharura hivyo kufanya jumla ya mchango wangu kwa Simba kufikia shilingi Bilioni 87 hivyo kusema Mo hatoe hela ni kauli ya kupotosha yenye mwelekeo wa chuki, tuachane na fitna zisizo na msingi, tujenge palipotoboka, tuzibe ufa panapovuja na tusonge mbele bila kuonyeshana vidole" 

——— 
Mohammed Dewji, Mwekezaji na Rais wa heshima wa Simba Sports Club.

Monday, July 14, 2025

‎Mwenge wa Uhuru Waweka Jiwe la Msingi Ujenzi wa Ghala la Kuhifadhi Mazao Kiteto. ‎


Na John Walter -Kiteto 

Mwenge wa Uhuru umeweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa ghala la kuhifadhi mazao katika Wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara.

‎Taatifa ya mkuu wa wilaya ya Kiteto Remidius Mwema kwa Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025, Ismail Ussi, imesema lengo la mradi huo ni kutoa huduma za kiutawala kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala, kuinua uchumi wa wananchi na kutoa hifadhi salama ya mazao.

‎Mradi huo unagharimu shilingi milioni 149,680,000 ambazo ni mapato ya ndani ya Halmashauri.

‎Hadi sasa mradi umefikia asilimia 70 ya utekelezaji na unatarajiwa kuwa na uwezo wa kuhifadhi mahitaji ya tani kati ya 437.6 hadi 600 za mazao.

‎Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru na timu yake wameridhishwa na mradi huo na hatimaye wameweka jiwe la msingi kama ishara ya kuunga mkono jitihada hizo za maendeleo.

‎Kiongozi huyo wa Mwenge ameupongeza uongozi wa Wilaya kwa kuchukua hatua hiyo muhimu ya kuwakumbuka wakulima, akieleza kuwa kupitia ghala hilo wakulima watanufaika kwa kuhifadhi mazao yao kwa usalama na kupata fursa ya kuuza kwa bei bora kupitia mfumo wa stakabadhi za ghala.

‎Kauli mbiu ya Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025 ni:

‎"Jitokeze kushiriki uchaguzi mkuu wa 2025 kwa amani na utulivu."

Friday, July 11, 2025

Mkoa wa Manyara Wazindua Mpango wa Usambazaji Nishati Safi ya Kupikia kwa Bei ya Ruzuku


Na John Walter -Hanang'

Katika juhudi za kulinda mazingira na kuboresha afya za wananchi, leo julai 11,2025 mkoa wa Manyara umezindua rasmi mpango maalum wa usambazaji wa nishati safi ya kupikia kwa bei nafuu kupitia ruzuku ya serikali.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo uliofanyika wilayani Hanang', Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Queen Sendiga, amewataka Wakuu wa wilaya zote tano za mkoa huo kusimamia kikamilifu utekelezaji wa mpango huo ili kuhakikisha unafikia malengo yaliyokusudiwa. 

Ameongeza kuwa mawakala wanaosambaza mitungi hiyo ya gesi wanapaswa kuwa waaminifu kwa kuuza kwa bei iliyoelekezwa na serikali.

Mpango huu ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa Matumizi ya nishati safi kwa kizazi cha sasa na kijacho, ambao umeanza tangu mwaka 2020 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2034, chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa Mratibu wa mradi huo, Abdulrazack Mkomi, serikali imetoa ruzuku kwenye mitungi ya gesi ya kilo sita, ambapo kila wilaya imepokea mitungi 3,255. 

Wananchi wataweza kununua mtungi mmoja kwa shilingi 17,500 pekee, kwa sharti la kuwa na kitambulisho cha Taifa (NIDA).

Mradi huu una lengo la kuongeza upatikanaji wa huduma za nishati safi ya kupikia, kulinda afya za wananchi dhidi ya madhara yatokanayo na moshi wa mkaa na kuni, kuboresha uchumi wa kaya na pia kuhifadhi mazingira kutokana na kupungua kwa ukataji wa miti.

Kwa mujibu wa takwimu, jumla ya mitungi 16,275 itasambazwa kwenye wilaya zote tano za Mkoa wa Manyara, huku zaidi ya shilingi milioni 284.8 zikitumika kugharamia mradi huo.

Kwa hatua hii, serikali inatarajia kuona mabadiliko makubwa katika mtindo wa maisha ya wananchi, kupungua kwa uharibifu wa mazingira na kuongezeka kwa matumizi ya nishati salama na rafiki kwa mazingira.

Thursday, July 10, 2025

CPA Mkama azindua mfuko wa uwekezaji wa iDollar awataka Watanzania kuchamkia fursa


Katika hatua ya kimkakati ya kuimarisha uwekezaji wa ndani na kuongeza mchango wa fedha za kigeni katika uchumi wa taifa, kampuni ya iTrust Finance Limited imezindua rasmi Mfuko wa Uwekezaji wa Pamoja ujulikanao kama iDollar Collective Investment Scheme.

Mfuko huu utawawezesha Watanzania kuwekeza kwa kutumia sarafu za kigeni kama Dola za Marekani, Pauni za Uingereza, pamoja na sarafu nyingine za kimataifa.

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Masoko ya Mitaji na Dhamana (CMSA), CPA Nicodemus Mkama, alisema kuwa mafanikio haya ni matokeo ya mazingira bora ya kisera na kisheria yaliyowekwa na serikali kupitia CMSA kwa ajili ya kukuza sekta ya masoko ya mitaji nchini.

"Mfuko huu ni nyenzo muhimu ya kuhamasisha fedha za kigeni. Unachangia katika utulivu wa uchumi na kuimarisha uwezo wa nchi kukabiliana na changamoto zinazohusiana na sarafu za kigeni. Pia unawawezesha Watanzania kuwekeza akiba zao za fedha za kigeni moja kwa moja kutoka kwenye akaunti zao za benki," alisema CPA Mkama.

Aidha, aliongeza kuwa kwa kuzinduliwa kwa mfuko huu, Tanzania inajiunga na nchi nyingine za Afrika kama Kenya, Afrika Kusini, Mauritius na Ghana ambazo tayari zina mifumo kama hii. Aliwataka Watanzania, taasisi na kampuni mbalimbali kuchangamkia fursa hii ya kukuza uwekezaji kupitia sarafu za kigeni.


CPA Mkama alifafanua zaidi kuwa Mfuko wa iDollar ni miongoni mwa mifuko ya uwekezaji wa pamoja iliyosajiliwa na kuidhinishwa na CMSA, sambamba na ile inayoendeshwa na UTT AMIS. Alisisitiza kuwa mfuko huu pia utakuwa jukwaa la Watanzania wanaoishi nje ya nchi (diaspora) kuwekeza mapato yao ya kigeni na kuchangia ukuaji wa uchumi wa ndani.

Kwa upande wake, Prof. Mohamed Warsame, Mkurugenzi Mtendaji wa iTrust Finance Limited, alisema kuwa lengo la mfuko wa iDollar ni kutoa suluhisho kwa Watanzania wengi ambao tayari wana akaunti za dola katika benki lakini wanakosa njia rasmi na yenye manufaa ya kuwekeza fedha hizo.

"Mfuko huu unawapa Watanzania fursa ya kuwekeza dola zao moja kwa moja kutoka kwenye akaunti zao na kupata mapato katika dola. Tuliona umuhimu wa kuanzisha mfuko huu kufuatia mabadiliko ya kisheria yanayokataza matumizi ya sarafu za kigeni katika miamala ya ndani kama kulipa ada za shule, kodi au huduma nyingine," Prof. Warsame alieleza.

Aliongeza kuwa kufuatia agizo hilo la kisheria, Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ilielekeza kuwa sarafu za kigeni hazitakiwi tena kutumika katika miamala ya ndani, na hivyo mfuko huu unatoa njia mbadala ya uwekezaji kwa watu binafsi na taasisi zinazomiliki akiba ya fedha za kigeni.

Mfuko wa iDollar utasimamiwa na iTrust Finance Limited, taasisi iliyosajiliwa na kusimamiwa na CMSA, huku CRDB Bank ikihusika na kuhifadhi na kusimamia mali za mfuko huo kama mlezi (custodian).

Kwa uzinduzi huu, Tanzania inaendelea kuchukua hatua za kuhakikisha ushirikishwaji mpana wa wananchi katika fursa za masoko ya mitaji na kuimarisha usimamizi wa fedha za kigeni kwa maendeleo endelevu ya taifa.






 

 

Kaganda awataka vijana kuwa walinzi wa mali za Serikali Babati



Na John Walter -Babati 

Mkuu wa Wilaya ya Babati, Bi. Emmanuela Kaganda, amewataka wananchi hususan vijana kuhakikisha wanalinda na kutunza mali za Serikali, ikiwemo miundombinu ya barabara na madaraja, ili kuepusha uharibifu usio wa lazima.

Bi. Kaganda ametoa wito huo leo, tarehe 09 Julai 2025, wakati akiweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa boksi kalavati kwenye barabara ya Mamire-Qash, katika kijiji cha Ngarenaro, kata ya Galapo, tarafa ya Babati.

Mradi huo unahusisha:

  • Ujenzi wa boksi kalavati moja kubwa,

  • Makalavati madogo matatu, na

  • Uwekaji wa changarawe katika urefu wa kilomita moja.

Kwa mujibu wa taarifa iliyosomwa na Mhandisi Naftali Lyatuu kutoka TARURA wilaya ya Babati, mradi huu unagharimu shilingi milioni 272,320,400, ambazo zote zimetolewa na Serikali Kuu.

Mradi huu unatarajiwa kuboresha mawasiliano na usafirishaji kati ya kata tatu muhimu za Galapo, Mamire na Endakiso, ambazo ni maeneo makuu ya kilimo.

Bi. Kaganda ameishukuru Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za kutekeleza mradi huu muhimu.

Kwa upande wao, viongozi wa vijiji pamoja na wananchi wamenufaika, wakiishukuru Serikali kwa kuboresha miundombinu hiyo, kwani awali kipindi cha mvua walikuwa wakikumbana na changamoto kubwa za usafiri.

Daraja hilo linatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 15 Julai 2025, wakati Mwenge wa Uhuru utakapo kimbizwa katika miradi ya maendeleo katika Halmashauri ya Wilaya ya Babati.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...