Friday, November 9, 2018

Mwili wa Mama Mercy Anna Mengi Wawasili Moshi

Mwili wa Mama Mercy Anna Mengi Wawasili Moshi
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Muro ameungana na Mwenyekiti Mtendaji wa Makampuni ya IPP Dkt Reginald Mengi, familia, ndugu, jamaa na marafiki kuupokea mwili wa mmoja wa waanzilishi wa makampuni ya IPP Mama Mercy Anna Mengi katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).

Mwili huo umewasili leo majira ya Saa 4 asubuhi katika uwanja wa ndege wa KIA ukitokea jijini Dar es salaam na kupelekwa nyumbani kwa marehemu maeneo ya Shanty Town ambako ibada fupi yakuombea mwili wa marehemu ilifanyika na kuongozwa na Mchungaji Meena wa Kanisa la KKKT Usharika wa Moshi Mjini.

Mchungaji Meena amesema ndugu na marafiki wanapotafakari safari ya mwisho ya Mama Mercy Anna Mengi watambue njia hiyo aliyopita kila mtu atapita hivyo jambo kubwa ni kuimarika katika imani na kuendelea kuishi katika maisha ya ushuhuda na kusaidia wengine bila kuogopa wala hofu kwakuwa Mungu atazidi kuwaimarisha.

Mwili wa mama Mercy Anna Mengi unatarajiwa kuagwa kwa mara ya mwisho hapo kesho baada ya ibada itakayofanyika katika Kanisa la KKKT usharika wa Moshi Mjini na kisha kupelekwa kuhifadhiwa kwenye nyumba yake ya milele katika mahala palipotengwa na  wanafamilia.
Source
Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...