Monday, August 6, 2018

Wachezaji wa Simba waikubali Coastal Union


Wachezaji wa Simba waliotolewa kwa mkopo kwenda Coastal Union ya Tanga, Moses Kitandu na Haji Ugando wameeleza kuridhishwa na mwenendo wa mazoezi chini ya kocha Juma Mgunda huku wakiahidi kuwa wapo tayari kujitoa kwaajili ya timu hiyo.

Akiongea baada ya mazoezi ya jana, mshambuliaji Haji Ugando, alisema kuwa Coastal ni timu nzuri na ina mwalimu ambaye anajua ugumu wa ligi hivyo kama mchezaji anafuata maelekezo ya kocha huku yeye binafsi akijiandaa kuhakikisha anacheza mechi zote.

Kwa upande wake Moses Kitandu ambaye msimu uliopita alikuwa mshambuliaji chaguo la pili baada ya John Bocco kwa wekundu wa msimbazi, yeye amekiri kuwa mzunguko wa ligi ni mrefu lakini amejiandaa kushirikiana na wenzake ili kuipa timu hiyo matokeo mazuri.

Kwa upande wake kocha wa timu hiyo Juma Mgunda, ameeleza kuwa kila mchezaji anajituma na kuonesha uwezo kwenye mazoezi. ''Tunafanya mazoezi mara mbili kwa siku na wachezaji wananipa imani kuwa tutashindana kwenye ligi''.

Coastal United ni miongoni mwa timu 6 ambazo zimepanda ligi kuu msimu huu. Timu hiyo ilishuka daraja msimu wa 2016/17, ikacheza ligi daraja la kwanza msimu wa 2017/18 na kufanikiwa kurejea ligi kuu na itaanza msimu wa 2018/19, Agosti 22 kwa kuikaribisha Lipuli FC.

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...