Na John Walter-Babati
Mgombea Ubunge katika Jimbo la Babati vijijini anaesubiri kuapishwa baada ya kupita bila kupingwa Daniel Sillo, amesema baada ya kuapishwa atahakikisha anashughulikia changamoto mbalimbali za jimbo hilo.
Sillo akizungumza na wananchi wa kijiji cha Loto kata ya Bermi leo Oktoba 12,2020 amesema kuwa anafahamu changamoto zinazolikabili jimbo la Babati vijijini na vilio vya wana Babati, hivyo atahakikisha zinapatiwa ufumbuzi.
Amesema kuwa anafahamu kwamba kuna changamoto ya miundombinu ya barabara ambayo ameahidi kuishughulikia kupitia Wakala wa barabara mjini na vijijini (TARURA) ambacho ni chombo kilichoundwa na serikali.
Amesema kuwa changamoto ya maji iliyopo baadhi ya vijiji Jimboni hapo atahakikisha inatatuliwa katika kipindi cha uongozi wake.
Sillo amewataka wananchi kuwabeza watu wanaopita na kusema kwamba serikali ya CCM haijafanya kitu na kuwataka kuwachagua viongozi wa CCM kwenye ngazi zote kuanzia nafasi ya Urais ambapo John Magufuli amesimama kwenye nafasi hiyo, wabunge na madiwani ili kuweza kupata utatu wa maendeleo.
Naye diwani mteule katika kata hiyo Eliuteri Bura amesema kwa kushirikiana na wananchi wa kata hiyo,watapunguza matatizo yanayowakabili wananchi.