Friday, April 10, 2026

AMANI NI SILAHA YA KUTIMIZA NDOTO NA MAONO YETU- MSIGWA



Na mwandishi wetu, Dodoma

Msemaji Mkuu wa Serikali ya Tanzania Gerson Msigwa amesisitiza umuhimu wa kila Mtanzania kuendelea kufanya kazi kwa bidii pamoja na kulinda na kudumisha amani na mshikamano uliopo nchini kama msingi muhimu unaoweza kumsaidia kila Mmoja kuweza kutimiza ndoto na maono waliyo nayo kwa maendeleo na ustawi wa mtu mmoja mmoja, familia na Taifa kwa ujumla.

Msigwa ameyasema hayo wakati akizungumza ma Chombo kimoja cha habari Mjini Dodoma leo Jumamosi Aprili 10, 2026, akisisitiza kuwa hata matarajio, matamanio na mipango iliyo kwenye Dira ya maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 hayawezi kufikiwa bila ya amani, utulivu na mshikamano wa jamii utakaowezesha sekta binafsi na kila Mtanzania kujielekeza katika kuendeleza shughuli za kiuchumi na Kijamii.

"Hatuwezi kufanya kazi kama nchi haina utulivu, niwaombe Watanzania tulinde amani, utulivu na mshikamano wetu kwa gharama yoyote kwani ndoto hizi kubwa za kufikia matarajio na matamanio yetu zitatimia ikiwa tuna amani, utulivu na mshikamano." Amesema Msigwa.

Msemaji huyo wa serikali amesisitiza kuwa Dira 2050 katika kutimiza lengo la kuwa na uchumi wa Dola za Marekani trilioni moja unategemea sekta binafsi kwa takribani asilimia 70 na sekta ya Umma kwa asilimia 30 pekee, hivyo badala ya kupoteza muda kubishana na kushughulika na mambo ya maana, Msigwa ameomba kila Mtanzania kujielekeza katika uzalishaji mali na kutumia fursa za kiuchumi zilizopo nchini zikivutia zaidi kutokana na amani na utulivu uliopo nchini Tanzania.

Thursday, April 9, 2026

SAMAMBA ATOA WITO GST KUBORESHA MAZINGIRA YA KAZI, KUIMARISHA USHIRIKIANO


Na Mwandishi Wetu - Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Eng. Yahya Samamba, ameitaka Menejimenti ya Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) kuhakikisha inajenga mazingira rafiki ya kazi yatakayowawezesha watumishi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na kujisikia salama kazini.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Baraza la Wafanyakazi la GST uliofanyika katika ukumbi wa Tume ya Madini jijini Dodoma, Eng. Samamba amesema mazingira bora ya kazi ni msingi muhimu wa kuongeza tija, ubunifu na ufanisi katika utumishi wa umma.

Amesisitiza kuwa watumishi wanapaswa kufanya kazi kwa bidii na ubunifu ili kuiwezesha GST kuwa kitovu cha takwimu za jiosayansi zenye ubora na zinazopatikana kwa urahisi kwa wadau mbalimbali.

“Ni wajibu wa kila mtumishi kutekeleza majukumu aliyopewa kwa weledi na kuchangia kikamilifu mafanikio ya taasisi,” amesema Eng. Samamba.

Aidha, amewataka watumishi kuimarisha mshikamano, umoja na ushirikiano kazini, akibainisha kuwa hali hiyo itaongeza ufanisi katika utoaji wa huduma na kuinua hadhi ya utumishi wa umma.
Katika hatua nyingine, Eng. Samamba amewapongeza viongozi wapya wa Baraza la Wafanyakazi la GST, akieleza kuwa baraza hilo lina jukumu muhimu la kushauri uongozi juu ya ufanisi wa kazi, mipango ya maendeleo, pamoja na kuboresha ustawi wa wafanyakazi.

Amebainisha kuwa majukumu ya baraza yanajumuisha pia kujadili mipango ya mapato na matumizi, kupanga mikakati ya maendeleo ya taasisi, na kuimarisha ushirikiano kati ya wafanyakazi na uongozi.

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa GST, Eng. Ally Samaje, amesema taasisi hiyo itaendelea kuboresha utendaji wake ili kuchangia kikamilifu maendeleo ya sekta ya madini nchini.

Ameongeza kuwa GST imejipanga kuboresha huduma zake za jiosayansi na maabara, sambamba na kuendana na mabadiliko ya teknolojia, ili kutoa matokeo yenye tija kwa uchumi wa taifa.

Wednesday, April 8, 2026

TRA TANGA YAVUKA MALENGO KATIKA UKUSANYAJI WA MAPATO NDANI YA MIEZI TISA KUANZIA JULAI 2025 HADI MACH 2026.


 MAMLAKA ya mapato (TRA)mkoani Tanga imeweka rekodi mpya ya ukusanyaji wa mapato baada ya kukusanya jumla ya Shilingi Bilioni 406.17 katika kipindi cha miezi tisa (Julai 2025 – Machi 2026), ikiwa ni ongezeko la asilimia 137 ya lengo lililowekwa.


Katika kipindi hicho, Mkoa ulikadiriwa kukusanya kiasi cha Shilingi Bilioni 296.3, ambapo ufanisi huo mkubwa uliovuka lengo kwa takriban Shilingi Bilioni 110, umetajwa kuwa ni matokeo ya ushirikiano wa karibu kati ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), walipakodi, na vyombo vya ulinzi na usalama mkoani Tanga.


Akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa, Meneja wa TRA Mkoa wa Tanga, Castro John, amewashukuru walipakodi wa Tanga kwa kulipa kodi kwa hiari na kushirikiana na taasisi mbalimbali kama Chama cha Wafanyabiashara (JWT) na Chama cha Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo (TCCIA).


"Huu ni ufanisi mkubwa ambao haujawahi kutokea. Tunamshukuru Mkuu wa Mkoa na vyombo vya usalama kwa kuhakikisha mazingira ya ukusanyaji kodi yanakuwa salama. Sifa hizi ni za walipakodi wa Tanga ambao wamekuwa wasikivu na wazalendo kwa nchi yao," alisema John.


Licha ya mafanikio hayo, John ametoa onyo dhidi ya wafanyabiashara wanaotumia njia zisizo rasmi (njia za panya) kuingiza bidhaa nchini. Alibainisha kuwa bidhaa za magendo siyo tu zinaikosesha serikali mapato, bali ni hatari kwa afya ya mlaji kwani hazijapita katika taasisi za udhibiti wa ubora.


Aliongeza kuwa operesheni dhidi ya magendo zinaendelea na wafanyabiashara kadhaa wameshakamatwa na kutozwa faini kubwa (Penalties), huku akisisitiza kuwa chombo chochote kitakachokutwa kimebeba bidhaa za magendo kitataifishwa kulingana na sheria. Aidha, aliwataka wananchi kudai risiti za EFD na wafanyabiashara kutoa risiti halali katika kila manunuzi.


Meneja huyo, amewahimiza wafanyabiashara kutumia Bandari ya Tanga ambayo sasa inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kutoa mizigo kwa wakati, jambo linalochochea ukuaji wa biashara mkoani hapa.


Kuhusu wafanyabiashara wenye madeni makubwa, TRA imewataka kufika ofisini kwa ajili ya majadiliano (Negotiations) ili kuwekewa utaratibu wa kulipa kwa awamu. Mamlaka hiyo imebainisha kuwa imeweka "Dawati la Wafanyabiashara" kwa ajili ya kutoa elimu na kusaidia kukuza biashara ndogo ziweze kufikia hatua ya kuwa walipakodi wakubwa.


Meneja huyo ametoa wito kwa wafanyabiashara kujitokeza kukadiriwa mapato yao ili kuepuka changamoto wakati wa zoezi la ukaguzi barabarani.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...