Monday, February 18, 2019

Naibu Waziri, Kanyasu ataka ujenzi Ihumwa utumie zaidi vyuma


Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Constantine Kanyasu ametaka ujenzi wa majengo ya Wizara mbalimbali yanayojengwa katika eneo la Ihumwa  yajikite kutumia vyuma badala ya kutumia mbao ngumu ambapo kwa sasa Wizara ipo kwenye kampeni kubwa ya kuzuia matumizi ya miti hiyo ambayo ipo hatarini kutoweka

Amesema Wizara kwa sasa  imepiga marufuku  ukataji na usafirishaji wa magogo yanayozalisha mbao ngumu.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri huyo wakati alipotembelea eneo hilo kwa ajili ya kukagua hatua za ujenzi wa jengo hilo unaoendelea jijini Dodoma.

Aidha, Kanyasu ameshauri Jengo la Wizara hiyo lisitumie nguzo za mbao kwa upande wa mbele katika  sehemu ya kuingilia kama inavyoonekana kwenye ramani badala yake itumie nguzo za zege ili iweze kudumu kwa muda mrefu.

Pia, Constantine Kanyasu ametaka timu ya wataalam mbalimbali ifanye kazi kwa pamoja katika hatua za mwisho za ukamilishaji wa jengo hilo  la Wizara  katika mji wa Kiserikali wa Ihumwa.

Amesema licha ya kuwa  hatua ya ujenzi wa jengo hilo  ni ya kuridhisha ila ametaka nguvu ziongezwe ili kuweza kulikamilisha jengo hilo ndani ya muda wa wiki mbili zijazo licha ya kuwa muda uliotolewa na Waziri Mkuu, Mhe.Kassim Majaliwa tayari umeshapita.

Katika nyingine, Kanyasu ameshauri hatua za kupanda miti pamoja kuandaa bustani za maua zianze mapema katika jengo hilo ili likishakamilika liwe kwenye madhari nzuri badala ya kusubili  hadi pale jengo litakapokamilika kabisa.

Kwa upande wake, Mkandarasi wa Suma JKT, Clement Shaibu amemueleza Naibu huyo kuwa ujenzi unaendelea vizuri na wanatarajia kukamilisha ndani ya wiki mbili zijazo.
Source
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...