Mhe. Samia ameuambia mkutano maalumu wa pamoja wa bunge la seneti na bunge la kitaifa nchini Kenya ustawi wa mataifa hayo mawili unaathiri ustawi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kwa pamoja.
"Kila mara panapotokea kutoelewana kati yetu tunadhoofisha uhusiano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, bila kukusudia pia tunaathiri utangamano wa Afrika Mashariki, hivyo hatuna budi kuendelea kuelewana",amesema
Rais Samia amesema kuwa kuna kipindi jumuiya hiyo ilijaribiwa kufuatia, maneno na vitendo ambavyo vilipima uimara wa dhamira za nchi wananchama wa jumuiya hiyo kuendelea na safari ya utangamano.
"Niwahakikishie, mimi na wenzangu nchini Tanzania tutahakikisha kuwa uhusiano wetu unang'ara na kwa kufanya hivyo tung'arishe uhusiano wa Afrika Mashariki. Tanzania itaendelea kuwa jirani na mbia mwaminifu wa Kenya na mwanachama muadilifu wa Afrika Mashariki," amesisitiza Rais Samia.


